SERIKALI YAKABIDHIWA MALI ZENYE THAMANI YA ZAIDI TSH. BILIONI 58
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Balozi Augustine Mahiga akizungumza katika hafla ya Serikali kukabidhiwa mali zilizotaifishwa zenye thamani ya shilingi Bilioni 58. Wengine pichani , kushoto ni Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango na kulia ni Waziri wa Madini Mhe. Doto Biteko
Baadhi ya vipande vya dhahabu vikiwa katika begi.
Makasha yaliyohifadhi mali zilizotaifishwa zikiwemo fedha na dhahabu.
Baadhi ya Fedha zilizotaifishwa
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
SERIKALI kupitia Ofisi ya Taifa
ya Mashtaka chini ya uongozi wa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) imefanikiwa kupata
amri za kutaifisha mali mbalimbali zinazohusiana na uhalifu sambamba na fedha zilizolipwa kutokana na kesi za madini zilizopo katika
akaunti ya AFR katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zenye thamani ya zaidi ya Tsh
Bilioni 58.
Akizungumza na waandishi wa
vyombo vya habari mapema wiki hii Jijini Dar es Salaam, wakati wa makabidhiano
ya mali hizo Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP), Biswalo Mganga alisema Ofisi
yake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, imepata amri ya kutaifisha nyumba
24, magari 65, viwanja 9, mashamba 2, mbao 6894, jahazi moja (1) lililotokana na uvuvi haramu kwenye
ukanda wa bahari kuu ya Tanzania pamoja na boti moja ya Yohanda iliyohusika
katika kuingiza nchini vipodozi vyenye sumu.
‘’Kwa ufupi ukichukua thamani ya madini na
kiasi cha fedha zilizomo kwenye akaunti ya Asset Forfeiture Recovery (AFR) ya
BOT unapata Tsh 19,639,782,781.46 ambazo nakabidhi, hivyo ukijumuisha thamani
ya madini yote, fedha iliyolipwa kutokana na kesi zinazohusiana na madini
pamoja na fedha zilizomo kwenye akaunti ya AFR jumla yake inakuwa Tsh
58,604,375,783.56’’ alisema Biswalo.
Biswalo anasema tangu kuzinduliwa
rasmi kwa ofisi hiyo mwezi Agosti mwaka 2018, Ofisi yake imefanikiwa kutaifisha
jumla ya kilo 397.937 za dhahabu zenye thamani ya Tsh Bilioni 32.2 zilizokuwa
zikitoroshwa nje ya nchi na kuisababishia serikali kukosa mapato, ambapo kati
ya hizo, kilo 351.76 za dhahabu zenye thamani ya Tsh Bilioni 29
zimeshakabidhiwa kwa Katibu Mkuu Hazina ambaye ndiye mtunzaji wa mali za
Serikali.
‘’Leo hii nakabidhi jumla ya kilo
46.177 za dhahabu zenye thamani ya Tsh Bilioni 3.2, pamoja na hayo tumeendesha
kesi na kufanikiwa kupata amri za kutaifisha madini aina ya Almas, Tanzanite,
Silver, Amethyst, Rhodolite, Bati, Blue Sapphire, Spinel, Ruby, Tourmaline,
Acuamarine, ambapo jumla ya thamani ya madini yote yaliyotaifishwa pamoja na
faini zilizolipwa na washitakiwa ni Tsh Bilioni 42.2’’ alisema Biswalo.
Katika hatua nyingine, Biswalo
alisema kufuatia marekebisho ya sheria mbalimbali Na. 11 ya mwaka 2019, Ofisi
yake imeendesha kesi katika zoezi la washtakiwa kukiri makosa yao ambapo jumla
ya Tsh Bilioni 12.36 zimeshalipwa kama kodi iliyokwepwa, faini na fidia katika akaunti maalum iliyopo Benki Kuu
ya Tanzania.
Akifafanua zaidi Biswalo alisema
zoezi la urejeshaji wa fedha kwa washitakiwa 341 ambao hawajamaliza kutimiza
makubalino linaendelea na makubaliano hayo yanapaswa kutekelezwa kama
yalivyosajiliwa kwa amri ya mahakama, ambapo katika madai hayo Serikali
inawadai washitakiwa wote kiasi cha Tsh Bilioni 32.
Kwa upande wake Waziri wa Katiba
na Sheria, Dkt. Augustine Mahiga alisema wakati umefika kwa Watanzania
kunufaika kikamilifu na uwepo na rasilimali katika nchi yao ikiwemo madini
ambayo katika miaka ya nyuma hayakuwa na usimamizi madhubuti, hivyo Serikali ya
Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imejipanga
kikamilifu kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi zinaleta manufaa endelevu kwa Taifa
na wananchi wake.
Aidha Waziri wa Fedha na Mipango,
Dkt. Philip Mpango alisema zoezi la utaifishaji wa mali za uhalifu, ni dalili
tosha kuwa Tanzania sio nchi maskini na hivyo hakuna sababu ya Serikali kwenda
kukopa nje ya nchi na badala yake itaendelea kuweka mikakati madhubuti ya
kuhakikisha kuwa raslimali zake zitalindwa kwa nguvu zote hivyo kumtaka DPP na
Waziri Biteko kutoogopa vitisho badala yake wawe tayari kufa kwaajili ya
kulipigania Taifa. “kufa kwasababu ya kulipigania taifa ni heshima
itakayokumbukwa siku zote kuliko kufa kwa aibu” alimaliza Waziri Mpango.
Comments
Post a Comment