KUNA SULUHISHO LA KERO ZENU NDANI YA SERIKALI – MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

 

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akihutubia alipokuwa anazindua Kliniki ya sheria, Juni 26, 2024 Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo akitoa salaam kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi kuzindua Kliniki ya sheria, Juni 26, 2024 Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dodoma.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akimsikiliza Mwenyekiti wa Umoja wa Wataafu Tanzania wanaolipwa na Hazina mzee John Joseph Kanyeto akitoa kero yake kabla ya kuzindua Kliniki ya sheria, Juni 26, 2024 Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dodoma.

Meza Kuu kwenye picha ya pamoja na Mawakili wa Serikali kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya uzinduzi wa Kliniki ya sheria, Juni 26, 2024 Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dodoma.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

William Mabusi – WKS Dodoma

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi amewahakikishia wananchi kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha inatatua kero na changamoto zao katika kuimarisha utengamano na utulivu nchini.

Dkt. Feleshi ameyasema hayo alipokuwa anazindua Kliniki ya kutoa ushauri na elimu ya sheria iliyoandaliwa na Ofisi yake, tarehe Juni 26, 2024 Viwanja vya Mwalimu Nyerere Jijini Dodoma. Kliniki hiyo itafanyika kwa wiki nzima kuanzia leo Juni 26 hadi Julai 03, 2024.

“Kliniki hii na zingine zitakazoendelea kuratibiwa na Serikali zimelenga kutoa suluhisho ya kero zenu, kumwezesha mwananchi kupata huduma bora kwa wakati na kuongeza utengamano na utulivu na hivyo kuchochea maendeleo ya jamii. Mahala pasipokuwa na masikilizano na kuwepo namna ya kujadili changamoto au kero mara nyingi kunakuwa na fukuto ambalo hupelekea maendeleo yasifikiwe kwa wakati lakini pia husababisha uadui kwani miongoni mwa pande zilizo katika mgogoro hupoteza mali, haki na hata maisha.”  Alisema.

Ametoa rai kwa Mawakili  wa Serikali na Wadau wote wa sheria, “ili kujitofautisha na majukwaa mengine sisi wajibu wetu ni kutatua kero siyo kupapasa, Wadau wote wa sheria lengo letu ni kushughulikia kero za wananchi na si kuwaacha waangukie mikononi mwa watu wengine wasio wataalam na mwisho wa yote hawawezi kutatua kero zao kwa ukamilifu.”

Aidha, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesema uanzishwaji wa Kliniki za sheria ni kutekeleza maelekezo ya Katiba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwatumikia wananchi lakini pia ni utiifu wa kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo amekuwa akiyatoa kwenye hotuba zake akikumbusha viongozi kushughulikia kero za wananchi kwa wakati. Migogoro isiposhughulikiwa kwa wakati itaishia kwenda mahakamani ambako kuna gharama ya muda, gharama za ushindani kwa sababu mahakamani ni pande mbili zinapigania haki.

Awali akitoa salaam katika hafla hiyo kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo amesema kupitia Sheria ya Huduma ya Msaada wa Kisheria wananchi wameendelea kuangaliwa kwa jicho la pekee katika mageuzi yanayofanywa nchini ya kuboresha huduma za sheria kwa kuzisogeza karibu zaidi na waliko wananchi ili kero zao ziweze kutatuliwa kwa wakati.

Ameshukuru Wadau walioitika wito kushiriki katika Kliniki hiyo kutatua kero za wananchi kwa haraka akizitaja kwa uchache Wizara ya Ardhi, Wizara ya Mambo ya Ndani na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum. “Sisi sote tumewekwa kwa lengo la kuwasasidia wananchi kwa dhamana ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kitu ambacho tunapaswa kuendelea kukifanya kwa vitendo.” Alisema.

Aidha, Bi. Makondo ameshukuru Serikali kwa kuendelea kuiwezesha Wizara na Taasisi zake katika kutekeleza majukumu mbalimbali ya kuwatumikia wananchi. Akitumia mfano wa Kampeni ya Msaada wa Sheria ya Mama Samia amesema Wizara kwa kushirikiana na Wadau wa haki imeendelea kutatua kero nyingi kwa wananchi hususan wa hali ya chini.

Vile vile, Bi. Makondo amesema Wizara imeendelea kuboresha mifumo mbalimbali ya TEHAMA ikiwemo mfumo wa Usajili Watoa Huduma za Msaada wa Kisheria na kuanzisha Kituo cha kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi kwa njia ya simu - Call centre.




Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA