WOTE TUNA HAKI SAWA TUWAJALI WENYE MAHITAJI MAALUM – MAKONDO





Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo akisoma hotuba ya uzinduzi katika ukumbi wa American Corner uliopo Makumbusho ya Taifa Jijini Dar es salaam akimwakilisha Waziri wa Katiba na Sheria, Julai 12, 2024.

Baadhi ya wajumbe na washiriki wa uzinduzi wa Mradi wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala kwa watu wenye ulemavu, Julai 12, 2024 Jijini Dar es salaam.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo akizindua rasmi Mradi wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala kwa watu wenye ulemavu, Julai 12, 2024 Dar es Salaam.

Erick Mukiza, Mkurugenzi Mtendaji wa ESS Creative & Legal Foundation (ESS) akielezea malengo ya kuanzisha Mradi wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala kwa watu wenye ulemavu, Julai 12, 2024 Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Board ya ESS Creative & Legal Foundation (ESS) Dkt. Elly Ndyetabula akitoa salamu za ukaribisho kwa Mgeni Rasmi. Julai 12, 2024 Dar es Salaam.


xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

Na Lusajo Mwakabuku – WyKS Dar es salaam.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Bi. Mary Makondo amewataka Watanzania kwa ujumla kuwajali na kuwapa huduma zinazostahili watu wenye ulemavu kwani nao wana haki sawa katika jamii pamoja na kwamba ni kundi linalosahaulika katika masuala mbalimbali ya kijamii.

Bi. Makondo ameyasema hayo leo tarehe 12/07/2024 katika ukumbi wa American Corner uliopo Makumbusho ya Taifa Jijini Dar es salaam akimwakilisha Waziri wa Katiba na Sheria kama Mgeni Rasmi katika Hafla ya Uzinduzi wa Mradi wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala kwa watu wenye ulemavu.

Akisoma hotuba yake katika hafla hiyo, Bi. Makondo alisema sisi wote ni watu wenye mahitaji maalum watarajiwa sababu huwezi kujua kesho kitakupata kitu gani ndio maana ukiwaona hawa ujue wewe ni sehemu yao na kusisitiza kuwa ni lazima tuwahudumie kwa upendo na maadili.

“Matarajio ya Wizara ya Katiba na Sheria na Serikali kwa ujumla katika kushiriki kwenu katika mradi huu ni pamoja na kuwa kichocheo katika kusimamia na kutatua migogoro na kupunguza idadi ya kesi kupitia upatanishi hivyo kuimarisha juhudi za Serikali kupunguza mrundikano wa kesi Mahakamani, na  kushauri Serikali na taasisi zake wakiwemo viongozi katika ngazi mbalimbali za kushughulikia na kutatua migogoro kwa watu wenye ulemavu.” Alisema Bi. Makondo.

Makondo ametoa rai kwa wahusika kuhakikisha wanafuata kanuni za maadili za upatanisho wa migogoro kwa kuwa na tabia na mwenendo unaohakikisha haki, uadilifu, usiri, uwajibikaji na usawa.

“Tumesikia wakati dada akitoa shuhuda pale alisema kwamba anawashukuru wanasheria kwa kuendelea kuwa waadilifu kwa hiyo tuendelee kuwa waadilifu na kujali wengine na kuzingatia kwamba ulinzi wa haki ya mtu mwingine ni jukumu lako,” aliongeza.

Akielezea mradi huo, Erick Mukiza, Mkurugenzi Mtendaji wa ESS Creative & Legal Foundation (ESS) amesema lengo la kuanzisha mradi huo limetokana na tafiti mbalimbali katika bara la Afrika ambazo zimeonesha kuwa utatuzi wa migogoro bila kwenda Mahakamani imewasaidia wanawake wengi  kuweza kupata haki zao, lakini kwa upande wa Tanzania, watu wenye ulemavu hususan wenye ulemavu wa kusikia wameachwa nyuma hasa katika suala la kupata taarifa na faida za Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala.

“Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala (Altenative Disputes Resolutions - ADR) umeonekana kuwa njia bora zaidi na ya gharama nafuu katika kutatua migogoro nje ya shauri la Mahakama ikiwa ni pamoja na kuilinda amani kupitia upatanisho unaopatikana nje ya vifungu vya kisheria kama ambavyo Jaji Mkuu na Rais wa Tanzania wameelezea katika matukio tofauti tofauti.” Alisema Bwana Mukiza.

Awali akitoa salamu za ukaribisho kwa Mgeni Rasmi, Mwenyekiti wa Board ya ESS Creative & Legal Foundation (ESS) Dkt. Elly Ndyetabula alisema, “kutatua migogoro kwa njia mbadala inaokoa muda lakini pia inaendeleza mahusiano, tunakuwa na urafiki kwa sababu migogoro inatatuliwa kwa maridhiano.”



Comments

Popular posts from this blog

USAJILI WA VIZAZI NA VIFO NI TAKWA LA KISHERIA

TUFANYE KAZI KWA UADILIFU NA USHIRIKIANO - MHE CHANA