KASI YA MAENDELEO YATAJWA KUWA KICHOCHEO CHA AMANI NCHINI
Kasi ya maendeleo yatajwa kuwa kichocheo cha amani nchini.
Hayo yamesemwa na Mkuu
wa Wilaya ya Sumbawanga Dkt. Khalfan Haule alipotembelewa na Kamati ya Kitaifa
ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari ofisini kwake leo.
Dkt. Haule ametaja
mafanikio yaliyofanywa na Rais wa Awamu ya Tano Mhe. Dkt. John Joseph Pombe
Magufuli katika Sekta za Afya, Elimu, Barabara, Umeme, Maji na upatikanaji haki
kwa wakati kuwa ni kichocheo cha ujenzi wa amani na utulivu hapa nchini.
"Huduma za jamii
kama maji, elimu, umeme, afya, usafiri na usafirishaji ni haki ya msingi ya
kila mwananchi. Naipongeza Serikali yangu chini ya Rais wetu mpendwa Dkt. John
Joseph Pombe Magufuli kwa kuyapa kipaumbele masuala haya muhimu katika ujenzi
wa amani na uchumi wa Taifa kwa kwa ujumla" amesema Dkt Haule.
Mwananchi akipata haki
ya maendeleo kwa kuboreshewa na kusogezewa karibu huduma za jamii na nyingine
hawezi kujihusisha na migogoro yoyote katika jamii kwani akili yake inakuwa
imetulia, hivyo kujielekeza katika kufanya shughuli za maendeleo na kujipatia
kipato, ameongeza Dkt. Haule.
Hata hivyo, Dkt. Haule
ameiomba Serikali kuendelea kuweka mkazo na juhudi katika kuhakikisha huduma za
jamii zinawafikia wananchi wote katika maeneo yao kama inavyojieleza katika
Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020/2025.
Kwa upende wake Katibu
wa Kamati ya Kitaifa ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari Bwn. Miraji
Magai Maira wakati akimshukuru Mkuu huyo wa Wilaya ya Sumbawanga amesema
wanalazimika kufika kwa wananchi na kukutana na makundi mbalimbali ya vinaja,
wafugaji, wakulima, Walemavu, viongozi wa Mira na viongozi wa dini kwasababu
huko ndiko migogoro inakoanzia na isiposhughulikiwa kwa wakati huhatarisha
amani ya nchi.
Kamati ya Kitaifa ya
Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari iliyoanzishwa Februari, 2012 chini
ya itifaki ya Kuzuia Mauaji ya Kimbari na kuridhiwa na serikali ya Tanzania
kupitia Mkataba wa nchi za Maziwa Makuu wa Usalama, Utulivu na Maendeleo
itaendelea na mkakati wa utekelezaji wa majukumu yake ya msingi ya kujenga na
kudumisha amani na utengamano kwa kufanya vikao vya ujenzi wa amani kwa siku
mbili katika mkoa wa Rukwa, Wilaya ya Sumbawanga na baadae kumalizia vikao
hivyo mkoani Morogoro.
Comments
Post a Comment