JAMII YAASWA KUKABIDHI JUKUMU LA USIMAMIZI WA MIRATHI KWA RITA BADALA YA NDUGU WA MAREHEMU
Waziri wa Katiba na SheriaMhe. George Simbachawene (kulia) akipokea taarifa ya utekelezaji ya Bodi ya Ushauri ya RITA iliyomaliza muda wake kutoka kwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Hamis Dihenga. Anayeshuhudia katikati ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Geophrey Pinda.
Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya RITA iliyomaliza muda wake Prof. Hamis Dihenga akitoa taarifa fupi ya utekelezaji wa bodi hiyo kwa miaka mitatu kuanzia 2019 hadi 2022 kwa Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. George Simbachawene ( hayupo pichani) kabla ya kukabidhi kwake taarifa hiyo.
Aliyekuwa mjumbe wa Bodi ya Ushauri ya RITA Bi. Nkasori Sarakikya akifafanua jambo kuhusu taarifa ya utekelezaji ya bodi hiyo.
Baadhi ya wataalam waliohudhuria hafla hiyo ya kukabidhi taarifa ya utekelezaji.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. George Simbachawene (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na waliokuwa wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya RITA na viongozi wa Wizara.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Jamii imetakiwa kutokuhangaika
kutafuta watu ndani ya familia kusimamia mali za marehemu kutokana na baadhi
yao kutokuwa waadilifu kwa kusababisha migogoro ya kugombania na kufuja mali hizo na badala yake wakabidhi
jukumu hilo kwa Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) ambapo sheria umeupa mamlaka
kisheria kusimamia mirathi kuandika na kuhifadhi wosia.
Hayo yamesemwa hii leo Jijini Dodoma na Waziri wa Katiba na
Sheria Mhe. Goerge Simbachawene wakati akipokea
taarifa ya Bodi ya Ushauri ya RITA ambayo imemaliza muda wake tangu mwaka 2019 hadi 2022 chini ya
Mwenyekiti wake Prof. Hamis Dihenga.
Mhe. Simbachawene amekemea vikali tabia za baadhi ya wanandugu kuanzisha migogoro ya mirathi isiyokwisha
katika jamii na kusababisha mali nyingi za marehemu kupotea kwa kuchukuliwa
kiholela na watu wanaojifanya ni ndugu wa karibu au wasimamizi wa mirathi huku
nia yao ni kupora mali hizo na kuwaacha watoto na wajane wakiwa katika majonzi
ya kufiwa na kupokonywa mali na hivyo serikali kuingia katika jukumu la malezi
ya familia hizo.
‘’Ni afadhali uamue hivi sasa ukiwa na afya njema kuandika
wosia kwani RITA moja ya majukumu yao ni hilo kuandika na kutunza wosia na itasaidia
kutoa maelekezo na muelekeo wa namna mali zako zitakavyogaiwa hivyo kupunguza
au kuondoa kabisa uwezekano wa kuzuka kwa migogoro ya mirathi katika jamii’’ Alisema.
Waziri Simbachawene
alisema usajili wa vizazi na vifo ungekamilika kwa asilimia kubwa kwa nchi
nzima zoezi la sensa lingekuwa ni kazi rahisi na kuwezesha kujenga msingi bora
wa uchumi wa kisasa kwani uwepo wa
taarifa zilizo sahihi za vizazi na vifo husaidia kupanga mipango ya
maendeleo kwa nchi.
Pia ameziagiza Bodi za wadhamini wa Taasisi za Kidini, Asasi
za Kiraia na Vyama vya Siasa kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia maadili na
sheria za nchi ili kuepuka kugogoro na
kupelekea kuzorotesha usimamizi wa mali na utoaji wa huduma kwa jamii kama
inavyobainishwa majukumu yao kupitia katiba zao zilizowasilishwa wakati
wakisajiliwa na kutambulika kisheria kupitia RITA na Wizara ya Mambo ya Ndani.
‘’Bodi za wadhamini zinaposajiliwa zichunguzwe kwa umakini
malengo yao kupitia katiba zao ili kuepuka migongano ya kimaslahi baina yao
inayopelekea baadhi ya wanachama kukosa
haki na kushindwa kutekeleza majukumu yao kama yalivyoainishwa katika katiba
zao’’. Alisema Mhe Simbachawene.
Wakati huo huo ameipongeza Bodi ya ushauri ya RITA iliyomaliza
muda wake kwa kusimamia vizuri majukumu ya wakala na kuwezesha ongezeko la kiwango
cha usajili wa watoto wenye umri chini ya miaka mitano kutoka asilimia 13
(Sensa, 2012) hadi kufikia asilimia 65 Mwaka 2021 sawa na watoto 7,328,985 na
kuifanya Tanzania kuchaguliwa kuwa miongoni mwa nchi tano kati ya nchi 54 za
Afrika, kuwa kinara wa Usajili na kuongoza katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya ushauri ya RITA
iliyomaliza muda wake amesema kuwa wakati umefika kwa Serikali pamoja na wadau
mbalimbali kuamua kwa pamoja kuhusu masuala ya usajili wa vizazi na vifo
kulifanya kuwa ni jambo la lazima na kwa kuiwezesha RITA kwenye rasilimali watu
na fedha ili kuweza kuyafikia makundi yote yenye sifa za kusajiliwa kwani
taarifa zao zitaisaidia serikali katika kutekeleza majukumu yake ikiwemo
kupanga mipango mbalimbali ya maendeleo.
Katika kipindi cha miaka mitatu ya Bodi ya Usauri na Udhamini
ya RITA imetekeleza majukumu mbalumbali ikiwemo Mpango wa Usajili wa Watoto
walio na Umri wa Chini ya Miaka Mitano, Mpango wa kuondoa bakaa ya wasiosajiliwa,
Usajili wa watoto wa miaka 5-17, Usajili wa makundi mengine, Mpango wa Usajili
wa Matukio ya Vifo, Matumizi ya TEHAMA katika shughuli za usajili , Usajili wa
vizazi, vifo, ndoa na Bodi za Wadhamini kielektroniki na Mapitio ya Sheria mbalimbali ikiwemo ya
usajili wa vizazi na vifo sura ya 108.
Bodi ya Ushauri ya Wakala ilipewa jukumu kisheria la
kumshauri Waziri wa Katiba na Sheria kuhusu utendaji na utekelezaji wa majukumu
ya wakala kwa kipindi cha miaka mitatu ambapo hivi sasa bodi hiyo imemaliza
muda wake na kukabidhi rasmi taarifa yake ambayo imeonesha mafanikio makubwa
kwa kipindi hicho.
Comments
Post a Comment