WANANCHI MAKETE WALALAMIKIA FIDIA UHARIBIFU WA WANYAMAPORI

 

Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bw. Richard Jacopio akiwasilisha mada ya sheria kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Ivalalila Kata ya Iwawa, Mei 31, 2024 Makete.


Afisa Wanyamapori kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Bw. Francis Malembo akiwasilisha mada ya Sheria ya uhifadhi wa wanyamapori kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Ivalalila Kata ya Iwawa, Mei 31, 2024 Makete.

Afisa Msajili Msaidizi RITA Wilaya ya Kyela Bi. Nenduvotho Loy akiwasilisha mada ya Wosia, Mirathi, Usajili wa Vizazi na Vifo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Ivalalila Kata ya Iwawa, Mei 31, 2024 Makete.

xxxxxxxxxxxxxxxxx

William Mabusi – WKS Makete

Wananchi Wilayani Makete wameiomba Serikali kuongeza fidia inayotolewa kwa wananchi wanaojeruhiwa au kupata ulemavu wa kudumu, familia iliyopoteza ndugu kwa kuuliwa au kuharibiwa mazao na wanyamapori, kwani kiwango cha sasa hakikidhi uharibifu wa wanyamapori hao.

Malalamiko hayo yametolewa na wananchi wa kijiji cha Ivalalila Kata ya Iwawa Halmashauri ya Wilaya ya Makete Mei 31, 2024 kwenye Mkutano wa hadhara baada ya mada mbalimbali kutolewa ikiwemo ya Sheria ya uhifadhi wa wanyamapori ikiwa ni utekelezaji wa kampeni ya kutoa huduma ya msaada wa kisheria ya Mama Samia inayoendelea kutekelezwa kwenye Halmashauri zote Sita mkoani Njombe.

Bw. Amua Mahenge mkazi wa kijiji cha Ivalalila alisema, ”fidia ya uharibifu wa Wanyamapori ni ndogo ukilinganisha na gharama tunazoingia wakulima wakati wa kilimo. Kwa mfano kwenye heka moja tunatumia mifuko mitatu ya mbolea yenye thamani ya zaidi ya shilingi elfu sabini na nne (74,000/-) kwa mfuko mmoja sawa na shilingi 222,000 na hiyo ni gharama ya mbolea tu, halafu  fidia ya Serikali ni sh 100,000 kwa heka iliyoharibiwa na wanyamapori.”

Aidha, wananchi hao walionesha kutoridhishwa kwao kwa fidia ya shilingi laki tano kwa mtu aliyejeruhiwa na mnyamapori na kusababishiwa ulemavu wa kudumu, ila mtu akithibitika kamuua mnyama hukumu yake ni kifungo cha miaka isiyopungua ishirini na isiyozidi thelathini.

Akijibu swali hilo, Afisa Wanyamapori kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) Bw. Francis Malembo amesema viwango vya fidia kutokana na uharibifu wa wanyamapori vimelalamikiwa hata maeneo mengine na Serikali inafanyia kazi marekebisho ya viwango vya fidia, ingawa kwa sasa viwango vya zamani vya kifuta machozi na jasho vya mwaka 2011 vitaendelea kutumika.

Naye Bw. Nowadi Mbilinyi mkazi wa Ivalalila akichangia mada hiyo ameomba TAWA kuruhusu njia ya mkato kwa wananchi kutoka Ivalalila kwenda Kigala Kata ya Kigala  kupitia Pori la akiba la Mpanga Kipengele kwani pori hilo halina wanyama wakali wa kudhuru binadamu.


Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA