UTOAJI HAKI UZIDI KUIMARISHWA HASA KWA WASIO NA UWEZO ASEMA PROF. KABUDI

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akipokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko alipomtembelea ofisini kwake mjini Mpanda kabla ya kukagua mahakama za Hakimu Mfawidhi Katavi, Mahakama ya Wilaya Mpanda na Mahakama ya Wilaya Tanganyika.


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiongea na watumishi wa Mkoa wa Katavi (hawapo pichani) alipotembelea ofisini hapo kabla ya kufanya ziara katika mahakama za hakimu mkazi katavi, wilaya ya mpanda na wilaya ya Tanganyika.


 Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akisalimiana na watumishi wa Mahakama alipotembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi na Mahakama ya Wilaya Mpanda.


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akisisitiza jambo katika ziara hiyo.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akitoa ushauri wakati akikagua ujenzi wa mahakama ya Wilaya Tanganyika.

XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Waziri wa Katiba na Sheria Prof. Palamagamba Kabudi asisitiza kuzingatiwa kwa lengo la Rais la kuimarisha utoaji haki hasa kwa watu wa vijijini ambao wengi wao hawana uwezo.

“Lengo la Rais ni kuimarisha utoaji haki hasa kwa watu wa vijijini wasio na uwezo wa kuwalipa Mawakili” alisema.

Waziri Kabudi aliyasema hayo wakati akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mhe. Mwanamvua Mrindoko na kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa Katavi wakati alipomtembelea Mkuu wa Mkoa huyo ofisini kwake kabla ya kufanya ziara ya kukagua mahakama za Hakimu Mkazi Katavi, Mahakama ya Wilaya Mpanda na kukagua ujenzi wa Mahakama ya Wilaya Tanganyika.

Aliongeza, kwa kuwa Mawakili hutoza gharama katika kazi zao na hivyo kutegemewa zaidi na watu wa mijini, serikali inaangalia namna ya kuboresha kazi za wasaidizi wa kisheria kwa kuwapatia elimu ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi na kuwasaidia  watu hasa wa vijijini wasio na uwezo wa kulipa mawakili.

Alisisitiza, mahakama mbalimbali zinaendelea kujengwa ikiwemo mahakama ya Wilaya ya Tanganyika iliyopo Mkoani Katavi na mahakama za mwanzo nchini kote lengo likiwa ni kusogeza huduma ya utoaji haki karibu zaidi kwa wananchi na kuwawezesha kupata haki kwa wakati.

Waziri Kabudi alisema katika kuwapatia haki wananchi huduma za utoaji haki zimeimarishwa kwani kwa sasa mahakimu wenye shahada wameanza kufanya kazi katika ngazi ya mahakama za mwanzo na Mawakili pia wameruhusiwa kufanya kazi katika Mahakama hizo.

Aidha, Prof. kabudi alipongeza utendaji kazi wa Mahakama za Hakimu Mkazi Katavi na Mahakama ya Wilaya Mpanda kwa kutoa vifungo vya nje kama adhabu mbadala kwa wafungwa 32 wanaotumikia adhabu hiyo kwa sasa ikiwa na lengo la kupunguza msongamano magerezani.

 


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA