WATOTO WOTE WENYE UMRI CHINI YA MIAKA MITANO WASAJILIWE: KATIBU MKUU MAKONDO
Uzinduzi wa usajili wa watoto chini ya miaka mitano Mkoani Tabora.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary
Makondo ameagiza wananchi wote wenye watoto wa umri chini ya miaka mitano
kuwasajili na huduma hiyo inatolewa bure.
Bi. Makondo ametoa agizo hilo wakati akizindua
Mpango wa usajili wa watoto wa umri chini ya miaka mitano katika mkoa wa
Tabora, leo tarehe 03 Juni, 2022, ambapo hadi sasa Mikoa 22 nchini imenufaika
na mpango huo tangu ulipozinduliwa hapa nchini mwaka 2015.
Mpango huo unatekelezwa na Wakala wa Usajili,
Ufilisi na Udhamini (RITA) kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali wa Maendeleo
una lengo la kuboresha hali ya usajili wa vizazi nchini.
Mbali na kufungua mlango wa haki ya kutambuliwa
kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano, mpango huo umekuwa na matokeo
makubwa ya utatuzi wa changamoto mbalimbali zilizokuwa zinaikabili Serikali na
wananchi kuhusiana na usajili wa vizazi.
“Cheti cha kuzaliwa ni haki ya kila mtoto
aliyezaliwa katika ardhi ya Tanzania awe raia na asiye raia, kinachotakiwa ni
wazazi wa mtoto husika kuthibitisha uraia wao kabla taratibu za kumsajili mtoto
hazijaanza,” alisema Bi. Makondo.
Aidha, amewataka wananchi kutoa msaada na
ushirikiano katika zoezi la utambuzi wa wazazi wenye sifa za kusajili watoto
wao ili wapewe vyeti vya kuzaliwa.
Serikali imeipongeza RITA, Ofisi za Wakuu wa Mikoa
na Wilaya pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika Mikoa yote ambayo
Mpango huu unatekelezwa kwa namna wanavyoratibu zoezi hili kwa ufanisi mkubwa.
Kwa kutambua mchango mkubwa wa Wadau wa Maendeleo
katika utekelezaji wa mpango huo, Bi. Makondo ameshukuru Shirika la Umoja wa
Mataifa linalohudumia Watoto (UNICEF) na Serikali ya Canada.
Aidha, ameshukuru Kampuni ya Mawasiliano ya TIGO
pamoja na wadau wengine kwa kuendelea kuwa sehemu ya utekelezaji wa mpango huu
muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu.
Kwa upande wa Watendaji wa Kata na Wasajili katika
Vituo vya Afya, Bi. Makondo amewaagiza kufanya kazi kwa weledi, uadilifu na
uzalendo wa hali ya juu. “Serikali haitamfumbia macho yeyote atakayekiuka
taratibu na kukwamisha Mpango huo,” alisema.
Comments
Post a Comment