TANZANIA SIO NCHI YA KWANZA KUTUMIA KISWAHILI KATIKA UTOAJI HAKI - PINDA
Naibu
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe.Gephrey Pinda akifafanua jambo kwa washiriki
wakati wa Mkutano wa kujadili matumizi ya kiswahili katika Tasnia ya
sheria uliofanyika Juni 11,2021 jijini Dodoma.
Naibu
Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Amon Mpanju akitoa mada kuhusu
mabadiliko ya sheria na hatua zilizochukuliwa na Serikali wakati wa Mkutano wa
kujadili matumizi ya kiswahili katika Tasnia ya sheria uliofanyika Juni
11,2021 jijini Dodoma.
Mwalimu
kutoka Shule kuu ya Sheria ya chuo kikuu cha Dar es salaam Dkt. Asina Omari akitoa
mada kwa washiriki wakati wa Mkutano wa kujadili matumizi ya kiswahili katika
Tasnia ya sheria uliofanyika Juni 11,2021 jijini Dodoma.
Baadhi
ya washiriki wakifatilia hotuba ya Naibu Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe.Geophrey Pinda,(hayupo pichani) wakati wa Mkutano wa kujadili matumizi ya
kiswahili katika Tasnia ya sheria uliofanyika jijini Dodoma.
Tanzania
siyo nchi ya kwanza kuacha lugha ya kigeni na badala yake kutumia lugha yake ya
kiswahili katika utoaji wa haki kwa wananchi.
Hayo yameelezwa jijini Dodoma na Naibu Waziri
wa Katiba na Sheria Mhe. Geophrey Pinda wakati akifungua Mkutano wa
kujadili matumizi ya kiswahili katika Tasnia ya sheria. Waziri Pinda amewataka
washiriki kujadili kwa kina mchango wa Kiswahili nchini.
Mhe.Pinda amesema kuwa kuna nchi nyingine
ambazo zimekuwa zikitumia lugha zao rasmi katika kutoa haki ikiwemo India na
zimekuwa zikifanya vizuri katika eneo hilo
“Ziko nchi wanatumia lugha zao katika
uandishi wa sheria na utoaji wa huduma mbalimbali zikiwemo za haki, ifahamike
kuwa asili ya lugha ya kisheria si kiingereza kama inavyofahamika na wengi bali
lugha za kijerumani, kilatini na kifaransa kwa kuwa walionekana
kustaarabika’’amesema Pinda
Hata hivyo amesema kuwa licha ya lugha
ya Kiswahili kuwa moja ya nguzo inayosimamia ukuaji wa uchumi, serikali
iliona umuhimu wa kuanza kutumia lugha hiyo katika utoaji na upatikanaji wa
haki nchini.
”Kuna sheria nyingi ziko kwa kiingereza
ambayo ineonekana kuwa ni changamoto katika upatikanaji wa haki
nchini”amefafanua
Aidha Mhe.Pinda amewataka wanasheria
kujikita na kutumia lugha ya Kiswahili katika utoaji wa haki nchini.
‘’Niwaombe wanasheria kutumia lugha ya
Kiswahili kuna watu wamekosa haki zao sababu hawafahamu lugha , ni wakati sasa
kwa watanzania kutumia lugha yetu, hatuwezi kutumia lugha ambazo si za kwetu’’amesisitiza
Pinda amesema Kiswahili ni lugha ya kimataifa
ikiwa ya kumi duniani yenye wazungumzaji wengi Barani Afrika na duniani kote.
Pia ameeleza kuwa Wizara inaratibu ukuzwaji
na uendelezaji wa matumizi ya lugha ya kiswahili katika utoaji haki, kuratibu
wasimamiaji haki katika sekta nyingine katika kutekeleza na kutoa haki nchini.
‘’Wizara ya katiba na sheria inaratibu zoezi
la kutafsiri sheria zote kwa lugha ya Kiswahili, mchakato wa kutafsiri
unafanywa ndani ya Wizara pamoja na taasisi zake’’ amesema Mhe. Pinda
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya
Katiba na Sheria Ndg. Amon Mpanju amesema kuwa lengo la mkutano huo ni kujadili
matumizi ya lugha ya Kiswahili katika mfumo wa utoaji haki.
‘’Tumeona tukutane na wadau wenye ubobezi wa
lugha hii ya Kiswahili ili tuje na misamiati itakayokubalika katika mfumo wa
utoaji haki lakini pia tunahakikisha tunapata lugha sahihi ya Kiswahili
tutakayoitumia katika mfumo wetu wa utoaji haki’’amesema Mpanju
Naye Mwalimu kutoka Shule kuu ya Sheria
ya chuo kikuu cha Dar es salaam Dkt. Asina Omari akitoa neno la shukrani kwa
niaba ya washiriki amesema kuwa watahakikisha kuwa wanakuwa na sheria
ambazo zitasaidia wananchi kupata haki zao.
‘’Tumepokea maekezo tutakwenda kuyafanyia
kazi ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata haki zao kupitia sheria’’amesema Dkt.
Asina.
Mnamo tarehe 24/1/2021 Mhe. Samia Suluhu
Hassan akiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alihudhuria
ufunguzi wa Maadhimisho ya wiki ya sheria, alisisitiza kuwa ni vyema sheria za
uendeshaji wa kesi mahakamani ikawa kwa lugha ya kiswahili.
Ikumbukwe kuwa Hayati Dkt John Pombe Magufuli
wakati wa uhai wake alijipambanua katika matumizi ya lugha ya Kiswahili ambapo
hotuba zake nyingi alizitoa kwa Kiswahili ambapo alihimiza umuhimu wa Kiswahili
katika mfumo wa sheria na utoaji haki nchini katika nyakati tofauti.
Comments
Post a Comment