KATIBU MKUU KATIBA NA SHERIA AWATAKA POLISI, MAGEREZA KUHAKIKISHA HAKI ZA MTOTO ZINALINDWA NA KUHIFADHIWA
Katibu Mkuu Wizara ya katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome
(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo ya siku nne kwa
maafisa wa Jeshi la Polisi na Magereza kutoka katika mikoa ya Iringa na Mbeya
kuhusu utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria kwa watoto jana katika ukumbi wa
Mahakama ya Tanzania Kanda ya Mbeya- jijini
Washiriki wa Mafunzo ya siku nne kuhusu utoaji wa huduma ya
msaada wa kisheria kwa watoto jana katika ukumbi wa Mahakama ya Tanzania Kanda
ya Mbeya- jijini
Katibu Mkuu Wizara ya katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku nne kwa maafisa wa Jeshi la Polisi na Magereza kutoka katika mikoa ya Iringa na Mbeya kuhusu utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria kwa watoto jana katika ukumbi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Mbeya- jijini Mbeya.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
SERIKALI imewataka Polisi na
Magereza nchini kuhakikisha haki na maslahi ya mtoto anayekinzana na sheria zinalindwa
na kuhifadhiwa kwa kuhakikisha kuwa shauri linalomhusu linapewa kipaumbele na
linashughulikiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa
Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome wakati akifungua Mafunzo ya siku
nne kwa maafisa wa Jeshi la Polisi na Magereza kutoka katika mikoa ya Iringa na
Mbeya kuhusu utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria kwa watoto jana katika
ukumbi wa Mahakama ya Tanzania Kanda ya Mbeya- jijini Mbeya.
Prof. Mchome amesema Wizara kwa
kushirikiana na wadau, kama vile UNICEF na wengine, imeendelea kuzingatia
maslahi ya mtoto anayekinzana na sheria kwa kuhakikisha kuwa shauri linalomhusu
linapewa kipaumbele na linashughulikiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto.
“Ni rai yangu kuwa mnapokabiliana
na kesi za watoto hakikisheni mtoto anapata msaada wa kisheria mara unapokutana
naye au kusikia habari zake. Kwa kuwa mtakutana na watoto wa namna hii,
ninaomba mafunzo haya yawakumbushe wajibu wenu katika kumhudumia mtoto huyu ili
haki itendeke kwa wakati.”
Hivi karibuni, Mhe. Jaji Mkuu
alitoa Kanuni za ushughulikiaji wa mashauri yanayohusu watu wenye mahitaji
maalum, wakiwamo watoto. Kanuni hizo zinaweka masharti ya kuhakikisha
upelelezi, uendeshaji na utoaji wa hukumu kwa mashauri ya watoto unafanyika kwa
wakati kutokana na changamoto zilizopo katika mashauri hayo amesisitiza Prof.
Mchome.
Aidha, Prof. Sifuni Mchome ametaja
hatua za zilizochukuliwa na Serikali katika kuboresha mfumo wa haki jinai kuwa
ni marekebisho ya sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20 kwa kuweka
utaratibu wa kufifisha makosa na kuimarisha mfumo wa upatanishi katika makosa
ya jinai kwa lengo la kupunguza mrundikano wa mashauri Mahakamani na kuondoa
msongamano wa mahabusu na wafungwa katika vituo vya polisi na magereza, hivyo
kuwataka mafisa wa polisi na Magereza kuzitumia njia hizo.
“Ninyi mnaopatiwa mafunzo haya
mnapaswa kuwa mabalozi kuonesha mfano kwa kuzitumia njia hizi kwani zipo kwa
mujibu wa sheria kuwezesha mfumo huo kufanya kazi kwa mujibu wa Sheria.
Kutokana na Wizara yangu kusimamia masuala ya utoaji wa huduma ya msaada wa
kisheria na mfumo wa haki jinai, ni imani yetu kuwa, kama wadau wakubwa,
mtaitumia fursa hii kujitathimini na kushiriki kujenga mfumo wa utoaji haki
wenye tija usio na malalamiko kwa wananchi.”
Akiwashukuru UNICEF kwa jitihada
kubwa wanazofanya katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha haki za
mtoto zinalindwa na kuhifadhiwa Prof. Mchome amesema Serikali imejipanga
kuhakikisha inatatua changamoto zinazomkabili mtoto anayekinzana na sheria
katika maeneo mbalimbali nchini. Aidha, Wizara ya Katiba na Sheria, kwa
kushirikiana na UNICEF pamoja na wadau wa haki mtoto, imeandaa Mkakati wa Haki Mtoto ambao hivi
karibuni utazinduliwa. Mkakati huu unalenga kuhakikisha kuwa wadau wa masuala
ya mtoto wanafanya kazi kwa pamoja katika kusimamia masuala ya haki mtoto.
“Moja ya wadau wakubwa katika
mkakati huu ni Jeshi la Polisi na Magereza ambapo jukumu lenu ni kubwa mno
katika masuala ya haki mtoto. Mkakati huu unawalenga watoto wote walioathirika
na ukatili wa kijinsia, waliotenda makosa au kujikuta kizuizini kutokana na
mzazi kutenda kosa.”
Ni wazi kwamba Mkakati huu kitakuwa
chombo kinachoaminika na sehemu salama kwa mtoto tofauti na ilivyo sasa ambapo
kumekuwa na malalamiko ya watoto kupewa umri mkubwa tofauti na uhalisia,
amesisitiza Prof. Mchome.
“Ni rai yangu kwamba Wadau wote
tutashirikiana katika kuhakikisha ulinzi na ustawi wa mtoto linakuwa ni jukumu
letu la msingi. Hivyo, nawahimiza kwa mara nyingine kujaribu kutumia njia
mbadala za kushughulikia masuala yanayohusu haki za mtoto badala ya kujielekeza
katika kuwaweka vituoni au magereza jambo linalosababisha msongamano.”
Mwaka 2017 Wizara ya Katiba na
Sheria ilisimamia mchakato wa kutunga na kupatikana kwa sheria ya Msaada wa
Kisheria Na 1 ya 2017. Pamoja na mambo mengine, Sheria hiyo ina lengo la kutoa
huduma ya msaada wa kisheria kwa watu wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za
Mawakili. Aidha, sheria hii imeweka masharti ya kutoa msaada wa kisheria katika
mashauri ya jinai. Ni kwa muktadha huo, Wizara ya Katiba na Sheria iliingia
makubaliano na Wizara ya Mambo ya Ndani mwaka 2018 kuhusu utekelezaji wa
masuala ya msaada wa kisheria katika vituo vya Polisi na magereza nchini.
Comments
Post a Comment