WAZIRI CHANA AIPONGEZA TUME YA KUREKEBISHA SHERIA
Waziri wa Katiba na Sheria Balozi Dkt. Pindi Chana akiwa
katika picha ya pamoja na watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria leo tarehe 22
Septemba 2023 Jijini Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe, Balozi Dkt. Pindi Chana
akiongea na watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria katika ofisi zao zilizopo
udom leo tarehe 22 Septemba 2023 Jijini Dodoma.
Watumishi wa Tume ya Kurekebisha Sheria wakimsikiliza Waziri
wa Katiba na Sheria Mhe, Balozi Dkt. Pindi Chana katika ofisi zao zilizopo UDOM
leo tarehe 22 Septemba 2023 Jijini Dodoma.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Na George Mwakyembe & Faraja
Mhise - WKS.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.
Balozi Dkt. Pindi Chana amekutana na menejimenti pamoja watumishi wa Tume ya
Kurekebisha Sheria ikiwa ni muendelezo wa ziara zake zenye lengo la kuyafahamu
majukumu ya Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Katiba na Sheria tangu ateuliwe
kuwa Waziri wa Wizara hii.
Akiongea na watumishi hao leo
tarehe 22 Septemba, 2023 katika ofisi za Tume ya Kurekebisha Sheria zilizopo
Jijini Dodoma, Mhe. Chana amewapongeza kwa kazi kubwa wanayofanya ya utafiti wa
marekebisho ya Sheria pamoja na kutunga Sheria mpya zenye kuendana na
wakati.
“Tume hii imekuwa ikifanya
vizuri katika ukanda wa Afrika mashariki pamoja na ukanda wa Kusini mwa bara la
Afrika na imekuwa mfano wa kuigwa, pia Tume hii imekuwa ikifanya mapitio
mbalimbali ya Sheria muhimu katika nchi yetu, na wanasheria kutoka nchi
nyingine wamekuwa wakija kujifunza hapa nawapongeza sana “ amesema Mhe.
Chana.
Aidha, Mhe. Chana ameongeza kuwa
Tanzania ni nchi yenye amani, utulivu pamoja na usalama kwasababu
ya kuzingatia Sheria na taratibu za misingi bora ambayo imewekwa. Waziri Chana
aliongeza kuwa Sheria za Tanzania ni bora na ubora wake unatokana na utafiti
mzuri unaofanyika kabla ya kuzitunga sheria hizo lakini pia marekebisho ya
Sheria zenyewe yanayofanyika kila inapohitajika.
Pamoja na pongezi hizo pia Mhe.
Chana alipokea ripoti za mapitio ya mfumo wa sheria inayohusu mdhamini na
mapitio ya mfumo wa Sheria inayohusu maadili ambayo imefanyiwa utafiti na Tume
ya kurekebisha Sheria. Mhe, Chana amehaidi kushirikiana na Tume katika
kushughurikia mambo kadhaa ya kiutendaji yanayoikabili Tume ikiwemo upungufu wa
watumishi ili kuleta mabadiliko makubwa katika maendeleo yaTume na
Wizara.
Katika kikao hicho, Naibu Katibu
Mkuu Dkt. Khatibu Kazungu alisema ufanyaji wa tafiti za Sheria ambazo zinakidhi
mahitaji kutokana na wakati uliopo ni mkakati wa Wizara katika
kuhakikisha Sheria ambazo zinatakiwa kufanyiwa marekebisho basi zinafanyiwa
tafaiti ili ziweze kurekebishwa.
Naye, Mwenyekiti wa Tume Jaji
mstaafu January Msofe amempongeza Waziri Chana kwa kuendelea kuaminiwa na Mhe,
Rais na kuteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Mwenyekiti wa huyo akagusia
baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Haki ya Jinai likiwemo suala la
maadili, vifungo vya watoto, ulipaji wa fidia kwa wathirika na
vifungo, kuwa yote hayo yanafanyiwa utafiti ili kupata Sheria
zilizo bora na tayari wamejipanga kuhakikisha kuwa yote
yaliyopendekezwa na Tume ya Haki jinai yanafanyiwa kazi kwa manufaa
ya watanzania.
Comments
Post a Comment