MAADILI KWA WATUMISHI WA UMMA NI TIBA YA AMANI NCHINI
Usimamizi thabiti wa maadili kwa watumishi wa umma katika kata
na vijiji mkoani Morogoro umetajwa kuwa sababu ya kupunguza migogoro kati ya
wakulima na wafugaji.
Hayo yamesemwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Eng.
Emmanuel N.M. Kalobelo alipotembelewa ofini kwake leo na Kamati ya Kitaifa ya
Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari.
Eng. Kalobelo amesema ukosefu wa maadili kwa watendaji wa kata
na vijiji umeonekana kuwa kichocheo cha migogoro na uvunjifu wa amani katika
maeneo mengi nchini lakini Serikali chini ya Mhe. Rais Dkt. John Joseph Pombe
Magufuli imefanya kazi kubwa ya kulikomesha tatizo hilo mkoani Morogoro.
"Siku za nyuma Mkoa wa Morogoro ulikuwa kati ya mikoa yenye
migogoro mingi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji lakini baada ya kufanya
utafiti wa kina tukagundua watendaji na viongozi wa kata na vijiji walikuwa
ndiyo chanzo kwani waliidhinisha uuzaji wa maeneo yasiyopimwa bila kufuata
taratibu sahihi." Amesema Eng. Kalobelo.
Baada ya kubaini kinachofanyika na watendaji hao, Serikali ya
Mkoa kwa kushirikiana na wananchi wa maeneo husika tumesimamia kwa nguvu
maadili kwa kutumia mbinu mbalimbali kwa mafanikio na sasa wanafanya kazi zao
kiweledi jambo lililopunguza tatizo kwa kiasi kikubwa.
Aidha Katibu Tawala huyo wa Mkoa wa Morogoro amesema wameendelea
kushughulikia na kusimamia upimaji wa ardhi pamoja na ugawaji wa maeneo husika
ikiwa ni pamoja na kutenga maeneo ya wakulima na wafugaji kupunguza migogoro ya
ardhi katika mkoa huo na Wilaya zake.
"Kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
tumeanzisha Ofisi ya kusimamia Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ulisaidia
kupima maeneo na kusimamia ugawaji wake kwa kuyatenganisha ili wakulima wawe na
maeneo yao na wafugaji pia wawe na maeneo yao, mpango huu umesaidia kuzuia muingiliano
wa shughuli za kilimo na ufugaji." Ameongeza Eng. Kalobelo.
Kamati hii ya Kitaifa ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya
Kimbari iliundwa mwezi Februari, 2012 chini ya Itifaki ya Kuzuia Mauaji
ya Kimbari iliyoridhiwa na Serikali ya Tanzania kupitia Mkataba wa nchi
za Maziwa Makuu wa Usalama, Utulivu na Maendeleo (The Pact on Security,
Stability and Development in the Great Lakes Region).
Kamati hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wake Felistas Mushi wa
Wizara ya Katiba na Sheria inaundwa na Wataalamu wanne ambao ni Miraji Magai
Maira wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere ambaye pia ni Katibu wa Kamati, Saleh
Ambika wa Wizara ya Mambo ya Ndani (Jeshi la Polisi), Lina Kitosi kutoka Ofisi
ya Waziri Mkuu na Pius Katani kutoka Ofisi ya Rais Ikulu.
Kamati hiyo ya watalaamu watano imefika Ofisi ya Mkuu wa
Mkoa wa Morogoro na kuonana na Katibu Tawala Eng. Emmanuel Kolobelo kabla ya
kuelekea Mvomero kukagua utekelezaji wa masuala ya Ujenzi wa Amani inayohusisha
rasilimali na hatimaye kusababisha mapigano na hata mauaji kati ya wakulima na
wafugaji, wawekezaji na wananchi na wakati mwingine wananchi wenyewe kwa
wenyewe.
Comments
Post a Comment