WIZARA YA KATIBA KUTOA HUDUMA ZA KISHERIA KIDIJITALI – DKT NDUMBARO


Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro akifungua warsha ya siku mbili kwa watoa Huduma za Msaada wa Kisheria.
Washiriki wakiendelea na pamoja.

Picha ya pamoja.


XXXXXXXXXXXXXXX


Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro amesema Wizara ya Katiba na Sheria imekusudia kuhakikisha huduma za kisheria zinazotolewa na Wizara na Taasisi zilizo chini yake zinapatikana kwa njia ya TEHAMA.

Dkt. Ndumbaro ameyasema hayo wakati akifungua warsha ya siku mbili kwa Wasajili Wasaidizi wa Watoa Huduma za Msaada wa Kisheria, Wasaidizi wa Kisheria, Mawakili, Wanasheria na Maafisa wa Jeshi la Magereza ambayo inafanyika kuanzia leo Oktoba 17, 2022 Jijini Arusha.

Dkt Ndumbaro amesema “Kwa kutambua umuhimu wa TEHAMA kwenye utoaji wa huduma, Wizara ya Katiba na Sheria imekusudia kuhakikisha huduma za kisheria zinazotolewa na Wizara na Taasisi zilizo chini yake zinapatikana kwa njia ya TEHAMA. Hili litawezesha huduma kupatikana kwa wakati na hatimaye kuwezesha vyombo vingine vya utoaji haki kutoa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.”

Dkt. Ndumbaro ameongeza kuwa TEHAMA imekuwa na mchango mkubwa kwenye utoaji wa huduma na utendaji wa Serikali kwa ujumla. Faida zinazopatikana ni pamoja na  kuwepo kwa utunzaji wa kumbukumbu sahihi za wananchi, kuweka  uwazi na uwajibikaji wa utoaji huduma hususan panapokuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi, kurahisisha upatikanaji wa huduma, na vilevile kuondoa mianya ya rushwa kwenye utoaji huduma kwa kuwa  hakuna mwingiliano kati ya mtoa huduma na mteja.

Dkt. Ndumbaro alisisitiza kuwa ni vyema kuwa na mifumo mizuri ya kisheria ambayo itarahisisha upatikanaji wa haki kwa wakati; mifumo ambayo itawezesha wananchi kupata huduma za kisheria popote walipo kwa gharama nafuu katika kuifikia haki. Uwepo wa mifumo, utawapunguzia wananchi muda na gharama za kushughulikia masuala ya kisheria na badala yake watajikita zaidi katika shughuli zingine za kiuchumi na kimaendeleo hivyo basi kuleta maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Aidha, Dkt. Ndumbaro aliongeza kuwa Wizara ina jukumu kubwa la kutoa elimu ya Katiba  na Sheria kwa wananchi hususan vijana kwani hiyo itawasaidia kujua sheria na kudai haki zao.

Dkt. Ndumbaro amesema “Naamini kwamba Wizara ina jukumu kubwa la kutoa elimu ya Katiba kwani huwezi kwenda kutoa kitu kipya wakati hujui cha zamani, tupate elimu ya Katiba iliyopo sasa ili tujue mazuri yakwenda nayo katika Katiba mpya na kuacha mabaya yaliyopo.”

Akimkaribisha Waziri Ndumbaro kufungua warsha hiyo, Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa Bw. David Lyamongi amesema Wasaidizi wa kisheria wapewe kipaumbele katika kutekeleza kazi zao kwani wanasaidia sana jamii hasa wajane na yatima.

Bw. Lyamongi amesema “mchango wa Wasaidizi wa Kisheria ni mkubwa sana katika jamii hususan katika Mkoa wa Arusha kwenye masuala ya kisheria yaliyomshinda mwananchi au kushindwa kwenda mwenyewe mahakamani hivyo kuhitaji uwakilishi.”

Msajili wa Watoa Huduma za Msaada wa Kisheria nchini Bi. Felistas Mushi amesema mafunzo hayo yamewashirikisha Watoa Huduma za kisheria kutoka kwenye Mashirika kumi na tano, Wasajili Wasaidizi na Maafisa Magereza kutoka mikoa kumi ya Tanzania Bara. Washiriki hao wamechaguliwa kwa sababu wapo karibu na wananchi sanjali na kuwasaidia wananchi wengi wa chini waliopo kwenye maeneo yao.

Awali akitoa maelezo ya utangulizi Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Bw. Gabriel Ally amesema mafunzo hayo yatafanyika kwa awamu nne kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Bw. Gabriel amesema huduma za TEHAMA zinarahisisha kufikisha huduma za kisheria kwa wananchi popote pale walipo hivyo ni muhimu makundi hayo manne yakazingatia mafunzo hayo katika utendaji kazi wao kwa kuwa zinahusiana na wananchi kwa kiasi kikubwa.

Mafunzo haya yanahusisha mifumo inayohusu usajili wa watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria ambazo zinatolewa chini ya Sheria ya Msaada wa Kisheria ya Mwaka 2017, mfumo wa usajili wa watoa huduma za maridhiano, usuluhishi, na upatanishi kama ilivyobainishwa chini ya Sheria ya Usuluhishi ya Mwaka 2020.  Mifumo mingine ni pamoja na uwasilishaji wa malalamiko, maombi ya huduma za msaada wa kisheria, maombi ya kuongezewa muda wa kuwasilisha mashauri mahakamani nje ya muda pamoja na huduma nyingine za kisheria.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA