TUME YA KUREKEBISHA SHERIA YATAKIWA KUITUPIA JICHO SHERIA ZA USAFIRI WA ARDHINI
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe.
Balozi Dkt. Pindi Chana akihutubia wakati akifungua kikao kazi cha Kamisheni ya
Tume ya Kurekebisha Sheria, Juni 03, 2024 Morogoro.
Katibu Mtendaji Tume ya
Kurekebisha Sheria Tanzania Bw. George Mandepo akiongea wakat wa kikao kazi cha
Kamisheni ya Tume ya Kurekebisha Sheria, Juni 03, 2024 Morogoro.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe.
Balozi Dkt. Pindi Chana (katikati), wengine ni Mwenyekiti wa Tume ya
Kurekebisha Sheria Tanzania Mhe. Jaji Winfrida Beatrice Korosso (kushoto) na Katibu
Mtendaji Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania Bw. George Mandepo. Juni 03, 2024 Morogoro.
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
Na
Lusajo Mwakabuku & Bashiru Msangi - WKS Morogoro
Tume ya Kurekebisha Sheria
Tanzania imetakiwa kuangalia upya sheria za usafiri ardhini kwa kuzifanyia
mapitio na utafiti wa kina kwa kuwa zimeonekana kutodhibiti kikamilifu ajali za
barabarani ili ziweze kuwalazimisha wamiliki wa vyombo hivyo kuimarisha huduma
na kuwapunguzia kazi madereva kwa kuendesha mwendo mrefu kama hatua za
kupunguza ajali za barabarani.
Maelekezo hayo yametolewa leo
tarehe 03/06/2024 na Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Pindi Chana wakati akifungua
kikao kazi cha Kamisheni ya Tume hiyo ambacho kimefanyika Mkoani Morogoro
katika hoteli ya Morena kwa ajili ya
kupitia taarifa saba (7) za utafiti uliofanywa hivi karibuni.
Waziri huyo ameonesha masikitiko
yake jinsi ajali za barabarani hususan kwa mabasi yaendayo masafa marefu zinazotokana
na makosa yanayoweza kuzuilika zinavyopoteza maisha ya wananchi na
kuwasababishia ulemavu wa kudumu.
“Umefika wakati Tume ya
Kurekebisha Sheria Tanzania kufanya
utafiti na kuja na mapendekezo madhubuti
yatakayosaidia kuondoa ajali za barabarani ili kulinda afya na maisha ya
watanzania kwa kuwalazimisha wamiliki kuajiri dereva zaidi ya mmoja katika
chombo kimoja cha masafa marefu” alisema Waziri.
Mhe. Chana ameagiza Tume hiyo kushirikiana na wasimamizi wa sheria ya barabarani ili kutafuta suluhisho la kudumu la kuwalinda
wasafiri kwa usalama na kuhakikisha
wanafika kwa wakati, huku akiligusia swala la bima za maisha katika kuwasidia
waathirika.
“Sisi kama wabobevu wa sheria
lazima tuangalie kama kampuni inapata ajali za mara kwa mara waachane na
biashara ya kusafirisha watu na badala yake wasafirishe mizigo.” alisema
Aidha, ameendelea kueleza
kwamba Tume ya Kurekebisha Sheria kupitia Wizara ya Katiba na Sheria ambao ndio
wenye dhamana hazipotayari kuona wananchi wakipoteza maisha kila kukicha.
Waziri Chana pia ameitaka Tume
ya Kurekebisha Sheria wasisubiri kuletewa kazi za utafiti au mapitio kama ilivyo sasa na badala yake wafanye
kulingana na wanavyoona hali halisi na
wanayoyapata wakati wa utafiti.
Hata hivyo Mhe. Waziri aleeza
kufarijika kwake na utekelezaji wa mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai
yanayofanywa na Tume hiyo ambazo ni Taarifa ya Mapitio ya Mfumo wa Sheria zinazosimamia
Makosa ya Uhujumu Uchumi na Uhalifu wa Kupangwa Nchini; Taarifa ya Tathmini ya
Utekelezaji wa Kifungu cha 91(3) cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai;
Utekelezaji mwingi umekuwa katika Taarifa ya Tathmini ya
Utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Mashahidi na Watoa Taarifa; Taarifa ya Mapitio ya Mfumo wa Sheria
Zinazosimamia Dhamana; na Taarifa ya Mapitio ya Sheria Zinazosimamia
Adhabu ya Viboko Mahakamani na Katika Magereza.
Awali akimkaribisha Waziri
huyo Jaji wa Mahakama ya Rufani, Winfrida Beatrice Korosso, ambaye ni Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria
Tanzania, alieleza kwamba Kikao cha Kamisheni ya Tume ya Kurekebisha Sheria
Tanzania ni Kikao cha 94 toka Tume hiyo kuanzishwa ambapo Tume, inatekeleza
wajibu wake ipasavyo kwa kuhakikisha vikao vyote vya Kisheria vinafanyika hususan baada ya utafiti na mapitio ya kitaaluma.
Aidha, alieleza kwamba Taarifa
zilizokamilishwa na Sekretariati ya Tume
baada ya kufanyika Mapitio, Utafiti na Tathmini katika nyanja mbalimbali za sheria ni Taarifa
ya Mapitio ya Mfumo wa Sheria Zinazosimamia Uhujumu Uchumi na Uhalifu wa Kupangwa
Nchini na Taarifa ya Tathmini ya Utekelezaji wa Kifungu cha 91(3) cha Sheria ya
Mwenendo wa Mashauri ya Jinai Kuhusu Uondoshaji wa Mashauri Mahakamani.
Pia taarifa ya Tathmini ya
Utekelezaji wa Sheria ya Ulinzi wa Mashahidi na Watoa Taarifa; Taarifa ya
Tathmini ya Utekelezaji wa Sheria Zinazosimamia Usafiri Ardhini; Taarifa ya
Mapito ya Mfumo wa Sheria Zinazosimamia Dhamana; Taarifa ya Mapitio ya Sheria
Zinazosimamia Adhabu ya Viboko Mahakamani na Magereza;naTaarifa ya Tathmini ya
Utekelezaji wa Sheria Zinazosimamia Hakimiliki na Hakishiriki.
Comments
Post a Comment