Pelekeni kwa Wananchi Elimu ya Sheria Mliyopata: Dkt. Kazungu

 

Bw. Burton Mwasomola Mkurugenzi Msaidizi wa Katiba kutoka Wizara ya Katiba na Sheria akihutubia kwa niaba ya Naibu Katibu Mkuu Dkt. Khatibu Kazungu wakati wa kufunga mafunzo ya Sheria ya Ulinzi wa Watoa Taarifa na Mashahidi ya mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2023, tarehe 13 Oktoba, 2023 Morogoro.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Na William Mabusi – WKS Morogoro

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Dkt. Khatibu Kazungu ametoa rai kwa washiriki wa mafunzo ya Sheria ya Ulinzi wa Watoa Taarifa na Mashahidi ya mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2023 kupeleka elimu waliyoipata kwa wananchi ili watambue jitihada zinazofanywa na Serikali za kuendelea kupambana na uhalifu nchini.

Dkt. Kazungu ametoa rai kwenye hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Bw. Burton Mwasomola Mkurugenzi Msaidizi wa Katiba wakati wa kufunga mafunzo ya Sheria ya Ulinzi wa Watoa Taarifa na Mashahidi ya mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2023 kwa Maafisa Waandamizi Wachunguzi kutoka Taasisi Chunguzi na Waendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, tarehe 13 Oktoba, 2023 Mkoani Morogoro.

“Rai yangu mkaendelee kutoa elimu kwa umma wa watanzania na watumishi wenzenu kuhusiana na malengo ya Sheria hii na Kanuni zake ili wafahamu umuhimu wa kuwafichua wahalifu wa makosa mbalimbali ili hatimaye kutokomeza mtandao wa uhalifu nchini,” alisema.

Dkt. Kazungu aliongeza kuwa, “katika kutekeleza majukumu yenu mna watu ambao huwatumia kuwapa taarifa za uhalifu, kupitia mafunzo haya kawaambieni kwamba Serikali imeweka utaratibu wa ulinzi kwao pale ambapo itaonekana maisha yao yako hatarini kutokana na taarifa za uhalifu watakazotoa.”

Akitoa shukrani kwa niaba ya washiriki wengine, aliyekuwa Mwenyekiti wa mafunzo hayo, Wakili wa Serikali Bi. Florida Wenceslaus amesema mafunzo hayo yamewaongezea uelewa wa Sheria ya Ulinzi wa Watoa Taarifa na Mashahidi ya mwaka, 2015 na Kanuni zake za mwaka 2023 na hivyo kwenda kurahisisha utendaji kazi wao kwani utekelezaji wa Sheria hiyo utawapa hamasa wananchi kutoa taarifa za uhalifu.

Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

UONGOZI WA MAHAKAMA YA AFRIKA YA HAKI ZA BINADAMU NA WATU YAKUTANA NA VIONGOZI WA WIZARA YA KATIBA NA SHERIA

BODI YA KITAIFA YA USHAURI YA MSAADA WA KISHERIA YATEMBELEA WASAIDIZI WA KISHERIA IRINGA