SERIKALI KUANZISHA KITUO CHA KUDUMU KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO
Wakili wa Serikali Bi. Agness
Mkawe kutoka Wizara ya Katiba na Sheria akitoa maelezo kwa Mwanasheria Mkuu wa
Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Feleshi alipotembelea banda la Wizara, kwenye
viwanja vya Nyerere Square, tarehe 28 Januari, 2024.
XXXXXXXXXXXXXXXXX
Na William Mabusi – WKS Dodoma
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe.
Jaji Dkt. Eliezer Feleshi amesema Serikali inaangalia uwezekano wa kuanzisha
kituo cha kudumu Makao Makuu ya nchi kushughulikia kero za wananchi.
Dkt. Feleshi ameyasema hayo
alipoongea na Wanahabari baada ya kutembelea mabanda kwenye viwanja vya Nyerere
Square kunakofanyika maonesho ya Wiki ya Sheria tarehe 28 Januari, 2024.
“Pamoja na maadhimisho ya Wiki ya
Sheria kila mwaka, matumizi ya kurasa za maoni kwenye tovuti, simu za kupokelea
maoni na sasa kuna Mama Samia Legal Aid Campaign ambayo hadi sasa imetekelezwa
kwenye mikoa sita Tazania Bara tungeweza kusema sasa mifumo ya kupokelea maoni
na malalamiko inatosha, lakini unaona malalamiko yapo, bado wananchi wana kero,
mfano migogoro ya ardhi na mirathi.” Amesema na kuongeza “Hivyo Serikali
kupitia Wizara ya Katiba na Sheria kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria
Mkuu wa Serikali na Wadau wengine tutaangalia uwezekano wa kuanzisha kituo cha
kudumu kama njia ya nyongeza ya kutoa huduma za kisheria kwa maana ya
kuelimisha umma masuala ya sheria, kupokea malalamiko na kutoa huduma za
kisheria.”
Maadhimisho ya Wiki ya Sheria kwa
mwaka 2024 yamezinduliwa tarehe 27 Januari, 2024 na Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano Dkt. Tulia Ackson na hitimisho ni tarehe 01 Februari, 2024.
Comments
Post a Comment