HUDUMA ZA MSAADA WA KISHERIA ZINAPATIKANA SABASABA BILA MALIPO

 

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini (kushoto) akimsikiliza  Wakili wa Serikali Mkuu  Candid Nasua kutoka Wizara ya Katiba na Sheria,  akimpa tathmini  kuhusu hali ya utoaji wa huduma za Kisheria na huduma mbalimbali kwa Wananchi wanaotembelea banda hilo. Julai 5, 2024 Dar es Salaam.

Baadhi ya Wananchi wakiwa katika banda la Wizara ya Katiba na Sheria kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali kwenye Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Julai 5, 2024 jijini Dar es Salaam.

xxxxxxxxxxxxxx

Hyasinta Kissima – WKS Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini ametaka Wananchi wanaofika katika Maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) kutembelea katika banda la Wizara ya Katiba na Sheria ili  kutapa huduma mbalimbali ikiwemo Msaada wa Kisheria.

Naibu Waziri Sagini ameyasema hayo Julai 5, 2024 jijini Dar es Salaam  wakati alipotembelea banda la Wizara  kuangalia hali ya upatikanaji wa huduma hizo kwa  Wananchi wanaotembelea banda hilo.

"Wapo Wananchi wanatoka katika maeneo mbalimbali Nchini na wengi kutokea jijini Dar es Salaam  na wanahitaji msaada wa kisheria. Niwasihi sana kufika katika banda la Wizara ya Katiba na Sheria na kupata huduma hizi bure. Wizara imejizatiti kuhakikisha kuwa kila Mwananchi atakayetembelea katika banda na mwenye shida atapata huduma. Wapo Mawakili wa Serikali, Wanasheria  wenye weledi na ambao wapo tayari kuhakisha kuwa haki kwa kila Mtanzania inatendeka." Alisema Naibu Waziri Sagini.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti tofauti, baadhi ya Wananchi waliofika katika banda  la Wizara ya Katiba na Sheria akiwemo  Johnson Msemwa na Katarina Mpangilye  wameonesha kufurahishwa na uwepo wa huduma hizo viwanjani hapo jambo ambalo limewawezesha kupata ushauri kuhusu masuala  ya kisheria yaliyokuwa yakiwakabili.

“Nilikuwa nina changamoto kuhusu malezi ya watoto mara baada ya kutengana na mzazi mwenzangu. Nimefika katika banda hili la Katiba na Sheria nimepata elimu ya kutosha na Wataalamu wamenisaidia kufanya mawasiliano na mzazi mwenzangu na kupanga namna ya kuweza kufikisha huduma za matunzo kwa watoto.” Alisema mama mmoja ambaye hakupenda jina lake litajwe.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma za Msaada wa Kisheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Ester Msambazi amesema kuwa mpaka sasa Kampeni hiyo imeshafika katika mikoa 7 na kufikia zaidi ya Wananchi   495,000 wakiwemo Wanawake, Wanaume na Watoto na wengi wamenufaika kwa kupata elimu, ushauri na utatuzi wa migogoro yao.

Wizara ya Katiba na Sheria katika Maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara itaendelea kutoa huduma mbalimbali na kutatua changamoto mbalimbali za Wananchi ikiwemo migogoro ya Ardhi, Ndoa, Mirathi, ukatili wa kijinsia.



Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA