WIZARA YA YASHIRIKI KATIKA UZINDUZI WA MAONESHO YA KIBIASHARA YA SABASABA

 

xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Hyasinta Kissima – WKS Dar es Salaam

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini Julai 3, 2024 ameiwakilisha Wizara katika uzinduzi wa Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba yaliyofunguliwa rasmi  na Rais wa Msumbiji, Mhe. Filipe Jacinto Nyusi  akiambatana na mwenyeji wake  Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika uzinduzi wa Maonesho hayo yaliyofanyika katika viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa kampuni zaidi ya 11 Nchini zimeanza kunufaika na ufanyaji wa biashara katika Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA).

"Serikali itaendelea kutatua changamoto za Wafanyabiashara na katika Wizara milango ipo wazi kwa ajili ya kuwasikiliza." Alisema  Rais Samia.

Katika hatua nyingine Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii  Mhe.  Angellah Kairuki (Mb) aliongozana na Mhe. Sagini, Mhe. Chiwelesa pamoja na viongozi wengine kutembelea banda la  Wizara ya Maliasili na Utalii.

Katika kutembelea banda la Wizara ya Maliasili na Utalii, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini (Mb), ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa ubunifu wa kuyaalika makabila mbalimbali likiwemo kabila la Wazanaki  lililopo  katika wilaya ya Butiama mkoani Mara.

"Jambo lililonifurahisha zaidi ni kukutana na kabila la Wazanaki katika maonesho haya ya Kimataifa ya  kibiashara. Kupitia tamaduni hizi tunazozioana hapa za Wazanaki  ikiwemo kusaga kwa kutumia jiwe, vitanda na nyumba zilizokuwa zikitumika zinatukumbusha tulipotoka na kuona mambo ambayo walikuwa wanayafanya Wazee wetu. Niwaombe watu wafike kujifunza mema ya kabila la Wazanaki katika banda la Wizara ya Maliasili na Utalii." Alisema Sagini.

Ikumbukwe kuwa katika Maonesho hayo, Wananchi mbalimbali kutoka nje na ndani ya  Nchi hupata fursa ya kuonesha  shughuli zao jambo ambalo husaidia kukuza uchumi, ajira na kuongeza mapato ya Serikali. 


Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA