MAADILI KWA WATUMISHI WA UMMA NI TIBA YA AMANI NCHINI





 XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Usimamizi thabiti wa maadili kwa watumishi wa umma katika kata na vijiji mkoani Morogoro umetajwa kuwa sababu ya kupunguza migogoro kati ya wakulima na wafugaji.

 

Hayo yamesemwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Eng. Emmanuel N.M. Kalobelo alipotembelewa ofini kwake leo na Kamati ya Kitaifa ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari.

 

Eng. Kalobelo amesema ukosefu wa maadili kwa watendaji wa kata na vijiji umeonekana kuwa kichocheo cha migogoro na uvunjifu wa amani katika maeneo mengi nchini lakini Serikali chini ya Mhe. Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli imefanya kazi kubwa ya kulikomesha tatizo hilo mkoani Morogoro.

 

"Siku za nyuma Mkoa wa Morogoro ulikuwa kati ya mikoa yenye migogoro mingi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji lakini baada ya kufanya utafiti wa kina tukagundua watendaji na viongozi wa kata na vijiji walikuwa ndiyo chanzo kwani waliidhinisha uuzaji wa maeneo yasiyopimwa bila kufuata taratibu sahihi." Amesema Eng. Kalobelo.

 

Baada ya kubaini kinachofanyika na watendaji hao, Serikali ya Mkoa kwa kushirikiana na wananchi wa maeneo husika tumesimamia kwa nguvu maadili kwa kutumia mbinu mbalimbali kwa mafanikio na sasa wanafanya kazi zao kiweledi jambo lililopunguza tatizo kwa kiasi kikubwa.

 

Aidha Katibu Tawala huyo wa Mkoa wa Morogoro amesema wameendelea kushughulikia na kusimamia upimaji wa ardhi pamoja na ugawaji wa maeneo husika ikiwa ni pamoja na kutenga maeneo ya wakulima na wafugaji kupunguza migogoro ya ardhi katika mkoa huo na Wilaya zake.

 

"Kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi tumeanzisha Ofisi ya kusimamia Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ulisaidia kupima maeneo na kusimamia ugawaji wake kwa kuyatenganisha ili wakulima wawe na maeneo yao na wafugaji pia wawe na maeneo yao, mpango huu umesaidia kuzuia muingiliano wa shughuli za kilimo na  ufugaji." Ameongeza Eng. Kalobelo.

 

Kamati hii ya Kitaifa ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari iliundwa mwezi  Februari, 2012 chini ya Itifaki ya Kuzuia Mauaji ya Kimbari  iliyoridhiwa na Serikali ya Tanzania kupitia Mkataba wa nchi za Maziwa Makuu wa Usalama, Utulivu na Maendeleo (The Pact on Security, Stability and Development in the Great Lakes Region).

 

Kamati hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wake Felistas Mushi wa Wizara ya Katiba na Sheria inaundwa na Wataalamu wanne ambao ni Miraji Magai Maira wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere ambaye pia ni Katibu wa Kamati, Saleh Ambika wa Wizara ya Mambo ya Ndani (Jeshi la Polisi), Lina Kitosi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu na Pius Katani kutoka Ofisi ya Rais Ikulu.

 

Kamati hiyo  ya watalaamu watano imefika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na kuonana na Katibu Tawala Eng. Emmanuel Kolobelo kabla ya kuelekea Mvomero kukagua utekelezaji wa masuala ya Ujenzi wa Amani inayohusisha rasilimali na hatimaye kusababisha mapigano na hata mauaji kati ya wakulima na wafugaji, wawekezaji na wananchi na wakati mwingine wananchi wenyewe kwa wenyewe.

 

 


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA