SAGINI AKOSHWA NA UBUNIFU WA MAHAKAMA KATIKA KUWATUMIKIA WANANCHI

 

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini (kulia), Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel wakiwa katika nyuso za furaha mara baada ya kumalizika kwa mazungumzo baina yao ambayo awali yalitanguliwa na  kutembelea jengo kuu la Mahakama ya Tanzania Tambukareli jijini Dodoma, Julai 11, 2024.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akimwelezea Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini kuhusu utendaji kazi wa kituo cha huduma kwa mteja cha Mahakama kilichopo Tambukareli jijini Dodoma, Julai 11, 2024.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini (Kulia), Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel wakiwa wamesimama mbele ya Ukumbi wa Mahakama namba mbili, ambao utatumika kwa ajili ya kusikiliza kesi mbalimbali pindi utakapomalizika. Julai 11, 2024 Dodoma.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Hyasinta Kissima, WyKS Dodoma

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini Julai 11, 2024 jijini Dodoma, amekutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel, ikiwa ni mwendelezo wa ziara ya kuzitembelea na kujifunza majukumu ya Taasisi   zilizopo chini ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Katika mazungumzo hayo  yaliyotanguliwa na kulitembelea jengo la Makao Makuu ya Mahakama yaliyopo Tambukareli jijini Dodoma, Naibu  Waziri amefurahishwa na maboresho  makubwa yaliyofanywa na  Mhimili wa  Mahakama ikiwemo ujenzi wa jengo la Mahakama lenye Teknolojia na vifaa  vya kisasa ambalo litakuwa miongoni mwa majengo makubwa sita bora Duniani lenye thamani ya Shilingi Bilioni 129.7 fedha kutoka mapato ya ndani ya Serikali.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel amesema kuwa, maboresho yanayofanywa katika Mhimili wa Mahakama kama vile upatikanaji wa vifaa vya kisasa, rasilimali watu, ujenzi wa miundombinu ya kisasa, matumizi ya TEHAMA, yameleta mchango mkubwa katika ubora wa utoaji haki  Nchi na imani ya Wananchi kwa Mahakama imeongezeka maradufu.

"Nilipopewa jukumu la kumsaidia Mhe. Waziri Dkt. Balozi Pindi Chana katika Wizara ya Katiba na Sheria, nilisema lazima nijue hiki ninachoenda kukifanya.Tunapokea ripoti mbalimbali na tunazisoma. Lakini, ningeishia kwenye ripoti  pekee bila kufika katika jengo hili  na nimetembelea jengo hili sura ni tofauti kabisa.” Alisema Sagini.

Aliendelea kusema, "Nimeona makubwa kwenye TEHAMA. Jaji Mkuu aliniambia uje utembelee kwa kweli  mna maajabu. Ninaweza kuona taarifa ya Mahakama ya Mkoa fulani, inafanya nini, shauri gani limepangwa kusikilizwa, mashahidi au hukumu inatolewa kwamba hiyo taarifa ninaweza kuipata hapa. Lakini malalamiko ya Wananchi kituo cha huduma kwa mteja kwamba kutakuwa na watu masaa 24 kusikiliza kero za Wananchi, na kuzitafutia masuluhisho, huu ni ubunifu mkubwa sana. Niwapongeze Mahakama kwa dhati ya moyo wangu kuwa mmefanya ubunifu katika kuwatumikia Wananchi."

Naibu Waziri Sagini amemshukuru Rais wa wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuja na wazo la ujenzi wa jengo la Mahakama 2012, kutambua jitihada za Hayati  Dkt. John Pombe Magufuli kwa  kuanza ujenzi 2020 na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan 2021 kuendeleza ujenzi kwa kasi na  kukubali kotoa fedha zote mpaka kufikia hatua  hiyo.

Naibu Waziri Sagini amesema kuwa, Wizara ya Katiba na Sheria inaimani na kazi kubwa inayofanywa na Mahakama na itaendelea kushirikiana nao na kuisemea Mahakama katika majukwaa mbalimbali na pia kuitumia Mahakama kupitia maboresho yaliyofanyika kuwa sehemu ya eneo la kujifunza kwa Taasisi mbalimbali zilizopo chini ya Wizara na zinazohusika katika utoaji wa Haki kwa Wananchi.



Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA