RAIA WA ETHIOPIA WALIOMALIZA VIFUNGO WARUDI NCHINI KWAO – WAZIRI MAHIGA



Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga Ataka raia wa Ethiopia waliomaliza vifungo vyao warudishwe nchini kwao.

Waziri Mahiga ameyasema hayo katika ziara yake ya kikazi ya siku saba katika Mikoa ya Iringa, Njombe na Mbeya ambapo anatembelea magereza ili kuona Haki Jinai inavyotekelezwa katika mikoa hiyo.

“Hakuna sababu kwa nini raia hawa waendelee kutumia gharama kubwa ya Serikali yetu wakati wameshamaliza vifungo vyao, naahidi kuwa tutatumia kila njia kuhakikisha Serikali inatua mzigo huu”, alisema Balozi Mahiga.

Akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Ndg. Biswalo Mganga, Waziri Mahiga alianza ziara yake kwa kutembelea gereza la Wilaya ya Iringa mjini na kujionea namna Haki Jinai inavyotekelezwa katika gereza hilo.

Waziri Mahiga alizipongeza taasisi za Haki Jinai Mkoani humo kwa kuendelea kushirikiana katika kuhakikisha haki jinai inatekelezwa ipasavyo na kuepuka vitendo vya rushwa, unyanyasaji na ubambikizaji wa kesi kwa watuhumiwa.

Naye Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Ndg. Biswalo Mganga katika ziara hiyo ametumia mamlaka yake kisheria kufuta kesi 45 ambazo ziko mahakama za mwanzo na Wilaya na ameahidi kuendelea kufanya hivyo kwa kesi nyingine. Mkurugenzi Mganga alifikia uamuzi wa kufuta kesi hizo baada ya kupitia mafaili na kujiridhisha kuwa hakuna haja ya kuendelea na kesi hizo lengo ikiwa ni kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA