TAKWIMU ZA MATUKIO MUHIMU YA KIBINADAMU ZIBORESHA UTOAJI WA HUDUMA ZA KIJAMII – DKT. CHANA
Mwenyekiti wa Bodi ya
Ushauri ya RITA Dkt. Amina Msengwa akitoa salaam za Bodi hiyo kwenye Kikao Kazi
cha kutathmini hali ya Utekelezaji wa Mpango wa Usajili wa Watoto wa Umri Chini
ya Miaka Mitano na kuzindua Taarifa ya kitakwimu ya usajili wa matukio muhimu
ya kibinadamu, Juni 25, 2024 Jijini Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana akizindua Taarifa ya Kitakwimu ya usajili wa
matukio muhimu ya kibinadamu, Juni 25, 2024 Jijini Dodoma.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
William Mabusi – WKS Dodoma
Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana ametoa wito kwa Taasisi za Serikali na Wadau wa
Usajili wa matukio muhimu ya kibinadamu kutumia Takwimu za matukio hayo kuboresha
utoaji wa huduma za kijamii kwa umma.
Dkt. Chana ametoa wito huo
alipokuwa anahutubia kufungua kikao kazi kilichoandaliwa na Wakala wa Usajili Ufilisi
na Udhamini – RITA kutathmini hali ya Utekelezaji wa Mpango wa Usajili wa Watoto
wa Umri Chini ya Miaka Mitano na kuzindua Taarifa ya kitakwimu ya usajili wa
matukio muhimu ya kibinadamu, Juni 25, 2024 Jijini Dodoma.
“Matokeo ya taarifa hii yatumiwe
vizuri na Taasisi za Serikali pamoja na wadau wa usajili wa matukio hayo kuboresha
utoaji wa huduma za kijamii kwa umma. Aidha, takwimu hizi zitumike kuwezesha uandaaji
wa mipango na mikakati mbalimbali ya kuendelea kuboresha usajili wa matukio hayo
ili kutoa takwimu bora zaidi katika maeneo ya usahihi, ukamilifu na usajili kwa
wakati.” Alisema.
Akitaja faida za usajili wa matukio
muhimu ya kibinadamu amesema kunasaidia kupata taarifa sahihi za idadi ya watu
ambazo ni muhimu katika kupanga mipango sahihi ya maendeleo kama programu za
chanjo kwa watoto, huduma za afya na huduma za elimu. Takwimu hizo pia
zinawawezesha viongozi wa ngazi zote kutoa huduma kwa kusaidia kutambua ni afua
gani zinahitajika katika kukabiliana na changamoto katika maeneo yao.
Amezitaja faida zingine kuwa
ni kuwawezesha watu kupata nyaraka muhimu za kisheria zinazoweza kulinda haki
zao za msingi na haki za binadamu kama kuwa na jina, kitambulisho cha taifa, huduma
za matibabu, elimu, uraia na kuwezesha huduma nyingine za msingi zinawafikia
wananchi kwa uwiano sawa.
Dkt. Chana alitumia hafla
hiyo kukumbusha azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan kuona watoto wote wa umri chini ya miaka mitano wamesajiliwa
ifikapo mwaka 2025 na wananchi wote wa Tanzania Bara wamesajiliwa na kupatiwa
vyeti vya kuzaliwa ifikapo mwaka 2030. Hivyo akatoa wito kwa RITA kuendelea
kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma zake zote na kuandaa mpango
kazi utakaoonesha jinsi itakavyoongeza usajili wa matukio yote muhimu ya
binadamu katika kulifikia lengo hilo.
Awali akitoa salaam za Bodi
ya Ushauri ya RITA na baadaye kumkaribisha Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Bodi hiyo
Dkt. Amina Msengwa amemhakikishia Waziri kuwa Bodi itaendelea kufuatilia na kuisimamaia
RITA katika kutekeleza majukumu yake ya usajili wa matukio muhimu ya kibinadamu
kwa kadri ya malengo ya Serikali.
Comments
Post a Comment