WATANZANIA TUWE NA UTAMADUNI WA KUANDIKA WOSIA KUEPUKA CHANGAMOTO ZA MIRATHI- JAJI MRUMA

 




XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Tanga Mhe. Jaji Amir Mruma amesema watanzania tuwe na utamaduni wa kuandika wosia kwani suala la usimamizi wa mirathi huwa linakuwa rahisi sana pale kunapokuwa na wosia wa marehemu kuhusu mgawanyo wa mali zake pindi atakapoondoka duniani.

“Mara nyingi wosia umekuwa ukirahisisha na kuondoa migogoro ya umiliki wa mali za marehemu na pia umekuwa ukibainisha nani atasimamia mali hizo kwa maendeleo ya familia husika” alisema Jaji Mruma.

Jaji Mruma ameyasema hayo wakati akizindua rasmi Maadhimisho ya Wiki ya Msaada wa Kisheria yanayofanyika kitaifa Mkoani Tanga kuanzia tarehe 12 hadi 18 Novemba, 2020 yakilenga kupunguza changamoto za kisheria kwa wananchi.

Mhe. Jaji Mruma alisema kwa utafiti walioufanya baada ya kukaa muda mrefu mahakamani wamegundua changamoto kubwa zaidi ya mirathi katika jamii inasababishwa na familia nyingi kutoandika wosia mapema kabla ya kufariki.

Aliongeza kuwa usimamaizi bora wa mirathi ni ule ambao unalenga kuleta manufaa na maendeleo kwa walengwa wa mali zilizoachwa na marehemu na si kumnufaisha msimamizi ambaye si mke au mume au mtoto wa marehemu.

Alisema “Wajane na watoto yatima wamekuwa wahanga wakubwa na wamedumbukia kwenye dimbwi la umasikini kutokana na baadhi ya wasimamizi au watu wasiohusika katika usimamiaji kujinufaisha na mali hizo jambo ambalo linaleta umasikini kwa baadhi ya familia”

Alisisitiza “usimamizi bora wa mirathi una muda mahsusi wa kuifunga mirathi husika na unabainisha mali itagawanywa au kuuzwa na warithi kugawana mali husika ili waweze kujiendeleza nayo”

Vilevile, Jaji Mruma alitoa rai kwa watoa elimu waliopangwa kuhudumia wananchi katika maadhimisho hayo wajue kuwa eneo hilo ni muhimu na linagusa wananchi wengi hivyo wanapaswa kutoa elimu na ushauri ipasavyo.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Ndg. Amon Mpanju alisema Wizara hiyo inalengo la kutatua kero za wananchi hususan za kisheria ili kupunguza mashauri kwenye mfumo wa upatikanaji haki, hivyo Wizara ya Katiba na Sheria inahakikisha elimu inawafikia wanachi popote walipo ili kujua haki zao na namna gani wanaweza kuzifikia.

Aidha, Msajili wa Watoa Huduma za Kisheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bi . Felistas Joseph alisema Wizara na wadau wake wameamua kubadili mtindo wa kutoa huduma ya msaada wa kisheria kwa kuangalia upande mmoja wa wananchi peke yake na badala yake  kujenga uwezo wa upande wa pili ili wahitaji na watoaji wote wawe na uelewa wa masuala ya kisheria lakini pia uwezo wa kutatua kero hizo.

Bi. Felistas alisema “ katika mafunzo haya kutakuwa na makundi mbalimbali kuanzia ngazi ya kata, wilaya na Mkoa ambapo mada mbalimbali zitatolewa na wataalamu kutoka Wizara mbalimbali, Chama cha Wanasheria Tanganyika na Mashirika yanayotoa msaada wa kisheria”.

Aliongeza kuwa mafunzo hayo yanayofanyika Mikoa yote Tanzania Bara yanaenda sambamba na utoaji wa huduma ya msaada wa kisheria katika mikoa hiyo.

Maadhimisho haya yanaratibiwa na kusimamiwa na Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kwa mara ya nne tangu kupewa mamlaka hayo chini ya sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka 2017.

 

 

 


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA