OFISI ZA KATA KUTUMIKA KUSAJILI WATOTO CHINI YA UMRI WA MIAKA MITANO

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju akitoa elimu ya namna ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa Korona kwa wananchi waliofika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma kusajili wa watoto walio chini ya Miaka Mitano unaofanywa na RITA.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju akishuhudia zoezi la usajili wa watoto chini ya umri wa miaka mitano katika kituo cha usajili kilichopo katika Hospitali ya Misheni Peramiho Mkoa wa Ruvuma.

Baadhi ya Wazazi wakionesha vyeti vya kuzaliwa vya watoto wao walivyokabidhiwa na Naibu Katibu MKuu wa Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju baada ya kufanikiwa kuwasajili watoto wao.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini RITA umefanya maboresho ya mfumo wa usajili kuwezesha Vituo vya Afya pamoja ofisi za kata vitumike kuwasajili watoto na kupatiwa cheti cha kuzaliwa.

Hayo yameelezwa jana na Msajili wa Vizazi na Vifo na Mratibu wa zoezi la Usajili wa Watoto walio chini ya umri wa miaka mitano Mkoa wa Ruvuma Bwn Jonathan Magoti wakati akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya zoezi hilo mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bwana Amon Mpanju aliyetembelea Mkoa wa Ruvuma kujionea maendeleo ya usajili wa watoto hao.

Bwn. Magoti alieleza kuwa wameshapeleka maboresho hayo katika mikoa 16 ukiwemo mkoa wa Ruvuma baada ya kupitishwa na Bunge na kurasmisha kuwa usajili unaweza kufanyika katika Ofisi za Kata na Vituo vya Afya kwa lengo la kuhakikisha huduma hizi zinafikika kiurahisi na wananchi.

“Hapo awali maboresho haya yalikuwa yakifanyika kwa kutumia Hati ya makubalinao baina ya Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Rais Tamisemi na Wizara ya Afya lakini sasa Bunge limeshapitisha na kurasimisha kuwa usajili unaweza kufanyika katika Ofisi za Kata na Vituo vya Afya baada ya kupitia marekebisho ya sheria mbambali Na.4 ya mwaka 2019” alisema Magoti.

Kwa upande wake Kaimu Kabidhi Wasii Mkuu wa RITA Bi Emmy Hudson alisema kuwa maboresho ya ughatuaji wa mamlaka kutoka Serikali kuu kwenda Serikali za mitaa umerahisisha hatua za usajili kutoka hatua mbili hadi moja kwani hapo awali mtoto alipatiwa uthibitisho wa kizazi yaani tangazo na baadae kwenda ofisi ya mkuu wa wilaya kupata cheti lakini sasa mtoto hupatiwa cheti papo hapo na bila ya malipo.

“Uboreshwaji huu wa usajili wa watoto umesaidia Serikali na wadau mbalimbali kupata takwimu sahihi na kwa wakati ambazo zimekuwa zikitumika katika mipango ya maendeleo katika sekta mbalimbali nchini kama vile afya na elimu” alisisitiza Emmy Hudson.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju pamoja na kuupongeza uongozi wa RITA chini Mtenaji Mkuu wake Bi Emmy Hudson kwa kazi nzuri wanayofanya ya kupanua huduma ya usajili wa watoto chini ya umri wa miaka mitano kufikia mikoa 16 sasa, amewaasa kuendelea kuchukua tahadhari na kujikinga na ugonjwa wa Korona unaoitesa dunia kwa sasa.

“Ili tusikinzane na maelekezo ya serikali ya kujikinga na kuzuia maambukizi ya ugonjwa wa Korona, lazima muhakikishe kwamba watu wanakuja kujisajili kwa awamu na kwa kupeana muda maalumu ili kuzuia milundikano ya watu, wazazi wafike kwenye vituo kwa kutofautiana muda na wakae mbali mbali muda wote wawapo katik vituo vya usjili”. Alisema Mpanju.

Aidha, Amon Mpanju aliongea na wazazi waliojitokeza katika vituo vyote alivyotembelea na kuwasisitiza kufuata maelekezo yote yanayotolewa na serikali juu ya namna ya kujikinga na kuzuia maambukizi ya ugonjwa wa Korona popote watakapokuwa, ikiwa ni pamoja na kunawa mikono na sabuni kwa kutumia maji yanayotiririka, kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima pamoja na kuzingatia yote yanayoelezwa na serikali kupitia vyombo vya habari.

Usajili katika mkoa wa Ruvuma ulianza rasmi tarehe 20/03/2020 baada ya jumla ya watoa huduma 102 kupatiwa mafunzo ya ngazi ya taifa na mkoa na kula viapo vya uadilifu kuwa wanaenda kufanya kazi kwa nguvu na umakini wa hali ya juu kama walivyofundishwa. Mafunzo hayo yaliyoanza 09/03/2020 na kuhitimishwa tarehe 14/03/2020 mkoani Ruvuma yalilenga kuwaongezea uwezo maafisa hao ili waweze kutekeleza jukumu la usajili wa watoto kwa ufanisi ambapo kwa siku nne pekee wameweza kusajli watoto 37,544 kati ya watoto 242,000 sawa na asilimia 19.




Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA