WANANCHI WASHAURIWA KUIBUA KERO NZITO NZITO KUITWISHA MSLAC


 Afande Veronica Masele kutoka Dawati la Jinsia na Watoto Halmashauri ya Wilaya ya Singida akitoa mada ya ukatili wa kijinsia kwa wanafunzi wa shule ya sekondari ya Ikhanoda, 16 Januari, 2024.

Afisa Ardhi wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida Bi. Paskazia Kyaruzi akitoa mada kuhusu masuala ya ardhi, tarehe 16 Januari, 2024 Kijiji cha Ikhanoda.

XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

Na William Mabusi – WKS Singida

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kijiji cha Ikhanoda Kata ya Ikhanoda katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida Bw. Jumanne Idabu amewataka wananchi kuibua kero ambazo zimeshindika na kuitwisha Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia Legal Aid Campaign (MSLAC) ili zitatuliwe.

Bw. Idabu alitoa kauli hiyo kwenye mkutano wa kutekeleza kampeni hiyo uliofanyika kijijini hapo tarehe 16 Januari, 2024 ukihudhuriwa na wakazi wa vijiji vya Ikhanoda na Msimihi.

“Wananchi ibueni kero nzito ambazo walau zimeshachukuliwa hatua katika ngazi mbalimbali bila mafanikio ili Kampeni hii itusaidie,” alisema.

Katika mkutano huo wananchi walilalamikia Kampuni ya Majembe Auction Mart kushindwa kubomoa nyumba za mwanakijiji mwenzao ambaye amemega na kujimilikisha eneo la shule ya Msingi ya Ikhanoda lenye ukubwa wa hekari kumi na saba. Maamuzi kuhusu mgogoro huo yalishaamuriwa na Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Singida tarehe 14 Machi, 2022. Halmashauri ya Kijiji iliamua kuingia mkataba na Majembe Auction Mart baada ya mvamizi huyo kushindwa kuondoka kwa hiari baada ya siku kumi na nne alizokuwa amepewa na Baraza.

Akithibitisha kero hiyo Bw. Idabu amesema viambatisho vyote, kuanzia kushinda shauri hilo hadi vya malipo ya gharama za ubomoaji kwa kampuni ya Majembe wanavyo. Kampuni hiyo imelipwa gharama hizo tangu mwezi Desemba 2022.

Akijibu swali hilo kwa niaba ya timu ya MSLAC inayotekeleza kampeni kwenye Halmashauri hiyo, Mwanasheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Singida Bi. Lela Salum amesema kero hiyo ameichukua na itafikishwa vyombo husika ili Majembe Auction Mart wachukuliwe hatua.

Awali akitoa mada ya ardhi Afisa Ardhi wa Halmashauri hiyo Bi. Paskazia Kyaruzi alishauri wamiliki wa ardhi kuhakikisha wana hati za umiliki wa maeneo yao zinazotolewa na Serikali. Akitaja faida za umiliki wa ardhi yenye hati kuwa ni pamoja na kupandisha thamani ya ardhi, kuepusha migogoro na pia hati kutumika kama dhamana ya mkopo benki.

Kampeni hiyo ya Kitaifa iliyozinduliwa kutekelezwa kwenye Halmashauri zote mkoani humo na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana tarehe 10 Januari, 2024 itafikia tamati tarehe 19 Januari, 2024.

Comments

Popular posts from this blog

KAMATI YAIPONGEZA WIZARA KWA UTEKELEZAJI WA MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA