WATUMISHI KATIBA NA SHERIA WATAKIWA KUCHAPA KAZI NA KUZINGATIA UADILIFU NA NIDHAMU

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akiongea na watumishi wa Wizara hiyo.


Viongozi waliowahi kuongoza katika wizara hiyo kwa nafasi mbalimbali wakikabidhiwa zawadi.


Watumishi wastaafu wakikabidhiwa zawadi.

XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Watumishi wa Wizara ya Katiba na Sheria wametakiwa kuelewa majukumu waliyonayo si lelemama hivyo wayatekeleze kwa kuzingatia uchapakazi, uadilifu, nidhamu na kufanya kazi kama timu ili kuweza kuleta matokeo mazuri ya kazi zao.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro Novemba 3, 2022 jijini Dodoma alipokutana na kufanya mazungumzo na watumishi hao kabla ya hafla ya kuwaaga viongozi na watumishi wa Wizara hiyo waliostaafu.

Waziri Ndumbaro amesema ‘’Wizara hii ni wizara kubwa na nyeti kwa sababu imeshikilia Katiba ya nchi, pia inashughulika na sheria ambayo ndiyo kila kitu katika utawala wa nchi’’

Dkt. Ndumbaro ameongeza kuwa ‘’Nataka muelewe kwamba jukumu tulilonalo si lelemama tutaweza kulitekeleza tukizingatia uchapakazi, uadilifuna nidhamu na kufanya kazi kama timu’’

Dkt. Ndumbaro amesisitiza kuwa ni lazima watumishi wajitume, wawe na maadili na nidhamu ya kazi na Wakuu wa Idara na Vitengo wajue uwezo wa watumishi wanaowasimamia ili kujenga taswira mpya ya wizara.

Mbali na hayo Dkt. Ndumbaro amewaasa watumishi hao kuwa ‘’wajibu wetu ni kuendelea kushirikiana tuishi kama familia, nataka hii wizara iwe sehemu nzuri Zaidi ya mtu kufanya kazi’’

Naye Katibu Mkuu Bi. Mary Makondo amemhakikishia Waziri kuwa maelekezo yake yamepokelewa na kumuahidi watumishi watafanya kazi kwa bidii na kuendelea kuwa wabunifu ili kuleta matokeo chanya kwa wizara.

Bi. Makondo amesema ‘’tukuahidi tumesikia maelekezo yako na tutaendelea kuwa wabunifu, tuna jukumu kubwa la kuwajibikja ipasavyo na tutafanya kazi kwa weledi’’.

Wakati huohuo kwenye hafla ya kuwaaga viongozi na watumishi waliostaafu Dkt. Ndumbaro aliwashukuru kwa utumishi na kuthamini mchango wao katika kipindi walichotumikia wizara hii kwa kuwakabidhi zawadi mbalimbali kama ukumbusho kwao.

Viongozi waliowahi kuongoza wizara hii na kuagwa jana ni pamoja na Mhe. George Simbachawene, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, Prof. Sifuni Mchome na Bw. Amon mpanju.

Watumishi wengine walioagwa ni Bw. Simbaufoo Swai, Bi. Diana Makule, Bi. Iluminata Matindi na Bw. Amani Goha.

 

Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA