KUTUNGWA KWA SHERIA YA UFILISI KUTAPUNGUZA CHANGAMOTO ZA MFUMO WA UFILISI NCHINI


 Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akiongea mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Dkt. Joseph Mhagama akiongea wakati wa uwasilishaji wa taarifa ya RITA kuhusu mafanikio na changamoto katika utekelezaji  wa uratibu wa majukumu ya usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu, Ufilisi na Udhamini

Afisa Mtendaji Mkuu wa RITA Bi. Angela Anatory akiwasilisha taarifa kuhusu mafanikio na changamoto katika utekelezaji  wa uratibu wa majukumu ya usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu, Ufilisi na Udhamini kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria

XXXXXXXXXXXXXX

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema Taasisi nyingi zimekuwa zinafanya ufilisi nchini kutokana na kuwa na sheria nyingi za ufilisi, hivyo kukiwa na sheria ya ufilisi moja kutawezesha Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) waendelee na shughuli yake ya ufilisi kwani ndiyo Taasisi pekee iliyopewa jukumu la ufilisi.

Hayo ameyasema wakati Afisa Mtendaji Mkuu wa RITA Bi. Angela Anatory akiwasilisha taarifa kuhusu mafanikio na changamoto katika utekelezaji  wa uratibu wa majukumu ya usajili wa Matukio Muhimu ya Binadamu, Ufilisi na Udhamini kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria leo Oktoba 27, 2022 jijini Dodoma.

Katika taarifa hiyo RITA wamependekeza kutungwa kwa sheria ya  Ufilisi ili kuweza kukabiliana na changamoto zinazoukabili mfumo wa ufilisi nchini.

Akitaja changamoto hizo katika taarifa yake Bi. Anatory amesema uwepo wa sheria nyingi zinazosimamia ufilisi nchini ni moja ya changamoto inayowakabili katika mfumo wa ufilisi.

Ameongeza kuwa Uwepo wa mamalaka nyingi za usimamizi wa masuala ya ufilisi, sheria kutoainisha taratibu za ufilisi unaovuka mipaka, kutokuwepo kwa chombo cha kusimamia wataalam wa ufilisi na kukosekana kwa usalama wa malipo ya waajiriwa wakati wa ufilisi wa kampuni ni miongoni mwa changamoto zinzoikabili Wakala katika utekelezaji wa jukumu lake la Ufilisi.

Bi Anatory amesisitiza kuwa Serikali iangalie namna gani taasisi zake zitabadilishana taarifa na kutunziana mifumo kwa gharama nafuu kwani huduma hiyo kwa sasa imekuwa ikitolewa kwa gharama kubwa.

Afisa Mtendaji huyo pia ameelzea huduma zao za usajili wa vizazi, vifo, ndoa, talaka na watoto wa kuasili na udhamini namna ambavyo zimefanikiwa kutokana na elimu inayotolewa kwa jamii na kampeni mbazo wamekuwa wakizifanya katika Mikoa mbalimbali.

Aidha, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Dkt. Joseph Mhagama ameishukuru wizara namna ambavyo inaishirikisha kamati katika mambo mbalimbali na hivyo kuiwezesha Kamati hiyo kupata uelewa wa kutosha kuhusu majukumu yake.

Miongoni mwa mambo yaliyohitaji ufafanuzi kutoka kwa Wabunge  ni pamoja na umri sahihi wa kuoa na kuolewa, suala la mirathi, usajili wa vizazi na changamoto ya sheria ya ufilisi. Dkt. Ndumbaro alitoa ufafanuzi na kuahidi maelezo zaidi yatatolewa kwa maandishi.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA