WAZIRI NDUMBARO AAGIZA KUKAMILIKA KWA UJENZI WA MAHAKAMA YA HYDOM KABLA YA JUNI 19, 2022.
Waziri Dkt. Ndumbaro atembelea mahakama ya Hydom wilayani Mbulu.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas
Ndumbaro ameagiza kukamilika haraka kwa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo
inayojengwa kwenye eneo la Hydom wilayani Mbulu na kuanza kutoa huduma ifikapo
June 30, 2022 ili kuokoa wananchi wanaofuata huduma za kimahakama umbali wa
hadi kilomita 86 na kutumia zaidi ya Shilingi laki moja kwa mwezi.
Dkt. Ndumbaro ametoa agizo hilo tarehe 5 Juni,
2022 wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa
hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya CCM Hydom wakitaka kujua lini Mahakama
hiyo itaanza kazi.
" Mheshimiwa Hakimu upo hapa na Mkurugenzi
natoa maelekezo hakikisheni ifikapo June 19, 2022 ujenzi uwe umekamilika na
June 30, 2022 Mahakama ianze kutoa huduma kwa wananchi, isipokamilika nitakuja
mwenyewe kujua nani huyo anayekwamisha mchakato wa Mahakama hii kukamilika na
kutoa huduma kwa wananchi wa Hydom" alisema Dkt. Ndumbaro.
Aidha, Dkt. Ndumbaro amewataka Wananchi kuitumia
Mahakama hii kuleta amani na kutenda haki kwa wananchi.
Naye Mbunge wa jimbo la Mbulu Vijijini, Mhe.
Flatey Maasay ameeleza kuwa wananchi wa eneo la Hydom hulazimika kutembea
umbali wa hadi kilomita 86 kufuata huduma hizo za kimahakama eneo la Mbulu
mjini na wakati mwingine kushindwa kurudi hivyo kulazimika kulala na kutumia
gharama zaidi
" hapa sisi kama wananchi husafiri kilomita
86 hadi Mbulu mjini kwenda na kurudi ni Shilingi elfu 12 na wakati mwingine
shughuli za kimahakama huchelewa kuisha na kupelekea mtu kulala Mbulu kwani
magari ya kurudi Hydom huishia kati ya saa tisa na saa kumi jioni" alisema
Mhe. Maasay
Nao wananchi wa eneo la Hydom wamepongeza na
kushukuru Serikali kwa kujenga Mahakama hiyo kwani wamekuwa wanapata tabu sana
kusafiri umbali mrefu.
Comments
Post a Comment