MAWAKILI WA SERIKALI TEKELEZENI MAJUKUMU YA SERIKALI KWA KUZINGATIA SHERIA – DKT. NDUMBARO


 
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akizungumza na Mawakili wa Serikali wakati akifunga mkutano wa siku tatu wa Mawakili hao jijini Dodoma.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo (kushoto) na Kabidhi Wasii Mkuu wa RITA Bi. Angela Anatory wakifuatlia hotuba ya kufunga Mkutano wa Mawakili wa Serikali.



Mawakili wa Serikali wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi.

XXXXXXXXXXXXXXXX


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas ndumbaro amewaasa Mawakili wa Serikali kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria kwa maendeleo ya nchi.

Dkt. Ndumbaro ameyasema hayo wakati akifunga mkutano Mkuu wa Mawakili wa Serikali leo tarehe 30 Septemba 2022 katika ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete Convention Centre jijini Dodoma.

Dkt. Ndumbaro amesema ‘’ katika kauli mbiu yenu nimeona kuna mambo kadhaa ikiwemo uzingztiwaji wa sheria, hivyo sisi Mawakili wa Serikali tuhakikishe kwamba utekelezaji wa majukumu ya Serikali popote mlipo unazingatia sheria kwa maendeleo ya Taifa’’.

Dkt Ndumbaro ameongeza kuwa Wizara inategemea kupitia Chama cha Mawakili wa Serikali mchango mkubwa utapatikana katika sera, Katiba na haki za binadamu kwani Serikali imekuwa ikishambuliwa sana katika maeneo hayo.

Amesisistiza, ‘’maeneo ya Katiba na Haki za Binadamu yawekewe mkazo kutokana na hoja mbalimbali zinazoibuliwa na wananchi ikiwemo mahitaji ya Katiba Mpya’’.

Vilevile, Dkt. Ndumbaro amemtaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara Mawakili wa Serikali ili kuwajengea uwezo na kuweza kuisaidia Serikali hasa katika maeneo ya Uendeshaji Mashtaka, Msaada wa Kisheria na Maliasilia za nchi.

Aidha, Dkt. Ndumbaro amewaasa Mawakili wa Serikali kujiepusha na vitendo vya rushwa kwani vinawavunjia heshima na uaminifu kwenye jamii katika kutenda kazi zao kutokana na watu wanaowapa rushwa kuwatangaza kwenye jamii.

Zaidi ya Hayo, Dkt. Ndumbaro amewasisitiza Mawakili hao wa Serikali kutunza siri za Serikali na kujikita kwenye matumizi ya TEHAMA yanayozingatia sheria na weledi na kuepuka kutumia vibaya mitandao na kuchafua sifa ya Serikali.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Feleshi amewaasa viongozi wa muda walioteuliwa na Chama cha Mawakili wa Serikali kuwa watiifu na kujitolea kwa moyo katika kutenda kazi za chama hicho na pia kujiepusha na mambo ya kisiasa kwani chama hicho sio cha kisiasa.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA