MRADI WA BSAAT NA UBORESHAJI WA MFUMO WA HAKI JINAI NCHINI
William
Mabusi – WKS Morogoro
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya
Katiba na Ufuatiliaji Haki kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Beatrice
Mpembo amesema Wizara imeendelea kunufaika na Programu ya Kujenga Uwezo wa
Taasisi katika Kupambana na Rushwa Nchini (Building Sustainable Anti-Corruption
Action in Tanzania - BSAAT) kwa kutekeleza majukumu mbalimbali yanayohusu
kuboresha mfumo wa haki jinai nchini.
Bi. Mpembo amesema hayo
kwenye kikao cha tathmini ya mradi huo kwa kazi zilizofanywa kwa mwaka 2023/24,
tarehe 28 Juni, 2024 mjini Morogoro.
“Wizara ya Katiba na Sheria
ni moja ya Taasisi nufaika na mradi wa BSAAT, kupitia programu hiyo Wizara imeendelea
kutekeleza majukumu yanayohusu kuboresha mfumo wa haki jinai nchini ili uweze
kuwa na ufanisi na tija katika kushughulikia haki jinai nchini.” Amesema na
kuongeza;
“Wizara inatekeleza maeneo
matatu katika program hii, maeneo hayo ni Kuimarisha utambuzi wa viashiria vya
rushwa kwenye mfumo wa haki jinai vinavyolenga kupunguza motisha kwa watumishi
na kujihusisha na masuala ya rushwa; Mfumo wa haki jinai unaolinda na
kuharakisha haki za wahalifu, wahanga na mashahidi; Ushahidi wa mifumo mizuri
inayopelekea ubora na ufanisi wa uendeshaji mashauri.”
Kupitia mradi huo Wizara
imeanzisha Kituo cha Huduma kwa Mteja – Call Center kilichoanza kufanya kazi
mwezi Februari, 2024 kikiwa na lengo la kuboresha utoaji huduma kwa wananchi,
ikiwemo usikilizaji wa malalamiko yanayohusu rushwa kubwa na kuwasilisha rufaa
hizo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa ajili ya
uchunguzi. Wateja wanawasiliana na Kituo kwa kupiga simu namba 026 216 0360,
kutuma jumbe mbalimbali kupitia WhatsApp namba 0739101910 na e-mail malalamiko@sheria.go.tz.
Mbali na kufanyia kazi
masuala yanayohusu rushwa kubwa, kituo hicho pia kinapokea malalamiko
mbalimbali yanayohusu masuala ya kisheria na yasiyo ya kisheria na
kuyashughulikia ipasavyo.
Mradi huo umeanza
kutekelezwa nchini tangu mwaka 2017 ambapo ndani ya Wizara Mradi unatekelezwa
kupitia Idara ya Katiba na Ufuatiliaji Haki, Idara ya Sera na Mipango na
Kitengo cha TEHAMA.
Comments
Post a Comment