SHERIA, MWENENDO WA MASHAURI NA HUKUMU ZIANDIKWE KWA LUGHA YA KISWAHILI – DKT MWIGULU NCHEMBA
Waziri wa katiba na Sheria
Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akisisitiza jambo wakati akizungumza na Menejimenti ya
Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (Law School of Tanzania) alipofanya ziara katika taasisi hiyo.
Waziri wa katiba na Sheria
Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akisisitiza jambo wakati akizungumza na Menejimenti ya
Taasisi ya mafunzo ya uanasheria kwa vitendo Tanzania (Law School of Tanzania).
Waziri wa katiba na Sheria
Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akikagua maktaba ya Taasisi ya mafunzo ya uanasheria
kwa vitendo Tanzania (Law School of Tanzania).
Naibu Waziri wa katiba na
Sheria Mhe Geofrey Mizengo Pinda akisisitiza jambo wakati akizungumza na
Menejimenti ya Taasisi ya mafunzo ya uanasheria kwa vitendo Tanzania (Law
School of Tanzania) alipofanya ziara ya kikazi hivi karibuni.
Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (Law School of Tanzania) Jaji Dkt. Benhajj Masoud akimkaribisha waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Mwigulu Nchemba (hayupo pichani) kuzungumza na watumishi wa taasisi hiyo alipofanya ziara ya kikazi hivi karibuni.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Serikali imedhamiria kuwasaidia kwa umakini mkubwa wananchi
katika tasnia ya sheria ambapo imeagiza kuanza haraka uandaaji wa sheria kwa
lugha ya kiswahili ikiwemo mwenendo wa mashauri na hukumu.
Agizo hilo kwa katibu mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria limeelekeza
kutafutwa haraka iwezekanavyo wataalamu watakaozitafsiri sheria zote
zilizoandikwa kwa lugha ya kingereza na kuwa katika lugha ya Taifa ya
kiswahili.
Waziri wa katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa
agizo hilo tarehe 22 Disemba 2020 alipotembelea Taasisi ya mafunzo ya
uanasheria kwa vitendo Tanzania (Law School of Tanzania) wakati akiwa
katika siku ya pili ya ziara ya kikazi Jijini Dar es salaam.
"Kwenye kauli nzuri za kuvutia tunasema kiswahili ndio
lugha nzuri tena ya kuvutia hivyo ni lazima tuanze kufundisha kwa kufuata
muelekeo wa lugha ya Taifa ili kuachana na utumwa wa matumizi ya lugha za
kikoloni katika sheria zetu" Amekaririwa Mhe Nchemba
Amesema kuwa Sheria ambayo mwananchi anahukumiwa imeandikwa
kingereza, hukumu anayopewa imeandikwa katika lugha ya kingereza hilo ni eneo
la haki za watu hivyo inapaswa kwanza lugha ya kiswahili ndiyo itumike kwenye
sheria kisha lugha zingine kama kingereza ziwe nyongeza.
Dkt Mwigulu amesema kuwa Sheria zinaandikwa katika lugha ya
kingereza na kuwaambia wananchi kutokujua kwao sheria sio sehemu ya utetezi
jambo hilo ni kinyume na utaratibu hivyo lazima kufanya mapitio ya sheria
zilizopo.
"Zipo nchi nyingi Duniani zimeendelea pasina kuwa
zinajua lugha ya kingereza hivyo ni wajibu wetu sasa rasmi kuitumia lugha ya
kiswahili" Amesisitiza
Waziri Mwigulu amesema kuwa katika mikutano mingi ya usaili
wa kazi inatumika lugha ya kingereza wakati huo huo viongozi wakuu wa usaili wanatumia
lugha ya kiswahili katika familia zao, na hata kazini.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Geofrey
Mizengo Pinda amesema kuwa uhitaji wa wataalamu wa kisheria katika maeneo mengi
ni mkubwa hivyo taaluma hiyo inapaswa kutolewa kwa weledi mkubwa kwa maslahi
makubwa ya Taifa.
Amesema kuwa mahitaji ya msaada wa kisheria ni makubwa hivyo
ni muhimu kuona ulazima wa kutembelea katika maeneo mbalimbali hususani
vijijini kutoa msaada wa kisheria kwani kumekuwa na manyanyaso kwa wananchi
wengi.
Ameongeza kuwa Taasisi ya mafunzo ya uanasheria kwa
vitendo Tanzania ni sehemu ya ukombozi kwa wananchi hivyo kuna kila sababu ya
kutengeneza chombo kama hicho kuwafikia wananchi kirahisi.
Comments
Post a Comment