RAIS MAGUFULI ASISITIZA KUHARAKISHWA KWA MATUMIZI YA KISWAHILI MAHAKAMANI
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Juma akitoa hotuba yake kwa viongozi na wananchi waliohudhuria sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria na miaka 100 ya Mahakama Kuu ya Tanzania.
Baadhi ya viongozi na wananchi waliohudhuria sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Sheria na Miaka 100 ya Mahakama Kuu ya Tanzania.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John
Pombe Magufuli ametoa rai kwa Mhimili wa Mahakama kuweka mkakati wa kutumia
lugha ya Kiswahili Mahakamani kwa manufaa ya wananchi huku akimpongeza na
kumteua Jaji Zephrine Galeba kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa kuonyesha
uzalendo wa kuandika hukumu kwa kutumia Kiswahili.
Rais Magufuli ambaye alikuwa mgeni rasmi katika sherehe
za maadhimisho ya siku ya sheria nchini yaliyofanyika kitaifa jijini Dodoma,
alisema kuwa Kiswahili ni miongoni mwa lugha kubwa duniani, ambayo inatumiwa na
Watanzania wengi.
“Nitumie fursa hii, kumpongeza sana Mheshimiwa Jaji
Galeba wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma kwa kutumia Kiswahili katika kutoa
hukumu kwenye Kesi ya North Mara Gold Mine dhidi ya Gerald Nzumbi katika kesi ya
Mapitio Na. 23 ya Mwaka 2020. Huyu ni Mzalendo wa kweli wa lugha ya Kiswahili
kwenye Mahakama. Na kwa sababu 27 ya uzalendo wake, kuanzia leo, namteua kuwa
Jaji wa Mahakama ya Rufaa,” alisema Mhe. Rais Magufuli.
Mhe. Rais alisema kuwa kushindwa kuitumia Lugha hii
kwenye masuala ya Kimahakama na Kisheria sio tu kunawanyima haki wananchi, bali
pia kuwaongezea gharama kupitia ukalimani wa kutafsiri hukumu na mienendo ya
kesi.
Aliendelea kwa kutoa rai kwa kuwasihi wadau wote wa
Mahakama, ikiwemo Mahakama, Bunge, Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu kuandaa Mkakati wa kuwezesha lugha ya Kiswahili kwenye masuala
ya Sheria na Mahakama, ikiwemo kuendelea kuzitafsiri Sheria za zamani na
kutunga Sheria mpya kwa lugha ya Kiswahili.
Kwa upande mwingine, Mhe. Rais alizungumzia pia tatizo la
ucheleweshaji wa mashauri kuwa bado lipo, hususan mashauri yanayohusu masuala
ya biashara na mikopo ambayo yanazorotesha ukuaji wa uchumi wa nchi.
“Ipo tabia ya baadhi ya wateja wa Benki kukimbilia
Mahakamani na kufungua kesi nyingi au kuweka mazuio kwa lengo la kuchelewesha
urejeshaji wa mikopo wanaodaiwa na benki. Kesi za namna hiyo zipo nyingi, na
nyingine zina zaidi ya miaka mitano hazijaamuliwa,” alieleza Mhe. Rais.
Alitoa mifano ya kesi zilizofunguliwa Mahakamani na
wateja wakubwa wa Benki nne ambazo ni Benki ya Posta Tanzania (TPB), Benki ya
Azania (Azania Bank Ltd) na Benki ya Maendeleo (TIB).
“Hali hii ya wadaiwa kukimbilia Mahakamani na kesi
kuchelewa kutolewa maamuzi, imekuwa na athari nyingi za kiuchumi kwa nchi yetu.
Baadhi ya athari hizo ni kupungua kwa uwezo wa benki zetu kutoa mikopo kwa
wateja; (ii) kuongezeka kwa gharama za riba kutokana na benki kulazimika
kuongeza riba na kadhalika,” alieleza.
Aliongeza kuwa kwa mujibu wa taarifa Desemba 31, 2020 inaonyesha
kuwa Azania Bank Ltd ina kesi 36 zilifunguliwa na wadaiwa wake zenye thamani ya
shilingi bilioni 352.27; Benki ya Maendeleo (TIB) ina kesi 44 zenye thamani ya
shilingi bilioni 167.267; Benki ya TPB ina kesi 16 zilizofunguliwa na wadaiwa
wake zenye thamani ya shilingi bilioni 6.2; CRDB ina kesi 282 zenye thamani ya
shilingi bilioni 113.25.
Akizungumzia Maadili ya Watumishi wa Mahakama, Mhe. Rais
alimpongeza Mhe. Jaji Mkuu kwa hatua kinidhamu zilizochukuliwa na Mahakama
dhidi ya Maafisa wake wanaoichafua Taasisi huku akitoa wito kwa Kamati za
maadili za Maafisa wa Mahakama za Mikoa na Wilaya kukutana.
“Hata hivyo, nimesikitika sana na taarifa kwamba, Kamati
za Maadili za Maafisa wa Mahakama za Mikoa na Wilaya, ambazo kisheria
zinaongozwa na Wakuu wa Mikoa na Wilaya zimekuwa hazikutani; na hivyo,
kushindwa kuchukua hatua za kinidhamu kwa watumishi wenye makosa. Napenda
kutumia fursa hii kuagiza Wakuu wa Mikoa na Wilaya wote kuhakikisha Kamati hizo
za Maadili 24 zinakutana ili kujadili masuala ya maadili ya watumishi wa
Mahakama. Naagiza pia Wakuu wote wa Mikoa kuwasilisha Ripoti vya Vikao vya
Kamati hizo mwezi huu,” alisisitiza Mhe. Rais.
Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof.
Ibrahim Hamis Juma ameiomba Serikali na Bunge kuyapa kipaumbele mahitaji ya
Mahakama yaliyooneshwa katika mpango wa miaka mitano wa maendeleo ya
miundombinu ya Mahakama 2016/17-2020/2021 itakapojadili na kupitisha Mpango wa
Taifa wa maendeleo wa miaka mitano.
“Mhimili wa Mahakama peke yake hauwezi kutatua
changamoto bila kuwezeshwa na Mihimili ya Serikali na Bunge inayosimamia
rasilimali za aina zote, hapa napenda kutambua namna mihimili ya
Serikali na Bunge ilivyokubali jukumu la kutatua changamoto zinazoikabili
Mahakama ya Tanzania”, alisema Jaji Mkuu.
Kwa mujibu wa Prof. Juma, mfano wa Mhimili wa Mahakama
kuwezeshwa na Serikali ni kukamilishwa kwa mazungumzo na Benki ya Dunia kuhusu
namna ya kusaidia kuendeleza juhudi za maboresho ya utoaji huduma za Mahakama
kwa kuwezesha upatikanaji wa fedha za kuboresha shughuli na huduma za Mahakama.
Mwaka 2016, Benki ya Dunia iliridhia kuisaidia Mahakama
ya Tanzania kupitia Serikali ya Tanzania kupata fedha za mkopo wenye masharti
nafuu uliogharimu Dola za Marekani milioni 65 ambazo ni saw ana shilingi
bilioni 139.5 za kitanzania.
Akizungumzia namna mhimili
huo ulivyowezeshwa, Jaji Mkuu alisema miongoni mwa mafanikio yaliyotokana na
uwezeshwaji huo ni kukamilika kwa ujenzi wa majengo ya
Mahakama Kuu kanda za Kigoma na Musoma. Aliongeza kuwa, Mahakama inatarajia
kukamilisha ujenzi wa majengo ya Mahakama Kuu nyingine sita katika miji ya
Mwanza, Arusha, Dodoma, Morogoro pamoja na wilaya za Temeke na Kinondoni mkoani
Dar es salaam.
Alisema katika kuendelea kusogeza huduma za Mahakama
karibu zaidi na wananchi, Mahakama ya Tanzania inatarajia kuanza ujenzi wa
majengo ya Mahakama za wilaya 25 katika mwaka wa fedha 2020/21. Alisema ujenzi
huo utawapunguzia mzigo wananchi ambao hulazimika kupata huduma kwenye
Mahakama za wilaya jirani.
Comments
Post a Comment