MABORESHO YA HAKI JINAI KUTATUA CHANGAMOTO ZA UPATIKANAJI HAKI – HOMERA




 Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera akizungumza katika ufunguzi wa Wiki ya Msaada wa Kisheria.




Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Zuberi Homera ( wa pili kushoto) akifurahia jambo wakati akipata maelezo kutoka kwa Wakili George Mollel (wa tatu kulia) alipotembelea banda la Wizara ya Katiba na Sheria kabla ya kuzindua rasmi Wiki ya Msaada wa Kisheria inayofanyika kitaifa Mkoani Mbeya.


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe Juma Homera akipata maelezo alipotembelea banda la Haki za Binadamu.



Watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera (waliokaa katikati) baada ya uzinduzi wa Wiki ya Msaada wa Kisheria.





Wananchi wakipata huduma katika mabanda mbalimbali katika viwanja vya Ruandanzovwe jijini Mbeya kwenye maonyesho ya Wiki ya Msaada wa Kisheria.


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Juma Homera amesema maboresho ya haki jinai yatasaidia kutatua changamoto za upatikanaji haki.

Mhe. Homera ameyasema hayo wakati akizindua Wiki ya Msaada wa Kisheria yanayofanyika kitaifa Mkoani Mbeya.

Alisema, “pamoja na utoaji wa msaada wa kisheria katika maeneo ya vizuizi ambayo hufanywa na wadau mbalimbali wakiratibiwa na Wizara ya Katiba na Sheria, bado zipo changamoto za ucheleweshaji wa upelelezi, ucheleweshaji wa mashauri mahakamani, mlundikano wa wafungwa na mahabusu magerezani, uchache wa watoa huduma ya msaada wa kisheria na mengi yanayokwamisha utolewaji wa haki kwa wakati hivyo inahitajika maboresho ya mfumo wa haki jinai ili kupunguza changamoto nilizozitaja”.

Aliongeza anafahamu kuwa yapo maboresho mengi sana yaliyofanywa na Serikali katika mfumo wa haki jinai ikiwemo kutenganisha shughuli za upelelezi na uendeshaji wa mashtaka na Ofisi za Mkurugenzi wa Mashtaka kufunguliwa katika Mikoa yote Tanzania Bara. Jambo hili limewezesha huduma za mashtaka kufanywa na Mawakili wa Serikali tofauti na hapo awali lilipokuwa linafanywa na waendesha mashtaka wa Jeshi la Polisi. Pamoja na kupungua kwa ubambikaji wa kesi, ofisi hizi bado hazijaenea katika Wilaya zote nchini ili kuondoa kabisa changamoto na mtu mmoja kukamata, kupepeleza na kuendesha mashtaka, jambo ambalo ni mgongano wa kimaslahi.

Alifafanua kuwa, Sambamba na hilo Sheria mbalimbali zilifanyiwa marekebisho ili kushughulikia mashauri ya jinai kwa wakati na kupunguza misongamano ya mahabusu na wafungwa magerezani. Marekebisho hayo yaliweka utaratibu wa kuingia makubaliano ya maungamo ili kupata nafuu ya adhabu, kufifisha makosa na kulipa faini zilizowekwa kwenye makosa hayo bila shtaka kwenda mahakamani; usuluhishi katika makosa ya jinai kwa makosa yenye kifungo kisichozidi miaka mitatu; uwemo wa majukwaa ya haki jinai kila Mkoa na Wilaya ili kutatua changamoto za masuala ya jinai; matumizi ya adhabu mbadala ikiwemo vifungo vya nje na kufanya kazi za jamii. Aidha, kutokana na ucheleweshaji uliopo kwenye makosa mengi ya Jinai, Mkurugenzi wa Mashtaka ametoa mwongozo wa kutokufungua baadhi ya kesi mahakamani hadi kwanza upelelezi wake ukamilike. Haya yote ni kuhakikisha kauli ya Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani na misongamano mahabusu na wafungwa magerezani kwa mashauri yasiyo na tija inatekelezwa.

Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Dunstan Shimbo alisema Wizara itaendelea kushirikiana na wadau katika kuhakikisha sheria ya msaada wa kisheria inatekelezwa ili kuendelea kutatua kero ya upatikanaji haki kwa wananchi, pia wizara inaendelea kutoa elimu kwa watoa msaada wa kisheria ili waweze kufanya kazi hiyo kwa ufanisi.

Aidha, Mwakilishi wa Msajili wa Watoa Msaada wa Kisheria Bi. Ester Msambazi amesema Yapo maboresho mengi ambayo yamefanyika katika sekta ya jinai ambayo yanalenga kutoa haki kwa wakati. Maboresho haya yanajumuisha sheria na taratibu za kushughulikia mashauri ya jinai ikiwa ni pamoja na matumizi ya adhabu mbadala zikiwemo faini na vifungo vya nje.

Alisema, ”Tunafahamu kuwa vyombo vyetu vya utoaji haki vinafanya kila liwezekanalo kupunguza msongamano Magerezani. Hata hivyo, ziko tafsiri potofu miongoni mwa wananchi kuwa kila mhalifu ni lazima afungwe gerezani. Wapo wananchi wanaoamini kuwa adhabu halali ni kifungo. Hii inasababisha matumizi ya vifungo mbadala kutotumika na kwa kuhofia kuonekana kuwa wamepokea rushwa. Hili ni jambo linaloturudisha nyuma kama sekta ya haki”

Aliongeza,”Kwa kutambua hilo, wadau wa msaada wa kisheria wameamua kuufahamisha umma kuwa matumizi ya adhabu mbadala ni halali kisheria na ni vema kutumia njia hizo kwa manufaa ya Taifa. Manufaa ya Taifa yanatokana na ukweli kwamba wafungwa wanapopewa kifungo cha nje wanapata fursa ya kujihusisha na kazi za kiuchumi kwa manufaa ya familia zao na za Taifa kwa ujumla”.

Maadhimisho haya yanaratibiwa na kusimamiwa na Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria na kwa mwaka huu ni mara ya tano kufanyika tangu kuanzishwa kwake.

 

 

 

 






Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA