TUISHAURI SERIKALI TUSIKAE KIMYA - SAGINI

 

Naibu Waziri wa Katiba  na Sheria Mhe. Jumanne Sagini akizungumza na Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (hawapo pichani) Julai 2, 2024 wakati alipowatembelea jijini Dodoma kwa lengo la kujitambulisha na kufahamu majukumu yao.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Prof. Kennedy Gastorn akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ofisi hiyo kwa Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini, Julai 2, 2024 Jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Dkt. Khatibu Kazungu akizungumza na Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (hawapo pichani) Julai 2, 2024 jijini Dodoma.

Kikao cha Menejimenti ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja  na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Julai 2, 2024  jijini Dodoma.

Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakimsikiliza Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini alipowatembelea jijini Dodoma Julai 2, 2024.

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Hyasinta Kissima - WKS Dodoma

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini ameipongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuendelea kusimamia  jukumu lake la msingi la kuishauri Serikali katika masuala yote ya Kisheria ndani na Nje ya Nchi ambapo ameelekeza Ofisi hiyo kuendelea kusimamia haki, uadilifu na kuishauri Serikali kwa hekima na heshima.

Naibu Waziri Sagini aliyasema hayo Julai 2, 2024  jijini Dodoma, wakati akizungumza katika kikao na Menejimenti na Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mhe. Sagini amesema kuwa  katika uandaaji wa Sheria inapoonekana kunaweza kuibuka ukakasi katika utekelezaji wake ni  vyema Ofisi hiyo ikatoa taarifa mara moja kwa Viongozi na kushauri ipasavyo   ili kuzuia madhara kwa Serikali na Wananchi.

"Ninyi ni Taasisi ya Kikatiba. Tunaona jitihada kubwa zinazofanywa katika kuimarisha msaada wa Kisheria ikiwa ni pamoja na kuendelea kusimamia nidhamu ya Mawakili wa kujitegemea kwani wapo ambao wanawaonea Wananchi. Panapotokea jambo ambalo mnaona Kisheria linaweza kuleta maneno ni vyema mkaliwasilisha na mkatumia taaluma yenu kushauri badala ya kukaa kimya. Mnafanya kazi kubwa sana endeleeni kutimiza wajibu wenu  kwa maslahi makubwa ya Nchi yetu na pia endeleeni kuimarisha umoja na mshikamano pahala pa kazi." Alisema Naibu Waziri Sagini.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Dkt. Khatibu Kazungu amesema kuwa, Wizara kwa sasa imeanza kuandaa maandiko ya miradi mbalimbali ikiwemo mradi wa kuwajengea uwezo Wanasheria ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na moja kati ya mambo yaliyokusudiwa kupitia mradi huo ni kuimarisha utendaji kazi  wa Wanasheria katika maeneo mbalimbali yanayoibuka kwenye taaluma hiyo na ambayo mara nyingi hayapatikani katika Vyuo hapa Nchini.

Awali akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Ofisi hiyo kwa Naibu Waziri, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Prof. Kennedy Gastorn amesema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kipindi cha mwaka 2023/2024, imepata mafanikio kadha wa kadha ikiwa ni katika  kufanikisha Urekebu wa Sheria kuu 446 ili toleo la Sheria lililofanyiwa urekebu kwa mwaka 2023 liweza kutoka, kufanya tafsiri ya Sheria 300, kuhakiki Sheria ndogo 1228, kufanya upekuzi kwa hati za makubaliano 34, kutoa maoni 1707 kwenye Wizara na Taasisi na kufanikisha miswada 19 iliyoandaliwa ambapo miswada 17 ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Sheria.





Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA