WAZIRI DKT. MWIGULU NCHEMBA AWASILISHA TAARIFA KATIKA KIKAO CHA 66 CHA TUME YA AFRIKA YA HAKI ZA BINADAMU NA WATU


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba amewasilisha taarifa juu ya Haki za Binadamu na za Watu Barani Afrika na ugonjwa wa covid- 19 katika Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu.

Taarifa hii imewasilishwa kwa njia ya njia ya kikao cha mtandao (video conference) kwa washiriki waliopo Banjul, Gambia Julai 13, 2020.

Katika taarifa hiyo Waziri Nchemba amesema ugonjwa wa covid -19 sio tu ni janga la kiafya bali pia ni la kiuchumi na kijamii.

Katika kukabiliana na ugonjwa huu nchi ya Tanzania inakabiliana nao kwa kutofunga mipaka ya nchi na kuendelea na shughuli za uzalishaji mali huku wananchi wakipewa elimu na kusisitizwa kufuata njia za kujikinga na maambukizi ya virusi hivyo.

 Njia zinazotumika kukabiliana na covid-19 ni pamoja na kutumia dawa za asili katika kuimarisha kinga ya mwili na pia kujifukiza kwa kutumia  majani ya miti mbalimbali maarufu kama nyungu ili kupambana na ugonjwa huo.

Vilevile, Wananchi wameelimishwa kuondoa hofu mara wapatapo maambukizi ya virusi hivyo na badala yake kukabiliana navyo kwa kutumia dawa wanazoelekezwa na wataalam wa afya, na pia kuepuka misongamano, kuosha mikono mara kwa mara, na kuvaa barakoa bila kusahau kumuomba Mungu kwa imani zao.

Serikali ina uelewa wa kutosha juu ya hatari ya virusi vya covid-19 na umuhimu wa kuchukua tahadhari na tumejiridhisha na njia tulizochukua katika kukabiliana nao.

Ugonjwa huo ulipogundulika Tanzania kwa mara ya kwanza tarehe 16 Machi, 2020 Serikali ilichukua hatua za haraka kuwaelimisha wananchi kutotembelea nchi zilizoathirika, kujiweka karantini kwa siku 14 kwa wasafiri wote waingiapo nchini, kusitisha sherehe za kitaifa ikiwemo maadhimisho ya siku ya Muungano, kufunga shule na vyuo na kisitisha michezo mbalimbali ilim kupunguza maambukizi zaidi.

Aidha, Wizara ya afya imekuwa ikitoa elimu ya kujikinga na ugonjwa huo kwa taasisi mbalimbali za Serikali na elimu zaidi iliendelea kutolewa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na vipeperushi.

Waziri Nchemba alisema sekta ya afya imepanga mikakati mbalimbali katika kukabiliana na ugonjwa wa covid-19 ikiwemo kupeleka mahitaji  ya muhimu kwa watoa huduma za afya, kuongeza idadi ya madaktari na watoa huduma za afya, ushauri ulitolewa kwa wananchi kuhusu kutumia dawa za asili na sio kutegemea dawa za kisasa pekee na pia taasisi za utafiti wa dawa asilia zimeimarishwa.

Vilevile aliongeza kuwa Serikali imefungua maabara mpya yenye mashine 5 zenye uwezo wa kupima sampuli 1,800 kwa siku ambapo wahudumu 1,000 wa afya walipata ajira katika maabara hizo.

Aidha, Serikali imemuagiza Wakala wa Ugavi wa maji na usafi wa mazingira kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuhakikisha maji yanapatikana na kuweka vifaa vya kunawia mikono maeneo mbalimbali.

Mbali na hayo,upatikanaji wa haki umeendelea kuzingatiwa katika kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa covid-19. Wafungwa na mahabusu kadhaa waliachiwa ili kupunguza msongamano magarezani na kamati za afya za mikoa na wilaya  zilianzishwa ili kukabiliana na ugonjwa huo magerezani.

Katika taarifa hiyo Waziri Nchemba amesema Kwa sasa Tanzania imeanza kurudi katika maisha ya kawaida ambapo shule, vyuo, shughuli za utalii na michezo imefunguliwa huku wananchi wakiendelea kusisitizwa kuchukua tahadhari za kujikinga na covid-19.

Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA