MAZUNGUMZO YA AMANI YATAJWA KUWA NJIA BORA NA SALAMA YA UTATUZI WA MIGOGORO NCHINI.




 
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Mazungumzo ya amani ni muarobaini uliothibitika kutumika kama tiba ya migogoro ya ardhi Mvomero Mkoani Morogoro.

 

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe. Albinus Mgonya wakati akitoa taarifa ya hali ya amani wilayani humo kwa Kamati ya Kitaifa ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari iliyofika walayani kwake hivi karibuni.

 

Wakulima na wafugaji ni watanzania wanaoishi pamoja na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za kijamii, kisiasa na kiuchumi katika maeneo wanaoishi na zaidi, wengi wao ni wakulima na ni wafugaji kwa wakati mmoja hivyo njia ya mazungumzo ya amani imejipambanua kuwa tiba ya utatuzi wa migogoro inayowakabili.

 

"Unajua, hawa wakulima na wafugaji wanafahamiana kwasababu wanaishi pamoja, matumizi ya nguvu hususani vyombo vya ulinzi na usalama isingekuwa muarobaini, badala yake kwa kuwakutanisha na kuzungumza nao kumeonesha kuwa ni suluhisho la migogoro na ujenzi wa amani na utulivu baina yao."

 

Kwa niaba ya wakulima na wafugaji ndugu Moringe Kwinasei ameungana na Mkuu huyo wa Wilaya kwa kuthibitisha hali ya uwepo wa utulivu na amani uliotokana na utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo ya amani na kuwataka wakulima na wafugaji kuacha tabia ya uchochezi kwa kisingizio cha migogoro baina yao.

 

"Unajua sisi ni ndugu na wote tunahitajiana katika mambo mengi ikiwemo mazao ya mifugo na mimea ambayo ndiyo yanatugombanisha, tunagombana shambani baadae tunakaa hotelini tunakula wali-nyama! sasa kwanini tuendelee kugombania mambo ambayo ni sehemu ya mahitaji yetu muhimu? Ameongeza kwa kuuliza Martine Matingise.

 

Aidha, Mhe. Mgonya amesema Wilaya yake imeanzisha programu ya michezo mbalimbali hasa mashindano ya mipira wa Miguu kati ya Wakulima na wafugaji,  mbinu hii imeonesha kuwa na tija katika ujenzi wa amani katika Wilaya hiyo kwasababu michezo imewaleta wakulima na wafugaji pamoja na kuishi kwa upendo.

 

"Nimeanzisha na kuhamisisha michezo mbalimbali hasa mpira wa Miguu kati ya wakulima na wafugaji, na nimekuwa nikishiriki nao katika michezo husika. Kwakweli njia hii pia imeonesha mafanikio makubwa katika jitihada za Serikali katika ujenzi wa amani na kuzuia migogoro katika jamii." Amemaliza Mhe. Mgonya.

 

Kamati hii imehitimisha ziara yake ya utekelezaji wa majukumu muhimu ya Ujenzi wa Amani na Kuzuia Mauaji ya Kimbari katika Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro baada ya kufanya kazi kama hiyo katika Mikoa ya Arusha, Manyara na Rukwa.

 


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA