WAZIRI MWIGULU NCHEMBA AIPONGEZA MAHAKAMA KWA UFANISI


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akisisitiza jambo wakati akizungumza kwenye kikao kazi na Menejimenti ya Mahakama akiwa katika ziara ya kikazi jijini Dar Es Salaam.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba (Wa Pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe Jaji Prof. Ibrahim Khamis Juma (Wa Pili Kushoto), Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Geofrey Mizengo Pinda (Kushoto) na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi (Kulia) mara baada ya kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Mahakama.



Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Ernest Mchome akifuatilia hotuba ya Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba (hayupo pichani) akisisitiza jambo wakati akizungumza kwenye kikao kazi na Menejimenti ya Mahakama. 


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akifuatilia taarifa ya utekelezaji wa maboresho ya mahakama pamoja na taarifa ya usikilizaji wa mashauri wakati wa kikao kazi na Menejimenti ya Mahakama. 


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba akisisitiza jambo wakati akizungumza kwenye kikao kazi na Menejimenti ya Mahakama.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Serikali imeipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kazi kubwa yenye weledi uliotukuka inayoifanya kwa ajili ya kuwasaidia wananchi.

Pamoja na pongezi hizo kadhalika mahakama imetakiwa kuhakikisha kuwa inatekeleza kwa haraka mipango inayojiwekea kwani kutofanya hivyo husababisha utekelezaji wake kuwa wa gharama kubwa pasina sababu za msingi.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba ametoa rai hiyo tarehe 23 Disemba 2020 wakati akizungumza na Menejimenti ya Mahakama akiwa katika siku ya tatu ya ziara ya kikazi Jijini Dar es salaam.

Dkt Nchemba amesema kuwa serikali itazifanyia kazi changamoto zote zinazoikabili Mahakama kote nchini ili kuhakikisha kuwa wananchi wanahudumiwa ipasavyo ikiwemo mashauri kufanyiwa kazi kwa haraka.

Ameongeza kuwa kunapokuwa na uwezekano wa kutatua mambo kwa haraka ni vyema mahakama na taaisisi zote za serikali kuzitatua bila kuwa na mkwamo wowote ili kuwarahisishia wananchi upatikanaji wa huduma.

Dkt Nchemba amesisitiza kuwa Mahakama pamoja na watendaji wote wa serikali wanapaswa kufanya kazi kwa uthubutu na kuchukua hatua kama ambavyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. John Pombe Magufuli amekuwa akisisitiza kufanya maamuzi mbalimbali pasina kufanya uonevu kwa wananchi.

Kuhusu kubadilisha sheria, Mwenendo wa mashauri na Hukumu, Amesisitiza maelekezo yake aliyoyatoa wakati alipotembelea Taasisi ya mafunzo ya uanasheria kwa vitendo Tanzania (Law School) kuhusu kubadilisha sheria, Mwenendo wa mashauri pamoja na Hukumu kuwa katika lugha ya Kiswahili.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Geofrey Mizengo Pinda ameipongeza mahakama kwa kazi kubwa ambayo inazifanya kuhakikisha wananchi wanapata haki pasina uonevu.

“Kesi nyingi hazijaamuriwa kutokana na vyombo vingi kuingia katika kukamilisha kazi zao ikiwemo Polisi, hivyo kuna kila sababu ya ukamilishaji wa taarifa muhimu za upelelezi ili mahakama iweze kukamilisha utoaji hukumu kwa haraka” Amesisitiza Mhe Pinda

Akizungumza kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe Jaji Prof. Ibrahim Khamis Juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi ameshukuru kwa ushirikiano inaoupata kutoka Wizara ya Katiba na Sheria kwani bila uongozi madhubuti huenda baadhi ya mambo yangekuwa hayajakamilika.

Jaji Dt Feleshi amesema kuwa ushirikiano huo umeongeza uwajibikaji na utekelezaji wa haraka wa majukumu yake.

Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA