KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA KAZI YA UJENZI WA MAHAKAMA NCHINI
Baadhi
ya Mafundi wakiendelea na ujenzi wa jengo la ghorofa nne la Mahakama Kuu Kanda
ya Arusha ambalo pia litatumika kama kituo jumuishi cha utoaji haki.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakipokea maelezo kuhusu kukamilika kwa ujenzi wa jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi-Manyara.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakipokea maelezo kuhusu kukamilika kwa ujenzi wa jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi-Manyara.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga (kulia)
akizungumza jambo na Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na
Sheria Mhe. Emmanuel Mwakasaka wakati wa ziara ya Kamati hiyo ya kukagua ujenzi
wa jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Arusha.
Baadhi
ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakikagua samani
katika moja ya chumba cha Mahakama ya Wilaya ya Longido jijini Arusha.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria iliyoshirikisha
viongozi wa juu wa Wizara ya Katiba na Sheria na Mahakama wamefanya ziara ya
ukaguzi wa majengo yanayojengwa na Mahakama ya Tanzania katika Wilaya za Kondoa
mkoani Dodoma, Babati mkoani Manyara, na Longido mkoani Arusha. Aidha, ukaguzi
huo pia umefanyika katika majengo ya Mahakama Kuu ya jiji la Arusha na wiki
kesho utaedelea katika Mkoa wa Morogoro.
Katika ziara hiyo, Kamati imeonesha kuridhishwa na kazi nzuri
inayofanywa na Mahakama ya Tanzania katika maeneo yaliyotembelewa.
Akizungumza na Kitengo cha Habari na Mawasiliano Serikalini
wakati wa ziara hiyo Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na
Sheria ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Tabora mjini Mhe. Emmanuel Mwakasaka
amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli kwa uongozi wake mahili ambao ndiyo chachu ya ujenzi wa Mahakama
nyingi nchini kwa sasa. Kondoa, Manyara, Longido ambazo zimekamilika ni mfano
wa mahakama nyingi zilizojengwa na zinazoendelea kujengwa kwa kasi hapa
Tanzania.
“Kwanza tumpongeze Mhe. Rais Dkt. Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli kwa uongozi wake madhubuti katika kuhakikisha kwamba haki inapatikana
kwa haraka na kwa wakati. Kasi ya ujenzi wa majengo haya ya Mahakama ni
wakupigiwa mfano, niwapongeze sana watendaji wote wa Mahakama”, amesema
Mwakasaka.
Kwa upande wake, Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustine Mahiga
pamoja na kupongeza uzuri na ubora wa majengo ya Mahakama zote walizotembelea,
alionesha kufurahishwa na uimara wa samani zilizowekwa katika Jengo la Mahakama
ya Longido hivyo, kutoa rai kwa uongozi wa Mahakama kuzingatia utunzaji wa
samani na majengo ya mahakama zote nchini hususani zilizojengwa na zinazoendelea kujengwa.
“Hizi samani zilizowekwa katika Mahakama hii ni za kiwango
cha juu na zimetengenezwa kwa mbao zilizozalishwa hapa nchini na waliotengeneza
ni mafundi wazawa, hongereni sana watendaji wote mliohusika kutekeleza jambo
hili,” amesema Balozi Mahiga.
Ziara hii ya Kamati ya Kudumu ya Bunge katika mikoa ya
Dodoma, Manyara na Arusha imeendelea leo kwa kukagua ujenzi wa Jengo la ghorofa
nne la Mahakama Kuu ya Kanda ya Arusha ambalo imeelezwa pia litatumika kama
kituo jumuishi cha utoaji haki. Aidha, imethibitika kwamba majengo kama hili la
Mahakama Kuu ya Kanda ya Arusha yatajengwa katika mikoa ya Dodoma, Mwanza, Dar
es Salaam, Morogoro na Arusha yenyewe.
Comments
Post a Comment