MWENYEKITI WA CCM WILAYA YA MAKETE ASISITIZA MATUMIZI YA KISWAHILI MAHAKAMANI

 

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Makete Ndg. Clement Ngajilo akiongea na wananchi wa kijiji cha Ipelele Kata ya Ipelele kwenye Mkutano wa Kampeni ya Mama Samia, Juni 2, 2024 Makete.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Makete Ndg. Clement Ngajilo (wa pili kulia) akisikiliza mada zilizokuwa zinatolewa wakati wa mkutano wa Kampeni ya Mama Samia uliofanyika kijiji cha Ipelele Kata ya Ipelele, Juni 2, 2024 Makete.

Wakili wa Serikali kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Zakaria Mzese (kushoto) akitoa huduma ya msaada wa kisheria kwa mkazi wa kijiji cha Ipelele, Juni 2, 2024 Makete.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxx

William Mabusi – WKS Makete

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Makete Ndg. Clement Ngajilo ameiomba Serikali kutumia lugha ya Kiswahili kwenye Mahakama ili lugha isiwe kikwazo kwa wananchi kupata haki zao.

Ndg. Ngajilo ameyasema hayo kwenye mkutano wa hadhara wakati wa kutekeleza Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mamam Samia uliokuwa unafanyika kijiji cha Ipelele Kata ya Ipelele Juni 2, 2024 Wilayani Makete.

“Wananchi wengi hawana uwelewa wa lugha za Mahakama na wanapopeleka kesi zao mahakamani hususan kwenye ngazi za juu zinazohitaji uwakilishi lugha inayotumika kwa sehemu kubwa huwa kikwazo hali inayopelekea wananchi kupoteza haki zao. Naomba sheria hizo kuboreshwa na itumike lugha mama yaani Kiswahili ili hata mwananchi asiye na uwezo wa kumsimamisha Wakili kutokana na changamoto ya rasilimali fedha aweze kusimama mwenyewe.” Alisema.

Akiongelea kuhusu hifadhi ya barabara yaani road reserve amesema kwa baadhi ya maeneo Serikali ilipima vipimo hivyo muda mrefu bila kuyatumia na kama wananchi hawajui juu ya vipimo vilivyopimwa huamua kufanya shughuli zao, baadaye Serikali inapotaka kuyatumia maeneo hayo wananchi wanaambiwa kuwa wameingia kwenye hifadhi ya barabara na kuambiwa watoke bila fidia, mwananchi anaanza kuona kero, hivyo ni busara Serikali kwa nyakati tofauti iwe na utamaduni wa kutoa elimu kwa wananchi kuwa ndani ya eneo la mita kadhaa hawaruhusiwi kujenga au kufanya shughuli zote za kibinadamu kuepusha usumbufu unaojitokeza.

Bw. Ngajilo amesema kwa vijiji ambavyo havikupitiwa na Kampeni wananchi wana haki ya kupeleka changamoto kwenye ofisi za Halmashauri zao na kuwaagiza watumishi wa Halmashauri wanaoshiriki kwenye Kampeni hiyo kutumia elimu waliyopata wakati wa maandalizi na hatimaye uzoefu wakati wa utekelezaji wa kampeni hiyo kuendelea kutatua kero za wananchi.

Mwisho wa hotuba yake ameshukuru Serikali kwa kutenga muda wa kutoa elimu ya sheria kwa jamii kwani jamii huko vijijini ina migogoro mingi na kwamba wana Makete ne wana Njombe wameipokea kampeni hiyo kwa mikono miwili akiomba iwe endelevu pale inapowezekana ili kuwaondolea shida wananchi.

Akiongea kwenye mkutano huo Bw. Omega Frank Fungo mkazi wa Kijiji cha Ipelele amesema “ni uamuzi mzuri kwa kiongozi wa nchi kutuma Wizara kusikiliza kero za wananchi, kuna sehemu nyingi hatukujua haki zetu lakini sasa tunajua na tutafanyia kazi elimu tuliyopata, sasa Ipelele mambo safi.”


Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA