SERIKALI HAINA SHERIA KANDAMIZI, SHERIA ZOTE ZINAZOTUMIKA NCHINI ZIMETUNGWA NA BUNGE – MHE. GEOFREY PINDA
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Geophrey Pinda akijibu maswali bungeni wakati wa mkutano wa 12 Jijini Dodoma, Leo tarehe 5 Februari 2021.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Geophrey Pinda
amewahakikishia watanzania kuwa Serikali haina Sheria
Kandamizi hivyo Sheria zote zinazotumika nchini zilitungwa na
Bunge tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo halijawahi
kutunga Sheria Kandamizi.
Amesema kuwa Serikali kwa kuzingatia mahitaji ya wakati na
watu wake, imekuwa ikiwasilisha mapendekezo ya marekebisho ya Sheria mbalimbali
ili kuziboresha Sheria hizo.
Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe Zainab Katimba
aliyetaka kufahamu Serikali ina mpango gani wa kurekebisha baadhi ya
sheria kandamizi kwa wanawake ili ziendane na wakati, Mhe
Pinda amesema kuwa Kutokana na wakati uliopo na mahitaji ya
sasa Serikali imeanzisha mchakato wa kuzipitia baadhi ya sheria ili ziweze
kufanyiwa marekebisho kuendana na wakati.
Amesema Serikali kupitia Wizara ya Katiba na
Sheria imeandaa muswada wa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Ndoa
utakaowasilishwa Bungeni ili kuiboresha, kwa lengo la kulinda makundi
ya wanufaika na Sheria hiyo.
Aidha, Serikali inaendelea na hatua mbalimbali za kupitia Sheria
ya Usimamizi wa Mirathi na Sheria za Kimila. Hatua hizo zikikamilika, Muswada
wa mapendekezo ya kuzirekebisha sheria hizo utawasilishwa Bungeni, ili
Wabunge wapate nafasi nzuri ya kujadiliana na kuyapitisha marekebisho hayo.
Mhe Pinda amesema kuwa Wizara ipo katika mabadiliko makubwa
ya kuhakikisha kunafanyika maboresho makubwa ya Sheria zetu ikiwemo kuzitafsiri
kwa Kiswahili lakini pia kuweka vipengele kwenye sheria hizo vya kutoa hukumu
kwa lugha ya Kiswahili jambo ambalo litaleta tija kubwa katika ukuaji wa uchumi
wa Nchi yetu.
Hivyo amewaomba wabunge kuunga mkono juhudi za Serikali
katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha utawala wa Sheria na upatikanaji
wa haki nchini.
Comments
Post a Comment