SERIKALI YAITAKA JAMII KUTOA USHIRIKIANO KWENYE VITA DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA KWA WATOTO



                                                                                  
                                                                                            

                                                                                        


XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo amtoa wito kwa jamii kuwa mstari wa mbele kupinga unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya watoto. Bi. Makondo ametoa rai hiyo wakati akizindua Kampeni ya siku 10 za kupinga ukatili dhidi ya watoto leo tarehe 6 juni 2022, jijini Dodoma.

 

Kupitia Kampeni hiyo Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa kushirikiana na wadau wa watoto wamehimiza wazazi, walezi, jamii na wadau wengine kuheshimu haki za watoto na kuwapatia ulinzi stahiki ili kuepusha vitendo vya ukatili vinavyoendelea katika maeneo mbalimbali ya Nchi yetu.

 

Uzinduzi huo ulitanguliwa na maandamano yaliyohusisha waalikwa wote yakianzia viwanja vya Nyerere Square hadi zilipo ofisi za Tume eneo la Kilimani.

 

Kampeni hiyo ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika ambayo hufanyika Juni 16 ya kila mwaka, msingi wake ukiwa ni utetezi wa Haki za Mtoto kama ilivyoelekezwa na Mkataba wa Afrika wa Haki na Ustawi wa Mtoto wa mwaka 1990, unaobainisha kuwa mtoto ana haki ya kuishi, kulindwa, kuendelezwa, kushiriki na kutobaguliwa.

 

Kwa mujibu wa Takwimu za Jeshi la Polisi Tanzania, katika kipindi cha Januari hadi Desemba, 2021 jumla ya matukio 11,499 ya ukatili dhidi ya watoto yalitolewa taarifa katika vituo mbalimbali vya Polisi. Mikoa iliyoongoza ilikuwa ni Arusha (808), Tanga (691), Shinyanga (505), Mwanza (500) na Mkoa wa Kipolisi Ilala (489). Aidha, Makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa ni ubakaji (5,899), mimba kwa wanafunzi (1,677) na ulawiti (1,114).

 

 “Imetosha kwa nchi yetu kushuhudia takwimu kubwa kiasi hiki zikionyesha ukatili wa kijinsia juu ya watoto,” alisema Bi. Makondo.

 

Aidha, Bi. Makondo ametoa rai kwa watendaji wote wa Serikali katika ngazi mbalimbali pamoja na Wadau wa Haki za Watoto kuunga mkono Kampeni hiyo, kwa sababu inasaidia kuongeza uelewa wa watu kuhusu haki na ulinzi wa mtoto na hilo si jukumu la Tume pekee bali jukumu la jamii nzima.

 

 “Ni muhimu kupaza sauti kwa pamoja kukemea vitendo vya ukatili dhidi ya watoto kutokana na kuongezeka kwa taarifa za vitendo vya ukatili katika familia na jamii,” alisema.

 

Kauli mbiu inakayotumika kwenye Kampeni hiyo ni ile itakayotumika katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika ambayo ni “Tuimarishe Ulinzi wa Mtoto; Tokomeza Ukatili Dhidi yake, Jiandae Kuhesabiwa”.

 

 Kaulimbiu hii inaakisi lengo la kampeni hiyo la kuhamasisha jamii kushiriki kuimarisha ulinzi wa mtoto na katika kupinga kwa nguvu zote vitendo vya ukatili dhidi ya watoto.

 

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bw. Mohamed Hamis alisema kwa majonzi kwamba Tume inapinga na kulaani vitendo vya ukatili kwa watoto.

 

 “hakuna siku ambayo inapita bila Vyombo vya Habari kuripoti taarifa za ukatili wanaofanyiwa watoto” alisema Bw. Hamis.

 

Tume imekuwa ikifanya uchunguzi wa malalamiko mbalimbali yanayohusu uvunjwaji wa haki za watoto na kubaini kwamba watoto wengi wanakosa ujasiri wa kutoa taarifa za matukio ya ukatili wanayokutana nayo. Vilevile, baadhi yao wamekuwa wakiyumbishwa na wanafamilia wasio wema na hivyo kuficha maovu yanayotendeka katika jamii.

 

Naye Inspekta Yasinta Kayombo Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto, Polisi Mkoa wa Dodoma aliwasihi watoto wasiogope kutoa taarifa Dawati la Polisi wanapotendewa ukatili na endapo watashindwa basi wawambie wazazi, mwalimu wanayemwamini au mtu mzima wanayemwamini.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA