TUTAENDELEA KUTOA ELIMU NA KUTATUA CHANGAMOTO ZA KISHERIA KWA WANANCHI


Katibu Tawala wa Wilaya Singida Bi. Naima Bakari Chondo, akiongea baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa MSLAC katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida, tarehe 19 Januari, 2024.

Bi. Basuta Milanzi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa MSLAC katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida kwa Katibu Tawala wa Wilaya Singida Bi. Naima Bakari Chondo, tarehe 19 Januari, 2024

XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Na William Mabusi – WKS Singida

Katibu Tawala wa Wilaya Singida Bi. Naima Bakari Chondo ameahidi kutekeleza changamoto za wananchi ambazo hazikutatuliwa katika kipindi cha kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ili kuendelea kutatua migogoro kwenye jamii.

Bi. Naima ametoa kauli hiyo baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa Kampeni hiyo iliyokuwa inafanyika kwenye Halmashauri yake kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Singida, tarehe 19 Januari, 2024.

Aidha, akiongelea changamoto za kesi za ukatili wa kijinsia amesema, “ipo changamoto ya kesi za ukatili wa kijinsia na kuzifanya kuwa ngumu kuendesha na wakati mwingine kutofika mwisho kutokana na Mahakama kukosa ushahidi wakati ni kweli kabisa kitendo cha ukatili kimefanyika, niwaombe waathirika na wazazi kutokukubali kumaliza kesi kifamilia, maamuzi ya namna hii hayamtendei haki mwathirika.”

Katika hatua nyingine Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Singida Bi. Esther Chaula amesema kwa kutumia rasilmali kidogo waliyonayo wataendelea na utoaji elimu ya sheria kwa wananchi.

“Maeneo yaliyobaki tutajipanga na watu wangu kwa kadri tutakavyoweza kutumia rasilmali tuliyonayo na kupitia mikutano kutoa elimu ya kisheria na kuendelea kutatua migogoro kwenye jamii. Unakuta mwananchi hakuridhika na uamuzi wa Mahakama, kwa kutokujua masuala ya sheria anarudi tena Halmashauri. Wakati mwingine mwananchi anafanyiwa ukatili bila kujua ni ukatili na wakati mwingine hata akijua ametendewa ukatili hajui afanye nini.” Alisema Bi. Chaula.

Ameshukuru Wizara ya Katiba na Sheria  akisema kitendo cha kuwafuata wananchi kuwapa elimu na huduma ya msaada wa kisheria kinawadhihirishia kwamba Serikali iko karibu na wananchi. “Kupitia hii kampeni mmetuongezea maarifa kwani watumishi mliokuwa mnazunguka nao kutekeleza kampeni kuna jambo wamejifunza, hivyo tutawatumia kufika maeneo ambayo hamkuweza kufika.”

Kampeni ya Kitaifa ya kutoa elimu na huduma ya msaada wa kisheria ya Mama Samia Legal Aid Campaign ilizinduliwa  Mkoani Singida na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana tarehe 10 Januari, 2024 na kufanyika kwa siku kumi kwenye Halmashauri zote saba za mkoa huo na leo ndiyo imehitimishwa.


Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA