Katibu MKuu Katiba na Sheria Awataka TUMESHERIA Kuendeleza Watumishi Kitaaluma
Uongozi wa Tume ya
Kurekebisha Sheria Tanzania yatakiwa kuwaendeleza watumishi wake kitaaluma ili
kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuweka mpango maalum wa
kutambua mchango wa watumishi wao katika maendeleo ya Tume na Taifa kwa ujumla.
Maelekezo hayo yametolewa na
Katibu Mkuu wa Katiba na Sheria Profesa Sifuni Mchome wakati akizindua Baraza
jipya la Wafanyakazi wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania katika Mkutano wa
14 wa Baraza hilo uliofanyika jana katika ukumbi wa Mikutano wa Mamlaka ya
Hifadhi ya Ngorongoro.
“Watumishi ni rasilimali
muhimu kuliko zote kwani ndiyo inayowezesha rasilimali nyingine ziwe na
thamani, kwa maana hiyo kuna umuhimu mkubwa sana kwa Menejimenti ya Tume
kuwawezesha na kuwaendeleza watumishi
wake kitaaluma kulingana na kada zao” alisema Prof. Mchome.
Aidha, Prof. Mchome aliliasa
Baraza la Wafanyakazi la TUMESHERIA kuweka mzingira mazuri yanayomruhusu mwajiri
kuwajengea uwezo watumishi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kunakuwa na Mpango wa
Mafunzo ambao utafuatwa na kutekelezwa vizuri na kwamba, watumishi
watakaotekeleza majukumu yao vizuri, kuwepo na mpango maalumu wa kutambua
mchango wao kwa kipindi kinachokubalika ndani ya Taasisi. Kwa kujali maslahi ya
watumishi, ni dhahiri shahiri kwamba Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania
itapata matokeo chanya kutokana na kuboreka kwa utendaji na ufanisi wa
watumishi wake.
“Baraza la Wafanyakazi ni
ushahidi wa uwepo wa demokrasia mahala pa kazi kwakuwa ni chombo
kinachowashirikisha wafanyakazi kupanga, kusimamia na kutekeleza mipango mbalimabili
ikiwemo mafunzo ya watumishi hivyo ni lazima muweke mzingira mazuri
yanayomruhusu mwajiri kuwajengea uwezo watumishi wake ikiwa ni pamoja na
kuhakikisha kunakuwa na Mpango wa Mafunzo ambao utafuatwa na kutekelezwa
vizuri. Watumishi watakaotekeleza majukumu yao vizuri, hakikisheni kunakuwepo
na mpango maalumu wa kutambua mchango wao kwa kipindi kinachokubalika ndani ya
Taasisi” alisisitiza Prof. Mchome.
Aidha, Prof. Mchome amewaasa
Baraza la Wafanyakazi la TUMESHERIA kuwa mshiriki na mdau mkubwa katika kubuni
mbinu mpya za uendeshaji na kukabiliana na changamoto mbalimbali ili kuisaidia
Taasisi na Serikali kwa ujumla kuboresha maslahi wafanyakazi na uhusiano wa
kiutendaji baina ya Watumishi na Menejimenti badala ya kuwa chombo cha kupokea
malalamiko ya wafanyakazi pekee. “Mabaraza yanapaswa kusaidia kutoa suluhisho
na fursa kwa wafanyakazi kushiriki katika maamuzi mbalimbali na kuboresha
uhusiano baina ya Wafanyakazi na viongozi (menejimenti) pamoja na mazingira ya
utendaji kazi mahala pa kazi” alimalizia Katibu Mkuu huyo.
Kwa upande wake Katibu
Mtendaji wa Tume ya Kurekebisha Sheria Bw. Casmir Kyuki alisema kwamba TUMESHERIA
imefanya tathmini ya mahitaji ya mafunzo na kuandaa Mpango wa Mafunzo pamoja na
Urithishwaji wa Madaraka (Succession Plan) kwa lengo la kuwaongezea uwezo
watumishi wake na kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika kuipeleka Tanzania katika maendeleo
ya uchumi wa kati na wa viwanda.
Bwana Kyuki alifafanua
kwamba katika kipindi cha Julai hadi Desemba, 2019, watumishi saba wa kada
tofautitofauti walihudhuria mafunzo yaliyohusu kufanya manunuzi kwa njia ya
mtandao (TANEPS) na Uandaaji wa wa Mipango na Bajeti pamoja na mafunzo ya
Uandaaji wa Mfumo Mpya wa Neno Kuu (Key Word Filling Classification System) wa
utunzaji wa kumbukumbu lengo likiwa ni kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa
majukumu yao ndani ya Tume na serikali kwa ujumla.
“katika kipindi cha Julai
hadi Desemba, 2019, watumishi saba katika kada tofautitofauti walihudhuria
mafunzo ikiwa ni matokeo ya kufanya tathmini ya mahitaji ya mafunzo na kuandaa
Mpango wa Mafunzo pamoja na Urithishwaji wa Madaraka (Succession Plan) kwa
lengo la kuwaongezea uwezo watumishi wetu na kumuunga mkono Mheshimiwa Rais
Dkt. John Pombe Joseph Magufuli katika kuiletea Tanzania maendeleo ya uchumi wa
kati na wa viwanda”. Alisema Bw. Kyuki.
Mkutano wa 14 wa Baraza la
Wafanyakazi la TUMESHERIA unaofanyika kwa siku mbili katika Ukumbi wa Mikutano
wa Makao Mkuu ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na mambo mengine, mada
kuu nne zimewasilishwa na kuwapa fursa wajumbe kuzijadili na kujiongezea uwezo
na ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa mujibu wa sheria na kwa
kuzingatia agizo la Rais Na. 1 la mwaka 1970. Mada hizo ni: Umuhimu wa Maadili
katika Utumishi wa Umma; Mabadiliko yaliyotokana na Kuunganishwa kwa Mifuko ya
Pensheni; nyingine ni: Utekelezaji wa Bajeti ya Tume kwa mwaka 2019/20 na
Mwelekeo wa Bajeti ya Tume kwa mwaka wa Fedha 2020/2012 na Mwongozo wa Kuandaa
Ikama na Bajeti ya Mishahara kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 na Mabadiliko
Mbalimbali ya Miundo ya Kiutumishi.
Comments
Post a Comment