WATANZANIA TUWE NA UTAMADUNI WA KUANDIKA WOSIA KUEPUKA CHANGAMOTO ZA MIRATHI- JAJI MRUMA
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Tanga Mhe. Jaji Amir Mruma amesema watanzania
tuwe na utamaduni wa kuandika wosia kwani suala la usimamizi wa mirathi huwa
linakuwa rahisi sana pale kunapokuwa na wosia wa marehemu kuhusu mgawanyo wa
mali zake pindi atakapoondoka duniani.
“Mara nyingi wosia
umekuwa ukirahisisha na kuondoa migogoro ya umiliki wa mali za marehemu na pia
umekuwa ukibainisha nani atasimamia mali hizo kwa maendeleo ya familia husika”
alisema Jaji Mruma.
Jaji Mruma ameyasema
hayo wakati akizindua rasmi Maadhimisho ya Wiki ya Msaada wa Kisheria
yanayofanyika kitaifa Mkoani Tanga kuanzia tarehe 12 hadi 18 Novemba, 2020
yakilenga kupunguza changamoto za kisheria kwa wananchi.
Mhe. Jaji Mruma alisema
kwa utafiti walioufanya baada ya kukaa muda mrefu mahakamani wamegundua
changamoto kubwa zaidi ya mirathi katika jamii inasababishwa na familia nyingi
kutoandika wosia mapema kabla ya kufariki.
Aliongeza kuwa
usimamaizi bora wa mirathi ni ule ambao unalenga kuleta manufaa na maendeleo
kwa walengwa wa mali zilizoachwa na marehemu na si kumnufaisha msimamizi ambaye
si mke au mume au mtoto wa marehemu.
Alisema “Wajane na watoto
yatima wamekuwa wahanga wakubwa na wamedumbukia kwenye dimbwi la umasikini
kutokana na baadhi ya wasimamizi au watu wasiohusika katika usimamiaji
kujinufaisha na mali hizo jambo ambalo linaleta umasikini kwa baadhi ya
familia”
Alisisitiza “usimamizi
bora wa mirathi una muda mahsusi wa kuifunga mirathi husika na unabainisha mali
itagawanywa au kuuzwa na warithi kugawana mali husika ili waweze kujiendeleza
nayo”
Vilevile, Jaji Mruma
alitoa rai kwa watoa elimu waliopangwa kuhudumia wananchi katika maadhimisho
hayo wajue kuwa eneo hilo ni muhimu na linagusa wananchi wengi hivyo wanapaswa
kutoa elimu na ushauri ipasavyo.
Naye Naibu Katibu Mkuu
wa Wizara ya Katiba na Sheria Ndg. Amon Mpanju alisema Wizara hiyo inalengo la
kutatua kero za wananchi hususan za kisheria ili kupunguza mashauri kwenye
mfumo wa upatikanaji haki, hivyo Wizara ya Katiba na Sheria inahakikisha elimu
inawafikia wanachi popote walipo ili kujua haki zao na namna gani wanaweza
kuzifikia.
Aidha, Msajili wa Watoa
Huduma za Kisheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bi . Felistas Joseph
alisema Wizara na wadau wake wameamua kubadili mtindo wa kutoa huduma ya msaada
wa kisheria kwa kuangalia upande mmoja wa wananchi peke yake na badala
yake kujenga uwezo wa upande wa pili ili
wahitaji na watoaji wote wawe na uelewa wa masuala ya kisheria lakini pia uwezo
wa kutatua kero hizo.
Bi. Felistas alisema “
katika mafunzo haya kutakuwa na makundi mbalimbali kuanzia ngazi ya kata,
wilaya na Mkoa ambapo mada mbalimbali zitatolewa na wataalamu kutoka Wizara
mbalimbali, Chama cha Wanasheria Tanganyika na Mashirika yanayotoa msaada wa
kisheria”.
Aliongeza kuwa mafunzo
hayo yanayofanyika Mikoa yote Tanzania Bara yanaenda sambamba na utoaji wa
huduma ya msaada wa kisheria katika mikoa hiyo.
Maadhimisho haya
yanaratibiwa na kusimamiwa na Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kwa
mara ya nne tangu kupewa mamlaka hayo chini ya sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka
2017.
Comments
Post a Comment