CHETI CHA KUZALIWA NI HAKI YA MTOTO RAIA NA ASIYE RAIA – WAZIRI KABUDI


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiongea katika hafla ya uzinduzi wa usajili wa watoto chini ya miaka mitano katika mikoa ya Katavi na Rukwa. Hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya shule ya msingi Kashatu Manispaa ya Mpanda Mkoani Katavi.

Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba Kabudi akizindua mpango wa usajili wa watoto chini ya miaka mitano katika mikoa ya Katavi na Rukwa.




Waziri Kabudi akitoa vyeti vya kuzaliwa watoto kwa wazazi waliofika katika viwanja vya shule ya msingi Kashatu Mkoani Katavi kusajili watoto wao.


Mkurugenzi wa Idara ya Haki za Binadamu kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Nkasori Sarakikya ambaye alikuwa Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria kwenye hafla hiyo akitoa salamu za wizara.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Cheti cha kuzaliwa ni haki ya kila mtoto aliyezaliwa Tanzania awe raia au asiwe raia, hii itasaidia utambuzi wa wananchi na kuwezesha Serikali kupanga mipango ya maendeleo ipasavyo kulingana na idadi ya wananchi waliopo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Mpango wa Usajili wa Watoto wa Umri Chini ya Miaka Mitano ulioambatana na utoaji wa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto hao katika Mikoa ya Katavi na Rukwa uliofanyika katika viwanja vya shule ya msingi Kashatu  Manispaa ya Mpanda Mkoani Katavi tarehe 24, Novemba, 2021.

Waziri Kabudi ambaye  alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo, amesema Serikali imechukua hatua  madhubuti na kufanya maboresho ya sheria, rasilimali fedha pamoja na wataalam wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano TEHAMA  kwa lengo la kuharakisha upatikanaji wa huduma za usajili wa matukio muhimu ya binadamu ikiwemo vizazi kwa watoto wa umri chini ya miaka mitano.

 “Usajili wa matukio muhimu ya binadamu hufanyika duniani kote ili kufahamu taarifa sahihi na kupanga mipango bora ya kuhudumia wananchi” alisema Prof. Kabudi.

Wakati huohuo Waziri Kabudi  ametoa maagizo kwa viongozi wa Mikoa inayopakana na nchi jirani wasimamie zoezi hilo kwa ufanisi ili watoto wanaostahili kusajiliwa tu ndio wasajiliwe na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa huku  akisisitiza Kamati za Ulinzi na Usalama zishirikishwe katika kila hatua ya zoezi hilo na kwamba udanganyifu wowote wa taarifa ni kosa kisheria na atakayefanya hivyo atachukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kifungo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya ya ushauri ya Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) Prof. Hamis Dihenga  amesema usajili wa watoto wanaozaliwa ni muendelezo wa usajili wa matukio muhimu ya binadamu na kwamba itawezesha upatikanaji wa takwimu sahihi na kwa wakati badala ya kutegemea Sensa na makisio katika upangaji wa mipango ya maendeleo.

Aliongeza kuwa kabla ya kampeni hii kuanza kwa Mkoa wa Katavi asilimia 6.3 na Rukwa asilimia 5.8 ya watu ndiyo  wamesajiliwa hivyo baada ya wiki mbili za kampeni hii tunategemea watoto ambao hawajasajiliwa watakuwa wamesajiliwa kwa asilimia 100 Kwani kupitia zoezi hili la  usajili wazazi au walezi wenye watoto wa kundi hilo hawatotozwa gharama yoyote ya malipo ya huduma ya  usajili na kupatiwa cheti cha kuzaliwa kwani tayari serikali kwa kushirikiana na wadau na mashirika ya maendeleo ya Kimataifa wameshagharamia.

 “ Mpango huu umerahisisha upatikanaji wa kuduma kwani vyeti hivyo vinatolewa katika ofisi za kata na vituo vya tiba vinavyotoa huduma ya mama na mtoto pamoja na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano imesaidia  kurahisisha taarifa kutoka katika vituo vya usajili kutumwa moja kwa moja hadi kwenye  kanzidata ya RITA Makao Makuu’’..Alisema Prof. Dihenga

 Nae Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Nkasori Sarakikya alitoa salamu za Wizara kwa kuipongeza RITA kwa kuwezesha watoto kupata haki yao ya kupatiwa vyeti vya kuzaliwa na kuwasihi wananchi wa Katavi na Rukwa kutumia fursa hiyo ipasavyo.

“Vyeti vya kuzaliwa ni ufunguo wa maendeleo kwa watoto kwa kuwa vinahitajika katika hatua muhimu za binadamu hivyo tuwasajili watoto wetu” alisema Bi. Sarakikya

RITA kupitia Wizara ya katiba na sheria inatekeleza na kusimamia mpango huo wa usajili wa watoto wa umri chini ya miaka mitano na mpaka sasa tayari Mikoa 22 inatekeleza mpango huo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo,Ofisi ya Rais TAMISEMI, Idara ya Uhamiaji, Wizara ya Afya Ustawi wa Jamii Wazee na Watoto, Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA) na wadau wa maendeleao Shirika la kuhudumia watoto Duniani UNICEF, Shirika la maendeleo la Canada na kampuni ya simu za mkononi Tigo.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA