NCHI IKITAWALIWA NA RUSHWA HAIWEZI KUFIKIA MALENGO: BI. MAKONDO
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi.
Mary Makondo akihutubia kwenye Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa juhudi dhidi ya
rushwa, tarehe 04 Desemba, 2023 Jijini Dodoma.
Washiriki kwenye Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa
juhudi dhidi ya rushwa, wakisikiliza hotuba, tarehe 04 Desemba, 2023 Jijini
Dodoma.
Meza Kuu kwenye picha ya pamoja na baadhi ya Watumishi wa Serikali kwenye Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa juhudi dhidi ya rushwa, wakisikiliza hotuba, tarehe 04 Desemba, 2023 Jijini Dodoma.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Na William Mabusi – WKS Dodoma
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi.
Mary Makondo amezitaka Taasisi za Serikali na Sekta Binafsi kuweka mazingira ya
kuzuia rushwa, kuepuka na kutokomeza vitendo vya rushwa nchini ili kuliwezesha
taifa kufikia malengo mbalimbali iliyojiwekea katika kuleta maendeleo nchini.
Bi. Makondo ameyasema hayo alipokuwa akihutubia
kwenye Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa juhudi dhidi ya rushwa tarehe 04 Desemba,
2023 Jijini Dodoma lililo hudhuriwa na Wadau kutoka Serikalini, Sekta Binafsi
na Viongozi wa Dini ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki
za Binadamu nchini. Siku ya Maadili na Haki za Binadamu nchini Tanzania ni
jumuisho ya siku mbili za Kimataifa ambazo ni siku ya Kupambana na Rushwa na
Siku ya Haki za Binadamu.
“Sote tunaelewa
rushwa ni adui mkubwa wa maendeleo, nchi ikitawaliwa na rushwa taifa
haliwezi kufikia malengo ililojiwekea katika nyanja mbalimbali. Aidha, rushwa
inakiuka haki za binadamu kwa kuwa ulaji rushwa unapokonya haki za binadamu na
kusababisha huduma mbalimbali kutowafikia wananchi kwa wakati,” alisema.
Siku ya Maadili na Haki za Binadamu ambapo kwa
mwaka huu uzinduzi wake umefanyika tarehe 3 Desemba, 2023 inaadhimishwa sanjari
na shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufanyika kwa Jukwaa la Kitaifa la
wadau wa juhudi dhidi ya rushwa, Maadhimisho ya Wiki ya huduma kwa jamii
yatakayofanyika kwenye viwanja vya Nyerere Square kuanzia tarehe 5 hadi siku ya
kilele Desemba 10, 2023 ambapo wadau wa Serikali na Mashirika yasiyo ya
Kiserikali yanayojihusisha na masuala ya maadili na haki za binadamu watatoa
huduma mbalimbali, watajibu maswali kuhusu haki katika nyanja ya maadili,
kuzuia na kupambana na rusha, utawala bora na haki za binadamu.
Ametaja shughuli nyingine kuwa ni utoaji wa
elimu kupitia Vyombo mbalimbali vya Habari ili kuendelea kuuhabarisha umma juu
ya umuhimu wa kuzingatia maadili, kutokujihusisha na rushwa na kuzingatia haki
za binadamu
Kwenye mjadala uliofanyika kwenye Jukwaa la Kitaifa la Wadau wa Juhudi dhidi ya rushwa washiriki wamesisitiza elimu kuhusu maadili mema kuendelea kutolewa ili jamii ijikite katika kufanya mambo mema vile vile wamewataka Watanzania kusimamia mali ya umma kama vile wanavyosimamia mali zao wenyewe kwa faida ya kizazi chetu kijacho na maendeleo ya nchi. Maadhimisho ya siku ya Maadili na Haki za Binadamu
Comments
Post a Comment