KISWAHILI KINAFANYA MAHAKAMA KUTEMBEA ‘KIFUA MBELE’
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akipokea maandamano ambayo yanahusu Kiswahili na haki kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Utamaduni Duniani (MASIKIDU).
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema mwelekeo wa
Serikali katika kukiendeleza Kiswahili unafanya Mahakama kutembea ‘kifua mbele’
kwa kuzingatia usemi wa “Thamini chako”.
Mhe. Ndumbaro amesema hayo Julai 4, 2022 Uwanja wa Uhuru jijini Dar es
salaam wakati anapokea maandamano ambayo yanahusu Kiswahili na haki kuelekea
Maadhimisho ya Siku ya Utamaduni Duniani (MASIKIDU).
“Kiswahili chetu tu, ndicho tunachopaswa kujivunia kila siku, lugha za
wengine siyo zetu. Kwa hiyo, Kiswahili ndiyo lugha pekee ambayo imetufanya
Watanzania kwa miaka sitini ya uhuru, kuishi pamoja na kufanya shughuli zetu
kwa undugu, utulivu, amani na umoja.
Hatua hiyo imekifanya Kiswahili kupigiwa upatu kitumike katika masuala
yote ya kisheria ikiwa ni pamoja na kanuni zake zote ambapo Mahakama ya
Tanzania ikiwa mdau wa Kiswahili wanaamini uamuzi unaofanywa na serikali ni wa
kizalendo na utawawezesha Watanzania na wananchi kupata fursa za kushiriki
katika shughuli za ukalimani, tafsiri, uhariri, uandishi na uchapishaji wa
vitabu vya sheria kwa Kiswahili.
Hizi ni jitihada za kuwawezesha wananchi kupata haki zao za kuelewa
kinachoamriwa na kuandikwa katika michakato ya uendeshaji wa mashauri kuanzia
ngazi za mabaraza ya usuluhishi hadi mahakama za juu.
Mhe. Dkt. Ndumbaro ameigiza Wizara ya Katiba na Sheria kushirikiana na
Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA)
kuendelea kutafsiri Sheria na Kanuni zote kwa Kiswahili ili wananchi wawawe na
nafasi ya kupata uelewa wa mwenendo wa kesi zao na hatua inayosaidia kupata
haki zao bila kumwonea mtu.
Aidha, Waziri Dkt. Ndumbaro amesema kuwa Mahakama za Tanzania utaratibu
wa kuwa Mahakama za kimtandao na kutafuta programu ya akili bandia ambao ni
mfumo wa kutafsiri na kuandika taarifa za mashauri mahakamani kwenye lugha
zaidi ya kumi ikiwamo lugha ya Kiswahili.
Zaidi ya hayo, amesema Programu hiyo itakuwa na hatimiliki ya modeli ya
Kiswahili na itakuwa chini ya Mahakama ya Tanzania ili Mahakama zingine duniani
zikitaka kutumia, lazima wapate kibali cha Mahakama ya Tanzania na walipe tozo
ya leseni ambayo ni chanzo cha mapato kwa Serikali.
Naye Katibu Mtendaji wa BAKITA Bi. Consolata Mushi amesema kuwa Tanzania
ndiyo asili ya Kiswahili ambapo Kiswahili kinatumika kutoka kunakucha hadi
kunakuchwa, watu wanaitumia lugha hiyo katika kutekeleza majukumu yao kitaifa,
kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Comments
Post a Comment