TUMIENI MITANDAO YA SIMU KUELIMISHA MASUALA YA KISHERIA - MAKAMU WA RAIS
Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan akishiriki matembezi ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria na miaka 100 ya Mahakama Kuu.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Ibrahim Juma na Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome wakifurahia jambo wakati wa matembezi ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria na miaka 100 ya Mahakama Kuu.
Watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria wakishiriki matembezi ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria na miaka 100 ya Mahakama Kuu.
Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria wakifuatilia hotuba ya Makamu wa Rais wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria na Miaka 100 ya Mahakama Kuu.Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia
Suluhu Hassan ameushauri Mhimili wa Mahakama nchini kutumia Mitandao ya simu
kutoa elimu ya sheria kwa wananchi kupitia jumbe fupifupi.
Akifungua rasmi Maonesho ya Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na
miaka 100 ya Mahakama Kuu ya Tanzania mapema leo jijini Dodoma, Makamu wa Rais
amesema kuwa kwa kufanya hivyo wananchi wengi watapata ufahamu juu ya taratibu
mbalimbali za kimahakama.
“Hivi sasa mitandao ya simu imekuwa na desturi ya kutuma meseji
mbalimbali kuhusu huduma kadhaa inazotoa, hivyo tumieni pia fursa hiyo pia
kutumia mitandao ya simu kutoa elimu kuhusu taratibu za Mahakama ili wananchi
wapate uelewa,” alisema Makamu wa Rais.
Akizungumzia matumizi ya lugha ya Kiswahili, Mhe. Suluhu
ameiomba Mahakama kutumia Kiswahili hata katika machapisho yake kueleza
taratibu mbalimbali za mhimili huo ili wananchi waweze kuelewa.
“Haitopendeza kuona Taifa huru ambalo Mahakama Kuu inatimiza
miaka 100 bado wananchi wake walio wengi wanakosa haki zao za msingi kutokana
na changamoto ya lugha Mahakamani,” alieleza.
Aidha, Makamu huyo wa Rais alitoa rai kwa Mahakama kuhakikisha
kuwa katika mikakati yake ihakikishe kuwa sheria za nchi zinakuwa na tafsiri
sahihi na malengo na azma ya kutungwa kwao na kuwa.
Kwa upande mwingine, Makamu wa Rais aliipongeza Mahakama kwa
kutimiza miaka 100 ya Mahakama Kuu nchini tangu kuanzishwa kwake huku akimsifu
Mhe. Jaji Mkuu kwa mageuzi na marekebisho mbalimbali katika sekta ya sheria.
“Mhe. Jaji Mkuu nafahamu tangu uteuliwe umesukuma mageuzi na
marekebisho mbalimbali ya sheria kwenye Mahakama ili kuweza kuufanya mhimili
huu kwenda na wakati lakini pia kuhimili mabadiliko. Nakupongeza sana wewe
binafsi na Mhimili wote wa Mahakama kwa kutimiza miaka 100 mkiwa mmeimarisha
vyema utendaji wa chombo chenu,” alisisitiza Mhe. Suluhu.
Kwa ujumla Mhe. Makamu wa Rais alipongeza pia maboresho
mbalimbali ya Mahakama yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika huku akiahidi
ushirikiano kutoka Serikalini ili huduma ya utoaji haki iendelee kutenda haki.
Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania-Mhe. Prof. Ibrahim Hamis
Juma amewataka wananchi kutumia tovuti ya Mahakama kupata taarifa zinazohusiana
na Mahakama.
“Nitumie nafasi hii kuwakaribisha wananchi wote watembelee
Tovuti za Mahakama na za wadau wa sekta ya Haki ili kupata taarifa muhimu kila
siku, wakati wowote na watoe maoni na mapendekezo kila siku yenye lengo la
kuboresha utoaji haki nchini,” alisema.
Aidha, aliwataka wananchi kutembelea maonesho hayo na kuongeza
kuwa wasiridhike na maboresho yaliyopo bali waendelee kudai maboresho zaidi
yanayolenga kuwawezesha kupata haki.
Akizungumzia matumizi ya Kiswahili Mahakamani, Mhe. Jaji Prof.
Juma alisema jitihada za kuhakikisha kuwa lugha ya Kiswahili inatumika katika
ngazi zote za Mahakama zilianza tangu wakati TELFORD PHILIP GEORGES alipokuwa
Jaji Mkuu wa Tanzania kati ya mwaka 1965 na 1971.
“Mahakama ya Tanzania imeanza matayarisho ya awali ili
kumbukumbu za mashauri na hukumu za Mahakama katika ngazi za Mahakama za
Wilaya, za Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani ziweze kupatikana
papo hapo, katika lugha ya Kiswahili na kwa lugha ya kiingereza kabla ya mwisho
wa mwaka huu,” alieleza Mhe. Jaji Mkuu.
Katika hafla hiyo, Mhe. Suluhu alizindua pia miongozo mbalimbali
ya Mahakama ikiwemo muongozo wa Dhamana, mwongozo wa utekelezaji wa mashauri,
mwongozo wa usimamizi wa uondoshaji wa vielelezo, mwongozo wa madalali na
Wasambaza nyaraka za Mahakama.
Mingine ni mwongozo wa watumiaji wa huduma za Mahakama, Mwongozo
wa utoaji hukumu kwa Maofisa wa Mahakama na Mwongozi wa kushughulikia mashauri
yanayohusu makundi maalum.
Maadhimisho ya wiki ya sheria yaliyozinduliwa rasmi Januari 24
na kilele cha Siku ya Sheria Nchini, huashiria kuanza kwa mwaka mpya wa
Kimahakama ambao ni mwanzo wa shughuli za Mahakama katika mwaka. Maonesho hayo
ambayo yanafanyika kitaifa katika Viwanja vya Nyerere ‘Square’ yameshirikisha
wadau mbalimbali kama Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu
wa Serikali, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka na wengineo.
Comments
Post a Comment