DKT NDUMBARO AZINDUA KANUNI ZA WATOA TAARIFA
Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro akizindua Kanuni za Watoa Taarifa na Ulinzi wa Mashahidi, tarehe 28 Februari 2023, Kulia Naibu Waziri Pauline Gekul na Kushoto Naibu Katibu Mkuu Khatibu Kazungu.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
Na Mwandishi wetu, Dodoma
Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt Damas Ndumbaro amezindua Kanuni za
Watoa Taarifa na Ulinzi wa Mashahidi za mwaka 2023 na kueleza kuwa Kanuni hizo
zitasaidia kufichua uhalifu na kuimarisha utoaji haki jinai.
Dkt Ndumbaro ameyasema hayo wakati wa kuzindua Kanuni hizo hatua
ambayo inaashiria kuanza utekelezaji wa Sheria ya Watoa Taaarifa na Ulinzi wa
Mashahidi ya mwaka 2016.
Katika uzinduzi huo ambao umefanyika tarehe 28 Februari, 2023 Dkt
Ndumbaro amesema kanuni hizo zinaenda kusaidia uimarishaji utoaji wa haki jinai
kwa sababu zinahusu utoaji wa taarifa za ukiukwaji wa sheria mbalimbali, makosa
ya jinai, wizi wa mali za umma na ufisadi.
“Watoa taarifa hizi ni muhimu sana kwenye jamii, wanatwambia mali ya
umma inaibiwa, katika historia ya nchi hii watoa taarifa wamesaidia kufukua
mambo mengi yenye maslahi kwa jamii lakini walikuwa hawatambuliki kisheria.”
Aidha, Dkt
Ndumbaro alisema sehemu ya pili ya kanuni hizo ni ulinzi wa mashahidi na kuwa
ni eneo ambalo lilikuwa limelegalega hasa kwenye mfumo wa haki jinai.
“Kuna wakati
mashahidi walikuwa wanaogopa kwenda kutoa ushahidi akihofia madhara ya yeye
kutoa ushahidi.” Dkt Ndumbaro alisema uwepo wa sheria na kanuni hizo zinabeba
mambo makuu matatu ambayo ni utawala bora, utoaji wa haki jinai na zinakoleza
vita ya mapambano dhidi ya uhalifu.
“Tunaamini
uzinduaji wa kanuni hizi unaenda kuwa chachu ya watu kuibua makosa mengi zaidi
yanayofanyika kwasababu wanakinga kisheria na kanuni.”
Vilevile, Dk Ndumbaro ameagiza kufanyika kwa
mafunzo na utoaji elimu kwa watanzania na kusisitiza kuwa sheria hiyo ikitumika
vizuri mali za umma zitaokolewa.
“Wale wadokozi
wadokozi, arobaini zao zimefika kwa sheria na kanuni hizi, inakwenda kulinda
uchumi wa nchini na kuwaumbua na kuwaanika wahalifu na kwenda kupunguza uhalifu
unaowaathiri sana wananchi.”
Pia Dkt Ndumbaro
amezitaka mamlaka zinazopaswa kupokea taarifa hizo za uhalifu kuhakikisha zinafika
kwenye vyombo vya dola ambavyo navyo vinatakiwa kutekeleza kwa haraka,
hatua itakayoongeza imani kwa watoa taarifa.
Dkt Ndumbaro
alisema pia kanuni hizo zitavisaidia vyombo vya habari ambavyo navyo vimekuwa
vikipokea taarifa kutoka kwa watoa taarifa na hapo nyuma ulinzi ulikuwa ni
maadili na sasa vitakuwa na kinga ya kisheria.
Naye Naibu Katibu
Mkuu, Dkt Khatib Kazungu alisema watoa taarifa na mashahidi ni watu muhimu
katika mnyororo wa haki jinai kwani taarifa wanazozitoa zinawezesha kufichua
uhalifu kwenye jamii, na mashahidi wamekuwa wakiongeza ufanisi katika
uendeshaji wa mashauri ya jinai kwa wakati.
“Uwepo wa kanuni hizi utawezesha wananchi
kujisikia huru, kutoa taarifa zozote za uhalifu uliofanyika au unaopangwa
kufanyika na pia utawafanya mashahidi kuwa huru kutoa ushahidi mahakamini kwani
zinawahakikishia ulinzi hatua ambayo itasaidia kuongeza imani.”
Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Katiba na Ufuatiliaji Haki, Kharist Luanda alisema kanuni hizo zinaweka mfumo wa kisheria wa kuwatambua, kuwalinda, kuwalipa fidia na kuwapatia zawadi watoa taarifa na mashahidi kulingana na taratibu na vigezo vilivyowekwa kwenye kanuni.
Comments
Post a Comment