SERIKALI YADHAMIRIA KUWEKA MISINGI THABITI KATIKA KUIMARISHA UPATIKANAJI WA HAKI – KATIBU MKUU MAKONDO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo akifungua kikao cha Wakuu wa Taasisi cha kupokea maoni kuhusu Rasimu ya Sera ya Taifa ya Mashtaka ya Mwaka 2022.Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango Bw. Emmanuel Mayeji akimkaribisha Katibu Mkuu kufungua kikao.
Washiriki wakichangia mada.
Washiriki wakimsikiliza Katibu Mkuu.
Picha ya pamoja.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Serikali ya Tanzania imedhamiria kuweka misingi thabiti ya
kisera na kiutawala katika kuimarisha upatikanaji wa haki jinai nchini.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bi.
Mary Makondo wakati akifungua kikao cha Wakuu wa Taasisi cha kupokea maoni
kuhusu rasimu ya Sera ya Taifa ya Mashtaka ya mwaka 2022 leo tarehe 26,
Septemba 2022 Mkoani Singida.
Bi Makondo amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania imekuwa ikifanya maboresho katika mifumo ya Haki Jinai, maboresho hayo
yanalenga kuimarisha mifumo ya kiutawala na kiutendaji katika kuendesha
mashauri ya jinai nchini.
‘’Matokeo ya maboresho hayo ni kuongezeka kwa ufanisi katika
kuratibu na kusimamia uendeshaji wa mashauri nchini ikiwa na madhumuni ya kuwa
na mfumo thabiti wa uendeshaji wa
mashauri ya jinai ili haki ipatikane kwa mtu anayestahili’’ameongeza Bi.
Makondo
Mbali na hayo Bi. Makondo amesema kutokuwepo kwa sera ya
Taifa ya Mashtaka inayotoa miongozo katika uendeshaji wa mashtaka kumesababisha
athari mbalimbali ikiwemo mlundikano wa mahabusu, ugumu wa kubaini mbinu za
makosa makubwa ya jinai na kutokuwa na mfumo madhubuti wa usimamizi wa
mashauri.
Vilevile, Bi. Makondo ameongeza ‘’Kwa kutambua hilo Serikali
kwa kushirikiana na Wadau wa Haki Jinai wameandaa Rasimu ya Sera ya Taifa ya
Mashtaka ili kuwezesha kuimarisha huduma
jumuishi za uendeshaji wa mashauri ya jinai nchini ili kufanikisha uwepo wa
amani na usalama katika jamii’’
Awali akimkaribisha Katibu Mkuu kufungua kikao hicho Kaimu
Mkurugenzi wa Sera na Mipango Bw. Emmanuel Mayeji amesema Serikali ya Tanzania
imekuwa ikifanya maboresho katika kuimarisha uendeshaji wa mashauri nchini,
maboresho makubwa yaliyofanyika ni pamoja na kuanzisha Ofisi ya Taifa ya Mashtaka mwaka 2018.
Aidha, Bw. Mayeji aliongeza kuwa Maboresho hayo yalilenga kuimarisha
mifumo ya kiutawala na kiutendaji wa kuendesha mashauri ya jinai.
Comments
Post a Comment