“UNYANYASAJI WA KIJINSIA HAUNA NAFASI KATIKA NCHI YETU” DKT. CHANA


 

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana akihutubia wakati akifungua Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia, tarehe 06 Desemba, 2023 Jijini Dodoma.


Washiriki siku ya kufungua Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia, wakimkaribisha ukumbini Mgeni Rasmi Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana tarehe 06 Desemba, 2023 Jijini Dodoma.


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana kwenye picha ya pamoja na baadhi ya viongozi walioshiriki hafla ya kufungua Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia, tarehe 06 Desemba, 2023 Jijini Dodoma.

                                   XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX


Na William Mabusi – WKS Dodoma

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana (Mb) amesema Tanzania inaweza kusonga mbele na kushinda vita dhidi ya Ukatili wa Kijinsia ikiwa wote tutazungumza na kupaza sauti kupinga Unyanyasaji wa kijinsia huku akiitaka jamii kushiriki kikamilifu katika kutoa ushahidi wa matukio ya unyanyasaji wa kijinsia mara inapotakiwa kufanya hivyo.

Ameziagiza Taasisi za dini na Wazee wa kimila, Wanahabari na Wadau wa Maendeleo na wananchi wote wawe tayari kuchukua hatua za maksudi kukomesha ukatili wa kijinsia kwenye jamii zetu kuanzia familia, makazini kwetu na kwenye jamii zetu kwa ujumla.

Dkt. Chana ameyasema hayo alipokuwa akifungua Maadhimidho ya siku 16 za Kupinga Ukatili dhidi ya Kijinsia, tarehe 06 Desemba, 2023 Jijini Dodoma, tukio ambalo limefanyika chuo Kikuu cha Dodoma.

“Tuwaamini wenzetu pale wanapotuambia wananyanyaswa, tuwasikilize na tuwasaidie, na hata tukiwa nyumbani tuwe wasikivu kwa watoto, wakituambia wanafanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia tufuatilie kwa ukaribu na kuchukua hatua za kisheria, tuache kumaliza masuala ya ukatili kifamilia kwani watendaji wataendelea kufanya vitendo hivyo.” Alisema.

Dkt. Chana ameongeza kuwa “ukatili wa kijinsia ni moja ya changamoto kubwa inayorudisha nyuma juhudi za kutambua usawa wa binadamu na utu wa mwanamke katika dunia ya leo, ni zao la mtizamo usio sahihi uliojengeka kwenye mila na desturi katika jamii unaomchukulia mwanamke kama mali ya mwanaume na kwamba ni kiumbe aliyeumbwa kutekeleza utashi wa mwanaume.”

Wakati Tanzania ikifanya Maadhimisho ya kimataifa ya Siku 16 za Kupinga Ukatili wa Kijinsia takwimu zinaonesha kuwepo kwa ongezeko la matukio ya ukatili huo hapa nchini. Ongezeko hilo linatokana na sababu mbalimbali ikiwemo jamii kuwa na uelewa zaidi juu ya madhara yatokanayo na ukatili wa kijinsia na kutoa taarifa za matukio ya ukatili huo katika Madawati ya Jinsia.

Sababu zingine ni mmomonyoko wa maadili, hali ngumu ya maisha ambayo huleta msongo wa mawazo kwa baadhi ya watu na kujikuta wakitenda matukio hayo. Sababu nyingine ni  mila na tamaduni kandamizi, kushamiri kwa mfumo dume katika jamii zetu, matumizi  mabaya ya teknolojia ambayo kwa kiasi kikubwa yamekuwa yakisababisha vijana kufanya vitendo vya kikatili hasa ubakaji wa watoto na wanawake lakini pia kulawiti.

Katika kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia nchini Dkt. Chana amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo ya upatikanaji haki kwa wananchi hususan wanawake, watoto na makundi maalum ikiwa ni pamoja na kutunga sheria mbalimbali, kufanya maboresho ya mara kwa mara ya sheria, kanuni, miongozo na hata sera zinazosimamia usawa na ulinzi wa makundi mbalimbali.

Aidha, Serikali inayo mikakati mbalimbali ya kutoa elimu kwa jamii kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia akiitaja moja ya mikakati hiyo kuwa ni Kampeni Kabambe ya Huduma za Msaada wa Kisheria iitwayo Mama Samia Legal Aid Camapign ambayo inatekelezwa na Wizara ya Katiba na Sheria kwa kushirikiana na Wadau wa masuala ya upatikanaji haki hapa nchini.

Amevipongeza vyombo vya utoaji haki kuhakikisha washukiwa wote wa vitendo vya ukatili wa kijinsia wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria, kushughulikia mashauri kwa wakati na hivyo kesi kuhitimishwa ndani ya muda mfupi.

Dkt. Chana amelishukuru Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ), kwa kushirikiana na Wizara na Chuo Kikuu cha Dodoma katika kuandaa maadhimisho hayo. Amemtaka Makamu Mkuu wa Chuo cha Dodoma Prof. Lughano Kusiluka na Amidi wa Shule ya Sheria Dkt. Ines Kajiru kuendelea kuwajenga wanafunzi wao katika misingi ya kuwa mabalozi wema wa masuala ya ukatili wa kijinsia,

Aidha, ameaomba Wadau wa Maendeleo na Mashirika yanayotetea haki za wanawake na watoto kuongeza mashirikiano ya muda mrefu na usaidizi katika kuunga juhudi za Serikali katika kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia miongoni mwa jamii huku akiyataka mashirika hayo kujikita zaidi katika maeneo ya pembezoni kwani kule ndipo kwenye changamoto zaidi kutokana na ukweli kwamba, elimu ya masuala haya bado haijafika vya kutosha kwahiyo jamii bado inaamini katika mila na desturi.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA