WIZARA YA KATIBA NA SHERIA YAANZA ZOEZI LA KUTAFSIRI SHERIA ZOTE NCHINI KUWA KATIKA LUGHA YA KISWAHILI





Wataalamu kutoka taasisi za sheria ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tume ya Kurekebisha Sheria na chama cha wanasheria Tanganyika wakiongozwa na Wanasheria wa Wizara ya Katiba na Sheria wakiendelea na zoezi la kutafsiri sheria kuwa katika lugha ya kiswahili. Awamu ya kwanza ya zoezi hili ilianza kufanyika Machi 3 na inategemea kukamilika Machi 11, 2021 na itahusisha utafsiri wa sheria 16. Kazi ya kutafsiri sheria zote itafanyika kwa awamu tatu ambapo awamu hizo zinategemea kukamilika mwezi Disemba, 2021.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Kikao kazi cha wataalamu wa sheria kutoka taasisi mbalimbali wakiongozwa na Wanasheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria chaanza kazi ya kutafsiri sheria zote nchini.

Kikao kazi hicho cha awamu ya kwanza cha siku 8 kilichoanza kazi Machi 3 kinatarajiwa kukamilisha kazi yake Machi 11 kwa kutafsiri sheria 16.

Huu ni utekelezaji wa agizo lilitolewa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba  kwa Katibu Mkuu wa wizara hiyo Prof. Sifuni Mchome Disemba 22, 2020 alipotembelea Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania. Katika ziara hiyo waziri Dkt. Nchemba alisema sheria ni sekta inayomsaidia mtu kupata haki hivyo inapaswa lugha ya Kiswahili itumike kwanza katika masuala mbalimbali ya kisheria kisha lugha nyingine ziwe ni za nyongeza, hivyo sheria, mwenendo wa mashauri na hukumu iandikwe kwa lugha ya Kiswahili ili kuwezesha wananchi kuelewa kwa urahisi kuhusu kesi zao,

Zoezi hili la kutafsiri sheria linategemewa kufanyika kwa awamu tatu kabla ya kuhakikiwa kwa tafsiri hiyo kuangalia kama kilichotafsiriwa ni sahihi na hakijapoteza maana ya kile kilichokusudiwa katika utungwaji wa sheria husika.

Zoezi la kutafsiri sheria linatarajiwa kukamilika mwezi Disemba, 2021 ambapo sheria zote nchini zinatarajiwa kuwa zimetafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA